Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 113

Somo Kuhusu Bidii​—Talanta

Somo Kuhusu Bidii​—Talanta

MATHAYO 25:14-30

  • YESU ATOA MFANO WA TALANTA

Yesu akiwa bado na mitume wake wanne kwenye Mlima wa Mizeituni, anawasimulia mfano mwingine. Siku chache zilizopita, alipokuwa Yeriko, alitoa mfano kuhusu mina ili kuonyesha kwamba Ufalme utakuja baadaye, wakati ujao. Mfano anaosimulia sasa una mambo kadhaa yanayofanana na mfano huo. Ni sehemu ya jibu lake kwa swali kuhusu kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo. Unakazia kwamba lazima wanafunzi wake wafanye kwa bidii kazi anayowakabidhi.

Yesu anaanza hivi: “Ni kama mtu aliye karibu kusafiri ng’ambo, aliyewaita watumwa wake na kuwakabidhi mali zake.” (Mathayo 25:14) Kwa kuwa tayari Yesu alikuwa amejilinganisha na mtu fulani aliyesafiri kwenda ng’ambo ‘kupokea mamlaka ya kifalme,’ mitume wanaweza kuelewa kwamba Yesu ndiye “mtu fulani” anayezungumziwa sasa.—Luka 19:12.

Kabla mtu anayezungumziwa kwenye mfano huo hajasafiri kwenda ng’ambo, anawakabidhi watumwa wake vitu vyake vyenye thamani. Katika kipindi cha miaka mitatu na nusu cha huduma yake, Yesu alikazia fikira kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu, na kuwazoeza wanafunzi wake kufanya kazi hiyo. Sasa anaondoka akiwa na uhakika kwamba wataendelea kufanya kazi aliyowazoeza kufanya.—Mathayo 10:7; Luka 10:1, 8, 9; linganisha na Yohana 4:38; 14:12.

Katika mfano huo, mtu huyo anagawa mali zake jinsi gani? Yesu anasema hivi: “Akampa mmoja talanta tano, mwingine mbili, na mwingine moja, kila mtumwa kulingana na uwezo wake, kisha akaenda ng’ambo.” (Mathayo 25:15) Watumwa hao watafanya nini na mali waliyokabidhiwa? Je, watafanya kazi kwa bidii na kumletea bwana wao faida? Yesu anawaambia hivi mitume wake:

“Mara moja yule aliyepokea talanta tano akaenda kufanya biashara nazo, akapata talanta tano zaidi. Vivyo hivyo, yule aliyepokea mbili akapata talanta mbili zaidi. Lakini mtumwa aliyepokea moja tu akaenda akachimba shimo ardhini na kuficha zile pesa za bwana wake.” (Mathayo 25:16-18) Ni nini kitakachotokea bwana wao atakaporudi?

Yesu anaendelea kusema hivi: “Baada ya muda mrefu, bwana wa watumwa hao akarudi na kufanya hesabu nao.” (Mathayo 25:19) Wale wawili wa kwanza walifanya yote waliyoweza, “kila [mmoja] kulingana na uwezo wake.” Kila mtumwa alifanya kazi kwa bidii sana na kupata faida kutokana na kile alichokabidhiwa. Yule aliyepokea talanta tano alizalisha talanta tano nyingine, na aliyepokea talanta mbili alifanya vivyo hivyo. (Nyakati hizo, mfanyakazi angefanya kazi kwa miaka 19 ili apate kiasi kinacholingana na talanta moja.) Bwana wao anawapongeza hivi wote wawili: “Vema, mtumwa mwema na mwaminifu! Umekuwa mwaminifu katika mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi. Ingia katika shangwe ya bwana wako.”—Mathayo 25:21.

Hata hivyo, mambo ni tofauti kwa mtumwa aliyepokea talanta moja. Anasema hivi: “Bwana nilijua wewe ni mtu mgumu, ambaye huvuna mahali ambapo hukupanda na kukusanya mahali ambapo hukupepeta. Kwa hiyo, niliogopa nikaenda na kuficha talanta yako ardhini. Chukua mali yako.” (Mathayo 25:24, 25) Hata hakuweka pesa hizo benki ili kupata angalau faida kidogo kwa ajili ya bwana wake. Badala yake amemletea bwana wake hasara.

Kwa kufaa, bwana wake anamwita “mtumwa mwovu na mvivu.” Kile alicho nacho kinachukuliwa na kupewa mtumwa aliye tayari kufanya kazi kwa bidii. Bwana anaweka kanuni hii: “Kila mtu aliye na kitu ataongezewa, naye atakuwa na vitu vingi. Lakini mtu asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.”—Mathayo 25:26, 29.

Wanafunzi wa Yesu wana mambo mengi ya kufikiria, hata kuhusu mfano huu. Wanaweza kutambua kwamba kazi ambayo Yesu anawakabidhi ni yenye thamani sana, yaani, pendeleo kubwa la kufanya wanafunzi. Naye anatarajia wafanye kazi hiyo kwa bidii. Yesu hafikirii kwamba lazima wote watimize kiwango kilekile wanapofanya kazi ya kuhubiri ambayo amewaagiza wafanye. Kama alivyofafanua, kila mmoja anapaswa kufanya yote anayoweza “kulingana na uwezo wake.” Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba Yesu atafurahi ikiwa mtu atakuwa “mvivu” na kukosa kujitahidi kabisa kuendeleza mali za Bwana.

Hata hivyo, lazima mitume wanafurahi sana wanapohakikishiwa hivi: “Kila mtu aliye na kitu ataongezewa”!