Zaburi 21:1-13
Kwa kiongozi. Muziki wa Daudi.
21 Ee Yehova, mfalme hushangilia kwa sababu ya nguvu zako;+Jinsi anavyoshangilia sana kwa sababu ya matendo yako ya wokovu!+
2 Umetosheleza tamaa ya moyo wake,+Nawe hujamnyima ombi la midomo yake. (Sela)
3 Kwa maana unamlaki kwa baraka tele;Unamvika taji la dhahabu bora* kichwani.+
4 Alikuomba uhai, nawe ukampa,+Maisha marefu,* milele na milele.
5 Matendo yako ya wokovu humletea utukufu mkubwa.+
Unamtunukia adhama na fahari.
6 Unamfanya awe na baraka milele;+Unamfanya afurahi kwa shangwe ya kuwa mbele zako.*+
7 Kwa maana mfalme anamtumaini Yehova;+Kwa sababu ya upendo mshikamanifu wa Aliye Juu Zaidi, hatatikiswa kamwe.*+
8 Mkono wako utawapata maadui wako wote;Mkono wako wa kuume utawapata wale wanaokuchukia.
9 Utawafanya wawe kama tanuru lenye moto mkali utakapofika wakati ulioweka wa kuwakazia uangalifu.
Yehova atawameza kwa hasira yake, na moto utawateketeza kabisa.+
10 Utawaangamiza wazao wao kutoka duniani,Na uzao wao kutoka kati ya wanadamu.
11 Kwa maana walikusudia kukutendea maovu;+Wamepanga njama ambazo hazitafanikiwa.+
12 Kwa maana utawafanya wakimbie+Kwa kuwalenga* kwa upinde wako.*
13 Inuka, Ee Yehova, katika nguvu zako.
Tutauimbia sifa* uwezo wako.
Maelezo ya Chini
^ Au “iliyosafishwa.”
^ Tnn., “Urefu wa siku.”
^ Tnn., “mbele za uso wako.”
^ Au “hatapepesuka (hatayumbayumba) kamwe.”
^ Tnn., “kulenga nyuso zao.”
^ Tnn., “kamba zako za upinde.”
^ Tnn., “Tutauimbia na kuupigia muziki.”