Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, BIBLIA INA FAIDA LEO?

Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Uaminifu

Viwango Vinavyomfaa Kila Mtu, Nyakati Zote—Uaminifu

KANUNI YA BIBLIA: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi.”Waebrania 13:4.

FAIDA: Watu wengine wanasema kwamba maneno hayo yamepitwa na wakati. Hata hivyo, wamekosea sana! Ukosefu wa uaminifu una madhara makubwa leo, sawa tu na ilivyokuwa Biblia ilipoandikwa.—Methali 6:34, 35.

Jessie, mwanamume aliyefunga ndoa na aliye na watoto wawili, alisema hivi: “Uaminifu katika ndoa umechangia kwa kiasi kikubwa furaha na uhusiano mzuri nilio nao pamoja na mke wangu. Kuaminiana ni jambo muhimu sana katika ndoa. Ukosefu wa uaminifu husababisha kutokuaminiana.” Vilevile watoto huathiriwa sana mume na mke wanapokosa uaminifu katika ndoa yao!

Ligaya * alihatarisha ndoa yake. Anasema hivi: “Nilianza kushirikiana na watu wasiofaa. Nikaanza kwenda kwenye vilabu vya usiku na pia kufanya uzinzi.” Je, maisha hayo yalimletea furaha? La hasha! Kila siku alikorofishana na mume wake, na hakuwa na furaha. Anaongezea kusema hivi: “Nilipotafakari kuhusu matatizo niliyojiletea, nilitambua kwamba wazazi wangu hawakuwa wamekosea walipokuwa wakiniambia, ‘Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.’”—1 Wakorintho 15:33.

Ligaya anaendelea kusema: “Kabla mambo hayajaharibika kabisa, niliamua kuacha njia zangu mbaya, na nikaanza kujifunza Biblia. Wakati huu niliamua kufuata mambo niliyokuwa nikijifunza.” Ikawaje? Ligaya aliokoa ndoa yake, na mume wake akaanza kumheshimu na kumtendea kwa fadhili. Anamalizia kwa kusema hivi: “Biblia ilibadili maisha yangu, na sijuti kwamba niliacha njia zangu mbaya na marafiki niliokuwa nao.”

^ fu. 6 Baadhi ya majina yamebadilishwa.