Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 47

Msichana Mdogo Afufuliwa!

Msichana Mdogo Afufuliwa!

Yairo anaona kwamba Yesu amemponya yule mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu. Bila shaka Yesu anaweza kumponya binti yake pia, ingawa anahisi kwamba ‘kufikia sasa binti yake atakuwa amekufa.’ (Mathayo 9:18) Je, bado binti yake anaweza kupata msaada?

Yesu akiwa bado anazungumza na yule mwanamke aliyeponywa, watu fulani wanafika kutoka nyumbani kwa Yairo na kumwambia: “Binti yako amekufa!” Wanamuuliza: “Kwa nini uendelee kumsumbua Mwalimu?”—Marko 5:35.

Habari hizo zinahuzunisha sana! Mtu huyu ambaye anaheshimika sana katika jamii, sasa hawezi kufanya chochote. Binti yake wa pekee amekufa. Hata hivyo, Yesu anasikia habari hizo, anamgeukia Yairo na kumtia moyo akisema: “Usiogope, uwe tu na imani.”—Marko 5:36.

Yesu anaenda na Yairo nyumbani kwa Yairo. Wanapofika wanapata mvurugo mkubwa. Watu waliokusanyika hapo wanalia, wanaomboleza, na kujipigapiga kwa huzuni. Yesu anaingia ndani na kusema maneno haya yenye kushangaza: “Mtoto hajafa bali amelala usingizi.” (Marko 5:39) Watu wanaposikia hivyo wanamcheka Yesu. Wanajua kwamba kwa kweli msichana huyo amekufa. Hata hivyo, akitumia nguvu ambazo Mungu alimpa, Yesu ataonyesha kwamba watu wanaweza kufufuliwa kama tu wanavyoamshwa kutoka kwenye usingizi mzito.

Yesu anaagiza wote watoke nje isipokuwa Petro, Yakobo, Yohana, na wazazi wa msichana aliyekufa. Yesu anaenda pamoja na watu hao watano mahali alipolala yule msichana. Anamshika mkono na kusema: “‘Talitha kumi,’ maneno ambayo yanapotafsiriwa, yanamaanisha: ‘Msichana mdogo, ninakuambia, “Inuka!”’” (Marko 5:41) Mara moja anainuka na kuanza kutembea. Wazia shangwe ambayo Yairo na mke wake wanahisi wanapoona jambo hilo! Akitoa uthibitisho zaidi kwamba msichana huyo yuko hai, Yesu anaagiza apewe chakula.

Hapo awali, Yesu aliwaagiza wale aliowaponya wasitangaze mambo aliyowafanyia, na hivyo ndivyo anavyowaagiza wazazi hawa. Hata hivyo, wazazi hawa wenye furaha na watu wengine pia wanaeneza habari hizo “katika eneo hilo lote.” (Mathayo 9:26) Ikiwa ungeona mpendwa wako akifufuliwa, je hungezungumzia habari hizo kwa msisimko? Huo ni muujiza wa pili ulioandikwa wa ufufuo aliofanya Yesu.