Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 35

Mahubiri Maarufu ya Mlimani

Mahubiri Maarufu ya Mlimani

MATHAYO 5:1–7:29 LUKA 6:17-49

  • MAHUBIRI YA MLIMANI

Lazima Yesu amechoka baada ya kusali usiku wote na kisha kuwachagua wanafunzi 12 wawe mitume. Sasa ni mchana, lakini bado ana nguvu na anatamani kuwasaidia watu. Anafanya hivyo kwenye mlima fulani ulio Galilaya, huenda si mbali na eneo analofanyia shughuli zake huko Kapernaumu.

Umati umekuja kwake kutoka maeneo ya mbali. Wengine wametoka kusini, huko Yerusalemu na maeneo ya Yudea. Wengine wametoka katika majiji ya pwani ya Tiro na Sidoni huko kaskazini magharibi. Kwa nini wamekuja kumtafuta Yesu? Ili “kumsikiliza na kuponywa magonjwa.” Na hivyo ndivyo inavyokuwa—Yesu ‘anawaponya wote.’ Fikiria jambo hilo! Wagonjwa wote wanaponywa. Yesu pia anawahudumia “wale [wanaosumbuliwa] na roho waovu,” ambao wanateswa na malaika waovu wa Shetani.—Luka 6:17-19.

Kisha Yesu anapata mahali palipo tambarare kwenye mlima, nao umati unakusanyika kumzunguka. Inawezekana kwamba wanafunzi wake, na hasa wale mitume 12, ndio walio karibu zaidi naye. Wote wanatamani kumsikiliza mwalimu huyu anayeweza kufanya miujiza hiyo. Yesu anatoa hotuba ambayo kwa kweli inawanufaisha wasikilizaji wake. Tangu wakati huo, watu wengine wengi wamefaidika na mahubiri hayo. Sisi pia tunaweza kufaidika na habari hizo za kiroho zenye kina ambazo zimeelezwa kwa njia rahisi na iliyo wazi. Yesu anatumia mifano ya kawaida na vitu ambavyo watu wanavifahamu. Hilo linafanya mawazo yake yaeleweke na watu wote wanaotafuta maisha bora katika njia ya Mungu. Ni mambo gani makuu ya mahubiri ya Yesu yanayofanya yawe muhimu sana?

NI NANI WALIO NA FURAHA YA KWELI?

Kila mtu anataka kuwa na furaha. Akijua jambo hilo, Yesu anaanza kufafanua kuhusu watu walio na furaha ya kweli. Wazia jinsi jambo hilo linavyofanya wasikilizaji wake wawe makini. Lakini kuna mambo yanayowatatanisha.

Anasema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao. Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa. . . . Wenye furaha ni wale walio na njaa na kiu ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa. . . . Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao. Wenye furaha ni ninyi, watu wanapowashutumu na kuwatesa . . . kwa sababu yangu. Furahini na kushangilia sana.”​—Mathayo 5:3-12.

Yesu anamaanisha nini anaposema “furaha”? Hamaanishi kuchangamka au kucheka, kama mtu anavyofanya anapofurahia burudani. Furaha ya kweli ni yenye kina zaidi. Inahusisha kuridhika kabisa, kutosheka na kuwa na kusudi maishani.

Yesu anasema kwamba watu wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, wanaohuzunishwa na hali yao ya kutenda dhambi, na wanaomjua na kumtumikia Mungu ndio wenye furaha ya kweli. Hata wakichukiwa au kuteswa kwa sababu ya kufanya mapenzi ya Mungu, wana furaha kwa sababu wanajua kwamba wanampendeza Mungu na kwamba atawathawabisha kwa kuwapa uzima wa milele.

Ingawa hivyo, watu wengi wanafikiri kwamba kuwa tajiri na kuishi maisha ya starehe ndiyo mambo yanayomletea mtu furaha. Yesu anasema jambo tofauti. Akionyesha tofauti inayowafanya wengi kati ya wasikilizaji wake wafikiri, anasema: “Ole wenu ninyi matajiri, kwa sababu mnapata faraja yenu kikamili. Ole wenu ninyi mlioshiba sasa, kwa sababu mtakuwa na njaa. Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, kwa sababu mtaomboleza na kulia. Ole wenu watu wote wanapowasifu, kwa maana hivyo ndivyo mababu zao walivyowatendea manabii wa uwongo.”—Luka 6:24-26.

Kwa nini kuwa na utajiri, kucheka kwa shangwe, na kufurahia kusifiwa na watu kunaleta ole? Kwa sababu mtu anapokuwa na vitu hivyo na kuvithamini sana, huenda akapuuza kumtumikia Mungu na hivyo kukosa furaha ya kweli. Yesu hasemi kwamba kuwa maskini au kuwa na njaa humfanya mtu awe na furaha. Hata hivyo, mara nyingi maskini ndio wanaokubali mafundisho ya Yesu na kupata baraka ya kuwa na furaha ya kweli.

Yesu anasema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Ninyi ndio chumvi ya dunia.” (Mathayo 5:13) Bila shaka, wao si chumvi halisi. Badala yake, chumvi hutumiwa kuhifadhi vitu. Kiasi kikubwa cha chumvi huwekwa karibu na madhabahu kwenye hekalu la Mungu na hunyunyizwa juu ya dhabihu. Pia chumvi inawakilisha kuwa huru kutokana na uchafu au kuoza. (Mambo ya Walawi 2:13; Ezekieli 43:23, 24) Wanafunzi wa Yesu ndio “chumvi ya dunia” kwa sababu wanaposhirikiana na watu wanaweza kuwahifadhi, kwa kuwasaidia wasioze kiroho na kiadili. Naam, ujumbe wao unaweza kuhifadhi uhai wa wote wanaoukubali.

Pia Yesu anawaambia wanafunzi: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu.” Taa haiwekwi chini ya kikapu bali huwekwa kwenye kinara cha taa, ili iangaze. Basi Yesu anawahimiza: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili waone matendo yenu mema na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:14-16.

AWAWEKEA WAFUASI WAKE VIWANGO VYA JUU

Viongozi wa dini ya Kiyahudi wanamwona Yesu kuwa mtu anayevunja Sheria ya Mungu na hivi karibuni walipanga njama ya kumuua. Basi Yesu anasema waziwazi: “Msifikiri nilikuja kuharibu Sheria au Manabii. Sikuja kuharibu, bali kutimiza.”—Mathayo 5:17.

Naam, Yesu anaheshimu sana Sheria ya Mungu na anawahimiza wengine wafanye hivyo pia. Kwa kweli anasema: “Kwa hiyo, yeyote anayevunja mojawapo ya amri hizi ndogo na kufundisha wengine kufanya hivyo, ataitwa mdogo kuhusiana na Ufalme wa mbinguni.” Anamaanisha kwamba mtu kama huyo hataingia kamwe katika Ufalme. Anaendelea kusema: “Lakini yeyote anayeshika na kufundisha amri hizi ataitwa mkubwa kuhusiana na Ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 5:19.

Yesu anashutumu hata mitazamo inayomchochea mtu avunje Sheria ya Mungu. Baada ya kutaja kwamba Sheria inasema “Usiue,” Yesu anaongezea hivi: “Kila mtu anayeendelea kumkasirikia ndugu yake atawajibika mahakamani.” (Mathayo 5:21, 22) Kuendelea kumkasirikia mtu mwingine ni jambo zito, ambalo hata linaweza kumfanya mtu aue. Hivyo Yesu anaelezea jitihada ambazo mtu anapaswa kufanya ili kupata amani: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo unakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, iache zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, uende zako. Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.”—Mathayo 5:23, 24.

Amri nyingine ya Sheria inakataza uzinzi. Yesu anasema: “Mlisikia kwamba ilisemwa: ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini ninawaambia kila mtu anayeendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:27, 28) Yesu hazungumzi kuhusu kuwazia tu kifupi ukosefu wa maadili; badala yake, anakazia uzito wa jambo hilo mtu ‘anapoendelea kutazama.’ Mara nyingi, kuendelea kutazama huamsha tamaa ya ngono. Kisha, nafasi ikitokea, mtu anaweza kufanya uzinzi. Mtu anawezaje kuepuka jambo hilo? Huenda akahitaji kuchukua hatua kali. Yesu anasema: “Basi, ikiwa jicho lako la kulia linafanya ujikwae, ling’oe na kulitupilia mbali. . . . Ikiwa mkono wako wa kulia unakufanya ujikwae, ukate na kuutupilia mbali.”—Mathayo 5:29, 30.

Ili kuokoa uhai wao, watu fulani wamekubali kwa hiari kupoteza kiungo fulani kilichoathiriwa na ugonjwa. Basi inaeleweka Yesu anaposema kwamba ni muhimu zaidi ‘kutupilia mbali’ kitu chochote, hata kiungo muhimu kama vile jicho au mkono, ili kuepuka mawazo machafu na matendo yanayofuatia. Yesu anaeleza: “Ni afadhali upoteze kiungo kimoja kuliko mwili wako wote utupwe katika Gehena” (rundo la takataka linalochomeka nje ya kuta za Yerusalemu), kumaanisha kuangamizwa kabisa.

Yesu anatoa ushauri pia kuhusu kushughulika na watu wanaowaumiza na kuwakosea wengine. Anasema: “Msimzuie mtu mwovu, bali yeyote anayekupiga kofi kwenye shavu la kulia, mgeuzie pia shavu la kushoto.” (Mathayo 5:39) Hilo halimaanishi kwamba mtu hawezi kujikinga au kuilinda familia yake inaposhambuliwa. Yesu anataja kofi, ambalo mara nyingi halikusudiwi kumjeruhi mtu vibaya au kumuua; badala yake, ni kitendo cha dharau. Anasema kwamba mtu akijaribu kuanzisha vita au mabishano, labda kwa kukupiga kofi au kukutukana, usilipize kisasi.

Ushauri huo unapatana na sheria ya Mungu ya kumpenda jirani. Basi Yesu anawashauri wasikilizaji wake hivi: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” Anatoa sababu muhimu ya kufanya hivyo: “Ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni, kwa kuwa yeye huwaangazia jua lake waovu na wema.”—Mathayo 5:44, 45.

Yesu anamalizia sehemu hiyo ya mahubiri yake kwa kusema: “Basi lazima muwe wakamilifu kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mathayo 5:48) Bila shaka, hamaanishi kwamba watu wanaweza kuwa wakamilifu kabisa. Hata hivyo, kwa kumwiga Mungu, tunaweza kupanua upendo wetu na kuwapenda hata maadui wetu. Kwa maneno mengine: “Endeleeni kuwa wenye rehema, kama Baba yenu alivyo mwenye rehema.”—Luka 6:36.

SALA NA KUMTEGEMEA MUNGU

Yesu anapoendelea na mahubiri yake, anawahimiza wasikilizaji wake: “Iweni waangalifu msionyeshe uadilifu wenu mbele ya watu ili wawaone.” Yesu anashutumu mtu kujionyesha kwamba anamwogopa Mungu kinafiki, anaongezea hivi: “Unapotoa zawadi za rehema, usipige tarumbeta mbele yako kama wanavyofanya wanafiki.” (Mathayo 6:1, 2) Ni bora kutoa zawadi za rehema faraghani.

Kisha Yesu anasema: “Mnaposali msifanye kama wanafiki, kwa maana wanapenda kusali wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye kona za barabara kuu ili watu wawaone.” Badala yake anasema: “Unaposali, ingia ndani ya chumba chako faraghani, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye mahali pa siri.” (Mathayo 6:5, 6) Yesu hapingi sala zote za hadharani, kwa maana hata yeye alisali hadharani. Anashutumu sala zinazotolewa ili kuwafurahisha wasikilizaji na kufanya watu wampongeze yule anayesali.

Yesu anaushauri umati hivi: “Mnaposali msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya.” (Mathayo 6:7) Yesu hamaanishi kwamba ni kosa kusali tena na tena kuhusu jambo lilelile. Anapinga kutumia maneno yanayokaririwa “tena na tena,” sala za kurudiwa-rudiwa. Kisha anatoa sala ya mfano iliyo na maombi saba. Maombi ya kwanza matatu yanakazia haki ya Mungu ya kutawala na makusudi yake, yaani, jina lake litakaswe, Ufalme wake uje, na mapenzi yake yatendeke. Baada ya kutaja mambo hayo tunaweza kuomba mambo ya kibinafsi kama vile chakula chetu cha kila siku na msamaha wa dhambi, na kwamba tusijaribiwe kuliko tunavyoweza kuhimili na tukombolewe kutoka kwa yule mwovu.

Mali zetu zinapaswa kuwa muhimu kadiri gani kwetu? Yesu anauhimiza umati: “Acheni kujiwekea hazina duniani, ambako nondo na kutu hula na ambako wezi huvunja na kuiba.” Ni ushauri wenye busara kwelikweli! Mali za kimwili zinaweza kuharibika nazo huharibika, na haziwezi kuboresha uhusiano wetu na Mungu. Basi, Yesu anaongezea hivi: “Jiwekeeni hazina mbinguni.” Tunaweza kufanya hivyo kwa kutanguliza utumishi wa Mungu maishani. Hakuna mtu anayeweza kuondoa msimamo wetu mzuri mbele za Mungu au thawabu ya kupata uzima wa milele. Basi maneno haya ya Yesu ni ya kweli: “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.”—Mathayo 6:19-21.

Ili kukazia jambo hilo, Yesu anatoa mfano: “Taa ya mwili ni jicho. Basi, ikiwa jicho lako linakazia jambo hususa, mwili wako wote utakuwa mwangavu. Lakini ikiwa jicho lako lina wivu, mwili wako wote utakuwa na giza.” (Mathayo 6:22, 23) Jicho letu linapoona vizuri, linakuwa kama taa ya mwili wetu. Lakini ili liwe hivyo, jicho letu linapaswa kukazia jambo moja; la sivyo, tunaweza kuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu maisha. Kukazia fikira vitu vya kimwili badala ya kumtumikia Mungu kunamaanisha kwamba ‘mwili wetu wote una giza,’ labda tunavutiwa na giza, yaani, ukosefu wa unyoofu.

Kisha Yesu anatoa mfano wenye kuchochea: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”—Mathayo 6:24.

Huenda baadhi ya watu wanaomsikiliza Yesu wanajiuliza jinsi wanavyopaswa kuona mahitaji yao ya kimwili. Basi anawahakikishia kwamba hawapaswi kuhangaika ikiwa watatanguliza utumishi wa Mungu. “Waangalieni kwa makini ndege wa angani; hawapandi mbegu, hawavuni, wala kukusanya ghalani, na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha.”—Mathayo 6:26.

Namna gani kuhusu mayungiyungi ya shambani yaliyo hapo mlimani? Yesu anasema kwamba “hata Sulemani katika utukufu wake wote hakupambwa kama maua hayo.” Hilo linaonyesha nini? “Ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo hapa leo na kesho hutupwa ndani ya jiko, je, hatawavika vizuri zaidi ninyi wenye imani kidogo?” (Mathayo 6:29, 30) Kwa hekima Yesu anawahimiza: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ . . . Baba yenu wa mbinguni anajua kwamba mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.”—Mathayo 6:31-33.

JINSI YA KUPATA UZIMA

Mitume na watu wengine wanyoofu wanataka kuishi maisha yanayompendeza Mungu, lakini hali yao inafanya iwe vigumu. Kwa mfano, Mafarisayo wengi wanawashutumu watu na kuwahukumu kwa ukali. Basi Yesu anawahimiza wasikilizaji wake: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa.”—Mathayo 7:1, 2.

Ni hatari kufuata mtazamo wa Mafarisayo wa kuwakosoa-kosoa watu kupita kiasi, kama mfano huu wa Yesu unavyoonyesha: “Je, kipofu anaweza kumwongoza kipofu mwenzake? Wote watatumbukia shimoni, sivyo?” Basi wasikilizaji wa Yesu wanapaswa kuwaonaje watu wengine? Hawapaswi kuwakosoa-kosoa, kwa sababu hilo lingekuwa kosa zito. Anauliza: “Unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Ndugu, niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako,’ wakati wewe mwenyewe huoni boriti lililo katika jicho lako? Mnafiki! Kwanza toa boriti katika jicho lako, kisha utaona vizuri jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.”—Luka 6:39-42.

Hilo halimaanishi kwamba wanafunzi hawapaswi kuhukumu kamwe. Yesu anawahimiza: “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msiwatupie nguruwe lulu zenu.” (Mathayo 7:6) Kweli za Neno la Mungu ni zenye thamani, kama lulu za mfano. Watu fulani wakitenda kama wanyama, kwa kutothamini kweli hizo zenye thamani, wanafunzi wanapaswa kuwaacha na kutafuta wale watakaosikiliza.

Akizungumzia tena kuhusu sala, Yesu anakazia uhitaji wa kuendelea kusali. “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa.” Mungu yuko tayari kujibu sala, kama Yesu anavyokazia kwa kuuliza: “Ni nani miongoni mwenu ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? . . . Kwa hiyo, ingawa ninyi ni watenda dhambi na mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomwomba?”—Mathayo 7:7-11.

Kisha Yesu anatoa kanuni ambayo inakubaliwa na wengi: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.” Je, sisi sote hatupaswi kukubali na kufuata himizo hilo tunaposhughulika na wengine? Lakini inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo, kama maagizo haya ya Yesu yanavyoonyesha: “Ingieni kupitia lango jembamba, kwa sababu lango ni pana, na barabara inayoongoza kwenye uharibifu ina nafasi kubwa, na ni wengi wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na ni wachache wanaoipata.”—Mathayo 7:12-14.

Kuna watu ambao wangejaribu kuwapotosha wanafunzi kutoka kwenye njia inayoelekea kwenye uzima, basi Yesu anawaonya: “Jihadharini na manabii wa uwongo ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo, lakini ndani wao ni mbwamwitu wakali.” (Mathayo 7:15) Yesu anasema kwamba miti mizuri na miti mibaya inaweza kutambuliwa kupitia matunda yake. Ndivyo ilivyo na watu. Kwa hiyo, tunaweza kuwatambua manabii wa uwongo kupitia mafundisho na matendo yao. Naam, Yesu anaeleza kwamba mtu hawi mwanafunzi wake kupitia tu mambo anayosema bali pia mambo anayofanya. Watu fulani wanadai kwamba Yesu ndiye Bwana wao, lakini namna gani ikiwa hawafanyi mapenzi ya Mungu? Yesu anasema: “Ndipo nitakapowaambia: ‘Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi mnaotenda uasi sheria!’”—Mathayo 7:23.

Akimalizia mahubiri yake, Yesu anasema: “Kila mtu anayesikia haya maneno yangu na kuyatenda ni kama mtu mwenye busara aliyejenga nyumba yake kwenye mwamba. Kisha mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, upepo ukavuma na kuipiga nyumba hiyo, lakini haikuporomoka, kwa maana msingi wake ulikuwa umejengwa kwenye mwamba.” (Mathayo 7:24, 25) Kwa nini nyumba hiyo haikuanguka? Kwa sababu mtu huyo “[ali]chimba kina kirefu na kuweka msingi kwenye mwamba.” (Luka 6:48) Kwa hiyo mengi yanahusika zaidi ya kusikia tu maneno ya Yesu. Tunapaswa kujitahidi ‘kuyatenda.’

Namna gani kuhusu “mtu anayesikia haya maneno” lakini “hayatendi”? Yeye ni kama “mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba juu ya mchanga.” (Mathayo 7:26) Mvua, mafuriko, na upepo hufanya nyumba hiyo iporomoke.

Katika mahubiri hayo, umati unashangazwa na njia ya Yesu ya kufundisha. Anafundisha kama mtu mwenye mamlaka na si kama viongozi wao wa kidini. Inawezekana kwamba wengi waliomsikiliza wanakuwa wanafunzi wake.