Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Kifo

Kifo

Wafu wako wapi?

“Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”—Mwanzo 3:19.

WATU HUSEMA NINI?

Watu fulani hufikiri kwamba, baada ya kifo, watu huenda mbinguni, motoni, toharani, au kwingineko. Wengine wanaamini mtu huzaliwa upya akiwa kiumbe kingine. Kwa upande mwingine, wale wanaokataa mawazo ya kidini wanaamini kwamba kifo ndio mwisho wa mambo yote.

BIBLIA INASEMA NINI?

Andiko la Mhubiri 9:10 linasema hivi: “Hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.” Biblia hueleza pia kinachowapata wanadamu na wanyama wanapokufa. Inasema: “Wote wanaenda mahali pamoja. Wote wametoka katika mavumbi, nao wote wanarudi mavumbini.”Mhubiri 3:20.

 Wafu wako katika hali gani?

“Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.”—Zaburi 146:4.

WATU HUSEMA NINI?

Wengi wamefundishwa kwamba mahali atakapoenda mtu baada ya kufa panategemea mambo aliyofanya alipokuwa hai duniani. Ikiwa alifanya mambo mazuri, thawabu yake itakuwa furaha ya milele; ikiwa alifanya mabaya, atateseka milele. Inasemekana kwamba lazima wanadamu wasafishwe dhambi kabla ya kukubaliwa kumwona Mungu baada ya kufa. Inadaiwa wale ambao hawajasafishwa hawawezi kupata shangwe hiyo milele.

BIBLIA INASEMA NINI?

Wafu hawafurahii wala kuteseka. Kwa kweli, kwa kuwa hawajui lolote, hawawezi kuhisi chochote, kuwasaidia au kuwaumiza walio hai. Andiko la Mhubiri 9:5, 6 linasema: “Kwa maana walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, . . . Pia, upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea, na mpaka wakati usio na kipimo hawana fungu lolote tena katika chochote ambacho kitafanywa chini ya jua.”

Je, wafu wana tumaini lolote?

“Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena? Mimi nitangojea siku zote za kazi yangu ya kulazimishwa, mpaka kitulizo changu kije.”—Ayubu 14:14.

WATU HUSEMA NINI?

Inaaminiwa kwamba mtu anapohukumiwa kwenda motoni, hana tumaini tena. Mateso ya motoni yanasemekana ni ya milele. Kwa upande mwingine, inasemekana kwamba wale walio toharani wanaweza tu kwenda mbinguni baada ya kuondolewa kabisa dhambi zao.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mwana wa Mungu atawafufua wale waliolala katika kifo, au kuwarudisha hai hapa duniani. Biblia inasema: “Msistaajabie jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:26, 28, 29) Baada ya hapo, vitendo vya mtu ndivyo vitakavyoamua kama Mungu atampa uzima wa milele. *

^ fu. 14 Kwa habari zaidi kuhusu ufufuo, tafadhali soma sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kinachopatikana kwenye www.jw.org/sw.