Kulingana na Mathayo 26:1-75

  • Makuhani wapanga njama ya kumuua Yesu (1-5)

  • Yesu amiminiwa mafuta yenye manukato (6-13)

  • Pasaka ya mwisho na kusalitiwa (14-25)

  • Mlo wa Jioni wa Bwana waanzishwa (26-30)

  • Yesu atabiri kwamba Petro atamkana (31-35)

  • Yesu asali huko Gethsemane (36-46)

  • Yesu akamatwa (47-56)

  • Kesi mbele ya Sanhedrini (57-68)

  • Petro amkana Yesu (69-75)

26  Basi Yesu alipomaliza kusema hayo yote, akawaambia wanafunzi wake:  “Mnajua kwamba baada ya siku mbili kutakuwa na Pasaka,+ naye Mwana wa binadamu atatolewa ili auawe kwenye mti.”+  Ndipo wakuu wa makuhani na wazee wa watu wakakusanyika katika ua wa kuhani mkuu aliyeitwa Kayafa,+  nao wakapanga njama pamoja+ ili kumkamata Yesu kwa hila* na kumuua.  Hata hivyo, walikuwa wakisema: “Si kwenye sherehe, ili watu wasifanye ghasia.”  Yesu alipokuwa Bethania katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma,+  mwanamke fulani aliyekuwa na chupa ya alabasta yenye mafuta ghali yenye marashi akamkaribia, akaanza kuyamimina juu ya kichwa cha Yesu alipokuwa akila.*  Walipoona hilo wanafunzi wakakasirika na kusema: “Hasara hii ni ya nini?  Kwa maana mafuta haya yangeuzwa kwa kiasi kikubwa cha pesa na kupewa maskini.” 10  Akijua jambo hilo, Yesu akawaambia: “Kwa nini mnataka kumsumbua mwanamke huyu? Amenitendea jambo jema. 11  Kwa maana maskini mnao sikuzote,+ lakini mimi hamtakuwa nami sikuzote.+ 12  Alipomimina mafuta haya yenye marashi kwenye mwili wangu, alifanya hivyo ili kunitayarisha kwa ajili ya mazishi.+ 13  Kwa kweli ninawaambia, popote ambapo hii habari njema itahubiriwa ulimwenguni, jambo alilofanya mwanamke huyu litatajwa pia ili kumkumbuka.”+ 14  Ndipo mmoja wa wale 12, aliyeitwa Yuda Iskariote,+ akaenda kwa wakuu wa makuhani+ 15  na kuwauliza: “Mtanipa nini ili nimsaliti kwenu?”+ Wakakubaliana naye vipande 30 vya fedha.+ 16  Basi tangu wakati huo akaanza kutafuta nafasi nzuri ya kumsaliti. 17  Siku ya kwanza ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu+ wanafunzi wakaja kumuuliza Yesu: “Unataka tukutayarishie wapi mlo wa Pasaka?”+ 18  Akawaambia: “Nendeni jijini kwa mwanamume fulani mkamwambie, ‘Mwalimu anasema: “Wakati wangu uliowekwa umekaribia; nitasherehekea Pasaka pamoja na wanafunzi wangu nyumbani kwako.”’” 19  Basi, wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, wakaandaa Pasaka. 20  Ilipofika jioni,+ Yesu alikuwa ameketi mezani pamoja na wale wanafunzi 12.+ 21  Walipokuwa wakila, akasema: “Kwa kweli ninawaambia, mmoja wenu atanisaliti.”+ 22  Wakiwa wamehuzunishwa sana na jambo hilo, kila mmoja wao akaanza kumuuliza: “Bwana, je, ni mimi?” 23  Akawajibu: “Anayechovya mkono wake pamoja nami katika bakuli ndiye atakayenisaliti.+ 24  Kwa kweli, Mwana wa binadamu anaenda zake, kama ilivyoandikwa kumhusu, lakini ole+ wake mtu atakayemsaliti Mwana wa binadamu!+ Ingekuwa afadhali kama mtu huyo hangezaliwa.”+ 25  Yuda, aliyekuwa karibu kumsaliti akauliza: “Je, ni mimi, Rabi?” Yesu akamjibu: “Wewe mwenyewe umesema.” 26  Walipokuwa wakiendelea kula, Yesu akachukua mkate, na baada ya kutoa baraka, akaumega,+ akawapa wanafunzi wake, akasema: “Chukueni mle. Huu unamaanisha mwili wangu.”+ 27  Kisha akachukua kikombe, akashukuru na kuwapa akisema: “Kunyweni ninyi nyote,+ 28  kwa maana hii inamaanisha ‘damu yangu+ ya agano,’+ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi+ ili wasamehewe dhambi.+ 29  Lakini ninawaambia: sitakunywa tena kamwe divai yoyote ya mzabibu mpaka siku nitakapoinywa ikiwa mpya pamoja nanyi katika Ufalme wa Baba yangu.”+ 30  Mwishowe, baada ya kuimba sifa,* wakaenda kwenye Mlima wa Mizeituni.+ 31  Ndipo Yesu akawaambia: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku wa leo, kwa maana imeandikwa: ‘Nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanyika.’+ 32  Lakini baada ya kufufuliwa nitawatangulia kuingia Galilaya.”+ 33  Lakini Petro akajibu: “Hata wengine wote wakikwazika kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!”+ 34  Yesu akamwambia: “Kwa kweli ninakuambia, usiku huu, kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.”+ 35  Petro akamwambia: “Hata nikilazimika kufa pamoja nawe, sitakukana kamwe.”+ Wale wanafunzi wengine wote wakasema vivyo hivyo. 36  Ndipo Yesu akaja pamoja nao mpaka mahali panapoitwa Gethsemane,+ akawaambia wanafunzi: “Ketini hapa, mimi naenda pale kusali.”+ 37  Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, naye akaanza kuhuzunika na kutaabika sana.+ 38  Ndipo akawaambia: “Nimehuzunika* sana, kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami.”+ 39  Akasonga mbele kidogo, akaanguka kifudifudi, akasali:+ “Baba yangu, ikiwa inawezekana, niondolee kikombe hiki.+ Lakini, si kama ninavyopenda, bali kama unavyopenda.”+ 40  Akarudi na kuwakuta wanafunzi wakiwa wamelala usingizi, akamuuliza Petro: “Je, hamngeweza kukesha pamoja nami hata kwa saa moja?+ 41  Endeleeni kukesha+ na kusali bila kuacha,+ ili msiingie katika majaribu.+ Bila shaka, roho inataka* lakini mwili ni dhaifu.”+ 42  Akaenda tena mara ya pili na kusali: “Baba yangu, ikiwa siwezi kuepuka kunywa kikombe hiki, acha mapenzi yako yatendeke.”+ 43  Akaja tena na kuwakuta wakiwa wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa mazito. 44  Basi akawaacha, akaenda tena kusali mara ya tatu, akisema tena jambo lilelile. 45  Kisha akarudi na kuwaambia wanafunzi: “Mnalala na kupumzika wakati kama huu! Tazama! Saa imekaribia ya Mwana wa binadamu kusalitiwa mikononi mwa watenda dhambi. 46  Simameni twende. Tazama! Msaliti wangu amekaribia.” 47  Alipokuwa bado akizungumza, tazama! Yuda, mmoja wa wale 12, akaja pamoja na umati mkubwa wakiwa na mapanga na marungu, walikuwa wametumwa na wakuu wa makuhani na wazee wa watu.+ 48  Basi msaliti wake alikuwa amewapa ishara, akisema: “Yule nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni.” 49  Akaenda moja kwa moja kwa Yesu akasema: “Salamu, Rabi!” kisha akambusu kwa wororo. 50  Lakini Yesu akamuuliza: “Mwenzangu, umekuja kufanya nini?”+ Ndipo wakaja na kumkamata Yesu na kumtia nguvuni. 51  Lakini tazama! mmoja wa wale waliokuwa pamoja na Yesu akanyoosha mkono wake, akauchomoa upanga wake, akampiga mtumwa wa kuhani mkuu na kumkata sikio.+ 52  Ndipo Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake,+ kwa maana wote wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga.+ 53  Au unafikiri siwezi kumwomba Baba yangu anipe sasa hivi vikosi zaidi ya 12 vya malaika?+ 54  Hata hivyo, Maandiko yanayosema lazima itendeke hivi yatatimizwaje?” 55  Saa hiyo, Yesu akauambia umati: “Je, mmekuja kunikamata mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba mimi ni mwizi? Siku baada ya siku nilikuwa nikiketi hekaluni nikifundisha+ lakini hamkunikamata.+ 56  Lakini yote haya yametokea ili kutimiza mambo yaliyoandikwa* na manabii.”+ Ndipo wanafunzi wote wakamwacha na kukimbia.+ 57  Wale waliomkamata Yesu wakampeleka kwa Kayafa+ kuhani mkuu, ambako waandishi na wazee walikuwa wamekusanyika.+ 58  Lakini Petro akaendelea kumfuata kwa mbali, mpaka katika ua wa kuhani mkuu, na baada ya kuingia ndani, akaketi pamoja na watumishi wa nyumbani ili aone itakavyokuwa.+ 59  Sasa wakuu wa makuhani na Sanhedrini yote walikuwa wakitafuta ushahidi wa uwongo dhidi ya Yesu ili wamuue.+ 60  Lakini hawakupata, ingawa mashahidi wengi wa uwongo walijitokeza.+ Baadaye, mashahidi wawili wakajitokeza 61  na kusema: “Mtu huyu alisema, ‘Ninaweza kuliangusha chini hekalu la Mungu na kulijenga kwa siku tatu.’”+ 62  Ndipo kuhani mkuu akasimama na kumuuliza: “Kwa nini hujibu? Watu hawa wanashuhudia nini kukuhusu?”+ 63  Lakini Yesu akakaa kimya.+ Basi kuhani mkuu akamwambia: “Ninakuapisha mbele za Mungu aliye hai utuambie kama wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu!”+ 64  Yesu akamjibu: “Wewe mwenyewe umesema. Lakini ninawaambia: Tangu sasa mtamwona Mwana wa binadamu+ akiwa ameketi kwenye mkono wa kuume wa nguvu,+ akija juu ya mawingu ya mbinguni.”+ 65  Ndipo kuhani mkuu akayararua mavazi yake ya nje, akisema: “Amekufuru! Tunahitaji mashahidi wengine wa nini? Tazama! Sasa mmemsikia akikufuru. 66  Mnaonaje?” Wakamjibu: “Anastahili kufa.”+ 67  Kisha wakamtemea mate usoni+ na kumpiga ngumi.+ Wengine wakampiga makofi usoni,+ 68  wakisema: “Tutolee unabii, wewe Kristo. Ni nani aliyekupiga?” 69  Basi Petro alikuwa ameketi nje katika ua, kijakazi akamjia na kumwambia: “Hata wewe ulikuwa pamoja na Yesu Mgalilaya!”+ 70  Lakini akakana mbele yao wote, akisema: “Sijui unachosema.” 71  Alipoenda kwenye chumba kilicho langoni, msichana mwingine akamwona na kuwaambia wale waliokuwa hapo: “Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu Mnazareti.”+ 72  Akakana tena akiapa: “Simjui mtu huyo!” 73  Baada ya muda mfupi wale waliokuwa wamesimama hapo wakaja na kumwambia Petro: “Hakika wewe pia ni mmoja wao, kwa maana matamshi* yako yanakutambulisha.” 74  Ndipo akaanza kulaani na kuapa: “Simjui mtu huyo!” Na mara moja jogoo akawika. 75  Naye Petro akakumbuka maneno aliyosema Yesu, yaani: “Kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.”+ Naye akaenda nje akalia kwa uchungu.

Maelezo ya Chini

Au “kwa ujanja.”
Au “alipokuwa ameketi mezani.”
Au “zaburi.”
Au “nafsi yangu inahuzunika.”
Au “inapenda.”
Au “maandiko.”
Au “lafudhi.”