MAONI YA BIBLIA
Masihi
Biblia ilitabiri kwamba Masihi angekuja ulimwenguni ili kuwakomboa watu kutokana na magonjwa, mateso, na kifo. Je, Yesu Kristo ndiye Masihi aliyeahidiwa?
Watu wangemtambuaje Masihi?
Kulingana na unabii wa Biblia, Masihi, au Kristo, angetimiza majukumu mawili, lakini kwa vipindi viwili tofauti. * Katika jukumu lake la kwanza, angekuwa mwanadamu. Ili wanadamu wamtambue, Biblia ilitaja mapema kuhusu maisha na huduma yake. Kwa kweli, “kutoa ushahidi kumhusu Yesu” ndiyo kusudi la unabii wa Biblia.—Ufunuo 19:10.
Alipokuwa duniani, Yesu alifanya mambo machache tu kwa kulinganisha na yale atakayofanya ulimwenguni kote akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu
BIBLIA INASEMA NINI?
Masihi angekuwa . . .
-
Mzao wa Mfalme Daudi.—Isaya 9:7; Luka 3:23-31. *
-
Angezaliwa katika mji wa Bethlehemu.—Mika 5:2; Luka 2:4-7.
-
Mtangazaji mnyenyekevu wa “habari njema.”—Isaya 61:1; Luka 4:43.
-
Angechukiwa na kudharauliwa.—Isaya 53:3; Mathayo 26:67, 68.
-
Angesalitiwa kwa vipande 30 vya fedha.—Zekaria 11:12, 13; Mathayo 26:14, 15.
-
Angenyamaza kimya wakati anapohukumiwa kifo na wapinzani wake.—Isaya 53:6, 7; Mathayo 27:12-14.
-
“Kondoo” wa dhabihu, ambaye angeondoa dhambi na kuwawezesha wanadamu kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu.—Isaya 53:7; Yohana 1:29, 34, 36.
-
Angeuawa lakini hakuna hata mfupa wake mmoja ungevunjwa.—Zaburi 34:20; Yohana 19:33, 36.
-
Angezikwa pamoja na matajiri.—Isaya 53:9; Mathayo 27:57-60.
-
Angefufuliwa katika siku ya tatu. —Mathayo 16:21; 28:5-7.
Yesu alitimiza unabii huo tuliozungumzia na mwingine pia. Vilevile aliponya wagonjwa na kufufua wafu. Kwa hiyo, kwa kutimiza unabii huo Yesu alituthibitishia kwamba yeye ndiye Masihi aliyeahidiwa na kwamba tunaweza kuwa na imani thabiti atatimiza kwa kiwango kikubwa ahadi zote za Biblia kuhusu wakati ujao. (Luka 7:21-23; Ufunuo 21:3, 4) Baada ya kufufuliwa na kurudi mbinguni, Yesu alikaa kwenye “mkono wa kuume” wa Mungu, akingojea wakati wa kukamilisha kazi yake akiwa Masihi.—Zaburi 110:1-6.
“Kristo atakapofika, je, atafanya ishara zaidi ya zile ambazo mtu huyu amefanya?”—Yohana 7:31.
Masihi atakamilishaje kazi yake?
Wayahudi katika siku za Yesu walitazamia Masihi awakomboe kutoka katika utawala wa Waroma na awe mtawala wa ufalme uliorudishwa wa Israeli. (Matendo 1:6) Baadaye wafuasi wa Yesu waliokuwa Wayahudi walielewa kwamba Yesu angekamilisha jukumu lake mbinguni akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu na aliyekabidhiwa mamlaka yote.—Mathayo 28:18.
BIBLIA INASEMA NINI?
Katika jukumu lake la pili, Masihi . . .
-
Atatawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ambayo ni serikali ya ulimwenguni pote.—Danieli 7:13, 14; Ufunuo 11:15.
-
Atawabariki wanadamu wote wanaomwamini yeye.—Mwanzo 22:17, 18; Zaburi 72:7, 8.
-
“Atayashtua mataifa mengi” atakapowaangamiza watawala wao wanaompinga.—Isaya 52:15; Ufunuo 19:19, 20.
-
Atauokoa “umati mkubwa” wa wanadamu waadilifu kutoka mataifa yote ili waishi katika ulimwengu mpya wenye amani.—Ufunuo 7:9, 10, 13-17.
-
Kwa msaada wa Yehova Mungu, atawafufua wafu ili waishi katika Paradiso duniani.—Luka 23:43; Yohana 5:21, 28, 29.
-
Atawafundisha raia zake jinsi ya kuishi kwa amani.—Isaya 11:1, 2, 9, 10.
-
Ataondoa dhambi, ambayo ndiyo chanzo kikuu cha magonjwa na kifo.—Yohana 1:29; Waroma 5:12.
-
Hatimaye, atazivunja kazi zote za Ibilisi na wanadamu watakuwa chini ya utawala wa Yehova Mungu.—1 Wakorintho 15:25-28; 1 Yohana 3:8.
Yesu alitimiza jukumu lake la kwanza akiwa Masihi. Pia atakamilisha jukumu lake la pili. Kwa hiyo, watu wenye hekima wanajifunza kumhusu Yesu kwa kuwa alisema hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.”—Yohana 14:6.
“Katika siku zake aliye mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena. Naye atakuwa na raia . . . mpaka miisho ya dunia.”—Zaburi 72:7, 8.
^ fu. 5 Jina “Masihi” linatokana na lugha ya Kiebrania. Ilhali jina “Kristo” ambalo lina maana sawa na Masihi; linatokana na Kigiriki.—Yohana 1:41.
^ fu. 7 Katika orodha hii, andiko la kwanza linahusu unabii; andiko la pili linahusu utimizo wa unabii huo.