Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 38

Yohana Anataka Kusikia Kutoka kwa Yesu

Yohana Anataka Kusikia Kutoka kwa Yesu

MATHAYO 11:2-15 LUKA 7:18-30

  • YOHANA MBATIZAJI AULIZA KUHUSU JUKUMU LA YESU

  • YESU AMSIFU YOHANA

Yohana Mbatizaji amekuwa gerezani kwa karibu mwaka mmoja. Lakini, bado anasikia kuhusu kazi za ajabu za Yesu. Wazia jinsi Yohana anavyohisi wanafunzi wake wanapomwambia kwamba Yesu amemfufua mwana wa mjane huko Naini. Hata hivyo, Yohana anataka kusikia moja kwa moja kutoka kwa Yesu kuhusu maana ya mambo hayo yote. Basi Yohana anawatuma wawili kati ya wanafunzi wake. Wakafanye nini? Waende wakamuulize Yesu: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja, au tumtarajie mwingine?”—Luka 7:19.

Je, hilo linaonekana kuwa swali la ajabu? Yohana ni mtu anayemwogopa Mungu, na alipombatiza Yesu karibu miaka miwili iliyopita, aliona roho ya Mungu ikishuka juu ya Yesu na akasikia sauti ya Yehova akimkubali Yesu. Hatuna sababu ya kufikiri kwamba imani ya Yohana imedhoofika. La sivyo, Yesu hangemsifu sana Yohana, kama anavyofanya pindi hii. Lakini ikiwa Yohana hana shaka, kwa nini anamuuliza Yesu swali hilo?

Huenda Yohana anataka kuhakikishiwa moja kwa moja na Yesu kwamba yeye ndiye Masihi. Hilo litamwimarisha Yohana akiwa gerezani. Na inaonekana swali la Yohana lina maana nyingine. Anafahamu unabii wa Biblia unaoonyesha kwamba Mtiwa Mafuta wa Mungu atakuwa mfalme na mkombozi. Ingawa hivyo, miezi mingi baada ya Yesu kubatizwa, bado Yohana yuko gerezani. Basi Yohana anauliza kama kuna mwingine anayekuja, mrithi wa Yesu, kwa njia ya mfano, ambaye atakamilisha mambo yote yaliyotabiriwa kwamba yatatimizwa na Masihi.

Badala ya kuwaambia tu wanafunzi wa Yohana, ‘Bila shaka mimi ndiye Yule anayekuja,’ Yesu anathibitisha kwamba Mungu anamuunga mkono kwa kuwaponya watu wengi magonjwa na udhaifu wa kila aina. Kisha anawaambia wanafunzi hao hivi: “Nendeni mkamwambie Yohana mambo mnayosikia na kuona: Vipofu wanaona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.”—Mathayo 11:4, 5.

Huenda swali la Yohana likaonyesha kwamba anatazamia Yesu atafanya mengi kuliko yale anayofanya sasa na labda kumfungua kutoka gerezani. Hata hivyo, Yesu anamwambia Yohana asitarajie mengi kuliko miujiza ambayo Yesu anafanya.

Baada ya wanafunzi wa Yohana kuondoka, Yesu anauhakikishia umati kwamba Yohana ni zaidi ya nabii. Yeye ndiye “mjumbe” wa Yehova aliyetabiriwa kwenye Malaki 3:1. Pia, yeye ndiye nabii Eliya, kama ilivyotabiriwa kwenye Malaki 4:5, 6. Yesu anafafanua hivi: “Kwa kweli ninawaambia, kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mtu mkuu kuliko Yohana Mbatizaji, lakini mtu mdogo zaidi katika Ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.”—Mathayo 11:11.

Yesu anaposema kwamba mtu mdogo zaidi katika Ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko Yohana, anamaanisha kwamba Yohana hatakuwapo katika Ufalme wa mbinguni. Yohana alimtayarishia Yesu njia, lakini anakufa kabla Kristo hajafungua njia ya kwenda mbinguni. (Waebrania 10:19, 20) Hata hivyo, Yohana ni nabii mwaminifu wa Mungu na ataishi duniani akiwa raia wa Ufalme wa Mungu.