Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 112

Somo Kuhusu Kuwa Macho​—Mabikira

Somo Kuhusu Kuwa Macho​—Mabikira

MATHAYO 25:1-13

  • YESU ATOA MFANO WA MABIKIRA KUMI

Yesu amekuwa akijibu maswali ya mitume wake kuhusu ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo. Akiwa na jambo hilo akilini, sasa anawapa himizo lenye hekima kwa kutumia mfano mwingine. Wale wanaoishi wakati wa kuwapo kwake wangeona utimizo wa mfano huo.

Anaanza kusimulia mfano huo hivi: “Ufalme wa mbinguni ni kama mabikira kumi waliochukua taa zao na kwenda kumpokea bwana harusi. Watano kati yao walikuwa wapumbavu, na watano walikuwa wenye busara.”—Mathayo 25:1, 2.

Yesu hamaanishi kwamba nusu ya wanafunzi wake wanaorithi Ufalme ni wapumbavu na nusu nyingine ni wenye busara. Badala yake, anamaanisha kwamba kuhusiana na Ufalme, kila mwanafunzi wake ana uwezo wa kuchagua kuwa macho au kukengeushwa. Hata hivyo, Yesu hana shaka kwamba kila mtumishi wake anaweza kuendelea kuwa mwaminifu na kupokea baraka kutoka kwa Baba yake.

Katika mfano huo, mabikira wote kumi wanaenda kumpokea bwana harusi na kujiunga na msafara wa harusi. Atakapowasili, mabikira watamwangazia njia kwa taa zao, wakimsifu anapomleta bibi harusi katika nyumba aliyotayarishiwa. Hata hivyo, hali inakuwaje?

Yesu anaeleza hivi: “Wale wapumbavu walibeba taa zao lakini hawakubeba mafuta, lakini wale wenye busara walibeba mafuta kwenye chupa zao pamoja na taa zao. Bwana harusi alipokawia kuja, wote walisinzia na kulala.” (Mathayo 25:3-5) Bwana harusi hafiki mapema kama ilivyotarajiwa. Inaonekana anachelewa sana, nao mabikira wanalala usingizi. Mitume wanaweza kukumbuka kwamba Yesu aliwasimulia kuhusu mwanamume fulani kutoka familia mashuhuri aliyesafiri na ‘mwishowe akarudi baada ya kupokea mamlaka ya kifalme.’—Luka 19:11-15.

Katika mfano wa mabikira kumi, Yesu anafafanua kile kinachotokea mwishowe bwana harusi anapowasili: “Katikati ya usiku kukatokea mwito, ‘Huyu hapa Bwana harusi! Nendeni mkamlaki.’” (Mathayo 25:6) Hali ya mabikira ikoje kuhusu kuwa tayari na kuwa macho?

Yesu anaendelea kusema: “Ndipo mabikira wote wakasimama na kuzitayarisha taa zao. Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, ‘Tugawieni mafuta yenu, kwa sababu taa zetu zinakaribia kuzimika.’ Wale wenye busara wakawajibu: ‘Labda hayatatutosha sisi sote. Nendeni kwa wauzaji mkajinunulie.’”—Mathayo 25:7-9.

Basi wale mabikira watano hawako macho na hawako tayari kwa ajili ya kuwasili kwa bwana harusi. Hawana mafuta ya kutosha kwa ajili taa zao nao wanahitaji kuyatafuta. Yesu anasimulia hivi: “Walipokuwa wakienda kununua mafuta, bwana harusi akaja. Mabikira waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya ndoa, na mlango ukafungwa. Baadaye wale mabikira wengine pia wakaja, wakisema, ‘Bwana, Bwana, tufungulie!’ Akawajibu, ‘Kwa kweli ninawaambia, siwajui ninyi.’” (Mathayo 25:10-12) Hayo ni matokeo mabaya sana ya kutoendelea kuwa macho na kutokuwa tayari!

Mitume wanaweza kutambua kwamba bwana harusi ambaye Yesu anamtaja, ni Yesu mwenyewe. Hapo awali hata alijilinganisha na bwana harusi. (Luka 5:34, 35) Namna gani wale mabikira wenye busara? Alipokuwa akizungumza kuhusu “kundi dogo” ambao watapewa Ufalme, Yesu alitumia maneno haya: “Vaeni mavazi, muwe tayari na mwashe taa zenu.” (Luka 12:32, 35) Basi, katika mfano huu unaohusu mabikira, mitume wanaweza kuelewa kwamba Yesu anamaanisha wao wenyewe. Sasa Yesu anawasilisha ujumbe gani katika mfano huo?

Yesu hawaachi na shaka hata kidogo kuhusu jambo hilo. Anamalizia mfano wake kwa kusema: “Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui ile siku wala saa.”—Mathayo 25:13.

Ni wazi kuwa Yesu anawahimiza wafuasi wake waaminifu kwamba kuhusu kuwapo kwake, watahitaji, ‘kuendelea kukesha.’ Yeye atakuja, nao wanapaswa kuwa tayari na kuwa macho—kama wale mabikira watano—ili wasije wakasahau tumaini lao lenye thamani na kukosa thawabu wanayoweza kupata.