Kulingana na Luka 23:1-56

  • Yesu mbele ya Pilato na Herode (1-25)

  • Yesu na wahalifu wawili watundikwa kwenye mti (26-43)

    • “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso” (43)

  • Yesu afa (44-49)

  • Yesu azikwa (50-56)

23  Kisha umati huo wote ukasimama na kumpeleka Yesu kwa Pilato.+  Ndipo wakaanza kumshtaki,+ wakisema: “Tulimkuta mtu huyu akipindua taifa letu na kuwakataza watu wasimlipe Kaisari kodi,+ akisema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo mfalme.”+  Sasa Pilato akamuuliza: “Je, wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?” Akamjibu: “Wewe mwenyewe unasema hivyo.”+  Ndipo Pilato akawaambia wakuu wa makuhani na ule umati: “Sioni mtu huyu akiwa na kosa lolote.”+  Lakini wakasisitiza wakisema: “Anawachochea watu kwa kufundisha katika Yudea yote, kuanzia Galilaya mpaka hapa.”  Pilato aliposikia hivyo akauliza ikiwa Yesu alikuwa Mgalilaya.  Baada ya kuhakikisha kwamba alitoka katika eneo lililotawaliwa na Herode, akaagiza apelekwe kwa Herode,+ ambaye pia siku hizo alikuwa Yerusalemu.  Herode alipomwona Yesu alifurahi sana. Kwa maana kwa muda mrefu alitaka kumwona Yesu kwa sababu alikuwa amesikia mengi kumhusu,+ na alitamani kumwona akifanya miujiza.  Basi akaanza kumuuliza maswali mengi, lakini Yesu hakumjibu.+ 10  Hata hivyo, wakuu wa makuhani na waandishi wakaendelea kusimama na kumshtaki kwa ukali. 11  Ndipo Herode na wanajeshi wake wakamtendea kwa dharau,+ naye Herode akamdhihaki+ kwa kumvika vazi la kifahari na kuagiza arudishwe kwa Pilato. 12  Siku hiyo Herode na Pilato wakawa marafiki, kwa maana kabla ya hapo walikuwa maadui. 13  Ndipo Pilato akawaita wakuu wa makuhani, watawala, na watu, 14  akawaambia: “Mliniletea mtu huyu mkisema anachochea watu kuasi. Tazama! Nilimhoji mbele yenu lakini sikupata msingi wa mashtaka yenu dhidi yake.+ 15  Kwa kweli, hata Herode hakupata, ndiyo maana alimrudisha kwetu, tazama! ni wazi hajafanya jambo lolote linalostahili kifo. 16  Kwa hiyo nitamwadhibu+ na kumfungua.” 17 * —— 18  Lakini umati wote ukasema kwa sauti kubwa: “Muue mtu huyu,* na utufungulie Baraba!”+ 19  (Mtu huyo alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya mauaji na uchochezi uliokuwa umetokea jijini.) 20  Pilato akawapazia sauti tena, kwa sababu alitaka kumfungua Yesu.+ 21  Ndipo wakaanza kupiga kelele, wakisema: “Atundikwe mtini! Atundikwe mtini!”*+ 22  Akawaambia mara ya tatu: “Kwa nini? Amefanya kosa gani? Mimi sikuona jambo lolote linalofanya astahili kifo; kwa hiyo nitamwadhibu kisha nimfungue.” 23  Lakini wakazidi kusisitiza, wakidai kwa sauti kubwa, kwamba auawe,* na sauti zao zikashinda.+ 24  Basi Pilato akaamua kutimiza dai lao. 25  Akamfungua yule mtu waliyemtaka, ambaye alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya uchochezi na mauaji, lakini akamkabidhi Yesu mikononi mwao ili wamtendee wanavyopenda. 26  Walipokuwa wakienda naye, wakamshika Simoni wa Kirene, aliyekuwa akitoka mashambani, nao wakamtwika mti wa mateso* aubebe na kumfuata Yesu.+ 27  Watu wengi walikuwa wakimfuata, kutia ndani wanawake waliokuwa wakijipigapiga kwa huzuni na kumwombolezea. 28  Yesu akawageukia wanawake hao na kuwaambia: “Binti za Yerusalemu, acheni kunililia. Bali jililieni ninyi wenyewe na watoto wenu;+ 29  kwa maana tazama! siku zinakuja ambapo watu watasema, ‘Wenye furaha ni wanawake walio tasa, wanawake ambao hawakuzaa, na wanawake ambao hawakunyonyesha!’+ 30  Ndipo wataanza kuiambia milima, ‘Tuangukieni!’ na vilima, ‘Tufunikeni!’+ 31  Ikiwa wanafanya mambo haya wakati mti ni mbichi, itakuwaje utakapokauka?” 32  Wanaume wengine wawili, wahalifu, walikuwa pia wakipelekwa wakauawe pamoja naye.+ 33  Walipofika mahali panapoitwa Fuvu la Kichwa,+ wakamtundika Yesu kwenye mti pamoja na wale wahalifu, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.+ 34  Lakini Yesu alikuwa akisema: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui wanachofanya.” Isitoshe, wakapiga kura ili wagawane mavazi yake.+ 35  Watu walikuwa wamesimama hapo wakitazama. Lakini wale viongozi walikuwa wakimdhihaki na kusema: “Aliwaokoa wengine; mwacheni ajiokoe mwenyewe, ikiwa yeye ndiye Yule Aliyechaguliwa, Kristo wa Mungu.”+ 36  Hata wale wanajeshi wakamdhihaki, wakamkaribia na kumpa divai kali+ 37  wakisema: “Ikiwa wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi, jiokoe.” 38  Kulikuwa pia na maandishi haya juu yake: “Huyu ndiye Mfalme wa Wayahudi.”+ 39  Ndipo mmoja wa wale wahalifu waliotundikwa akaanza kumtukana+ akisema: “Wewe ndiye Kristo, sivyo? Jiokoe na utuokoe sisi pia!” 40  Yule mwingine akamkemea akisema: “Je, wewe humwogopi Mungu hata kidogo, kwa kuwa umepata hukumu ileile? 41  Sisi tunastahili kuteseka kwa sababu ya makosa tuliyofanya; lakini mtu huyu hakufanya kosa lolote.” 42  Kisha akasema: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.”+ 43  Yesu akamwambia: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”+ 44  Sasa, karibu saa sita,* kukawa na giza katika nchi yote mpaka saa tisa,*+ 45  kwa sababu hakukuwa na nuru ya jua; kisha pazia la patakatifu+ likapasuka katikati.+ 46  Naye Yesu akapaza sauti na kusema: “Baba, naiweka roho yangu mikononi mwako.”+ Baada ya kusema hayo akafa.*+ 47  Alipoona mambo yaliyotokea, ofisa wa jeshi akaanza kumtukuza Mungu, akisema: “Kwa kweli mtu huyu alikuwa mwadilifu.”+ 48  Na watu wote waliokuwa wamekusanyika hapo ili kuona tukio hilo, walipoona mambo yaliyotukia, wakarudi nyumbani wakijipigapiga vifua. 49  Wale wote waliomfahamu walikuwa wamesimama mbali kidogo. Pia, wanawake waliokuwa wamefuatana naye kutoka Galilaya, walikuwa hapo na waliona mambo hayo.+ 50  Na tazama! kulikuwa na mwanamume aliyeitwa Yosefu, mshiriki wa Baraza, ambaye alikuwa mtu mwema na mwadilifu.+ 51  (Mtu huyo hakupiga kura kuunga mkono njama na kitendo chao.) Alikuwa wa kutoka Arimathea, jiji la Wayudea, naye alikuwa akiungojea Ufalme wa Mungu. 52  Mtu huyo alienda kwa Pilato akaomba apewe mwili wa Yesu. 53  Naye akaushusha+ na kuufunga kwa kitani bora, akaulaza katika kaburi* lililochongwa kwenye mwamba,+ ambamo hakuna mtu aliyewahi kulazwa. 54  Ilikuwa siku ya Matayarisho,+ na Sabato+ ilikuwa inakaribia kuanza. 55  Lakini wanawake waliokuja naye kutoka Galilaya, wakaenda kutazama kaburi* na jinsi mwili wake ulivyolazwa,+ 56  kisha wakarudi kutayarisha manukato na mafuta yenye marashi. Lakini, bila shaka, walipumzika siku ya Sabato+ kulingana na Sheria.

Maelezo ya Chini

Tnn., “Mwondoe mtu huyu.”
Au “Auawe kwenye mti! Auawe kwenye mti!”
Au “auawe kwenye mti.”
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Au “akakata pumzi.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”