Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?

Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Unyoofu

Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Unyoofu

KANUNI YA BIBLIA: “Ni nani atakayekuwa mgeni katika hema lako [Mungu]? . . . Yeye anayetembea bila kosa na kuzoea kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake.”Zaburi 15:1, 2.

FAIDA: Watu wengi huvutiwa na sifa ya unyoofu na uaminifu. Lakini wanatendaje wanapojua kwamba watafaidika kwa kutenda kwa njia ambayo si ya unyoofu na ikiwa hakuna yeyote atakayewakamata? Jambo hilo litategemea hali ya mtu ya moyoni.

Raquel, mwanamke ambaye kazi yake ilihusisha kununua bidhaa mbalimbali za kampuni, alisema hivi: “Wauzaji fulani walijaribu kunihonga. Waliniahidi kwamba iwapo ningenunua bidhaa zao, wangenipa kisiri baadhi ya pesa za ziada zilizokusudiwa kwenda kwenye kampuni niliyofanyia kazi. Lakini nilikumbuka ushauri wa Biblia kuhusu umuhimu wa unyoofu na nikakataa pesa hizo. Msimamizi wangu alipojua jambo hilo, aliendelea kuniamini zaidi.”

Ikiwa Raquel angekubali kupokea rushwa hiyo, huenda angefaidika kifedha kwa muda mfupi tu. Lakini hali ingekuwaje ikiwa mwajiri wake angegundua jambo hilo? Je, Raquel angefutwa kazi? Je, angefaulu kupata kazi nyingine wakati ujao? Jambo muhimu kwake lilikuwa kudumisha dhamiri njema na heshima yake. Andiko la Methali 22:1 linasema: “Ni afadhali kuchagua jina badala ya utajiri mwingi; kibali ni bora kuliko hata fedha na dhahabu.”

Jessie aliaminiwa na mwajiri wake kwa sababu ya kuwa mfanyakazi mnyoofu

Jessie pia alikuwa mnyoofu na mwaminifu, na aliaminiwa sana na mwajiri wake. Alifaidikaje? Mwajiri wake alimteua kuwa msimamizi na akampa uhuru wa kujipangia shughuli zake za kazi. Jambo hilo lilimsaidia apate muda zaidi wa kuwa pamoja na mke na watoto wake na hata muda kwa ajili ya mambo ya ibada.

Waajiri wengine hutafuta wafanyakazi miongoni mwa mashirika yanayojulikana kuwa na watu wenye sifa ya unyoofu. Kwa mfano, meneja mmoja wa kampuni nchini Filipino aliandika barua kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini humo akiomba Mashahidi wajaze maombi ya kazi katika kampuni yake. Alisema hivi: Wao ni “wachapakazi, ni wanyoofu, na waaminifu.” Bila shaka, utukufu na sifa zimwendee Yehova Mungu, ambaye anatufundisha ‘tuchukie yaliyo mabaya’ na ‘kupenda yaliyo mema.’—Amosi 5:15.