Kulingana na Mathayo 24:1-51

  • ISHARA YA KUWAPO KWA KRISTO (1-51)

    • Vita, njaa, matetemeko ya ardhi (7)

    • Habari njema itahubiriwa (14)

    • Dhiki kuu (21, 22)

    • Ishara ya Mwana wa binadamu (30)

    • Mtini (32-34)

    • Kama siku za Noa (37-39)

    • Endeleeni kukesha (42-44)

    • Mtumwa mwaminifu na mtumwa mwovu (45-51)

24  Yesu alipokuwa akitoka hekaluni, wanafunzi wake wakamkaribia na kumwonyesha majengo ya hekalu.  Akawaambia: “Je, mnaona vitu hivi vyote? Kwa kweli ninawaambia, hakuna jiwe litakaloachwa hapa juu ya jiwe lingine bila kuangushwa chini.”+  Alipokuwa ameketi kwenye Mlima wa Mizeituni, wanafunzi wakamkaribia faraghani, wakamuuliza: “Tuambie, mambo haya yatatukia lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo*+ kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”*+  Yesu akawajibu: “Jihadharini ili mtu yeyote asiwapotoshe,+  kwa maana wengi watakuja kwa msingi wa jina langu, wakisema, ‘Mimi ndiye Kristo,’ nao watawapotosha wengi.+  Mtasikia kuhusu vita na habari za vita. Msishtuke kwa maana lazima mambo hayo yatukie, lakini ule mwisho bado.+  “Kwa maana taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme,+ kutakuwa na upungufu wa chakula+ na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali.+  Mambo hayo yote ni mwanzo wa maumivu ya taabu.  “Kisha watu watawakabidhi kwenye dhiki+ na kuwaua ninyi,+ nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.+ 10  Pia, wengi watakwazika, nao watasalitiana na kuchukiana. 11  Manabii wengi wa uwongo watatokea na kuwapotosha wengi;+ 12  na kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi sheria, upendo wa wengi utapoa. 13  Lakini yule atakayevumilia* mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.+ 14  Na hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote,+ na ndipo ule mwisho utakapokuja. 15  “Kwa hiyo, mtakapoona kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa, kama alivyosema nabii Danieli, kikiwa kimesimama mahali patakatifu+ (msomaji na atumie utambuzi), 16  ndipo wale walio Yudea waanze kukimbilia milimani.+ 17  Mtu aliye juu ya paa la nyumba asishuke kuchukua mali ndani ya nyumba yake; 18  na mtu aliye shambani asirudi kuchukua vazi lake la nje. 19  Ole wao wanawake wenye mimba na wale wanaonyonyesha mtoto katika siku hizo! 20  Endeleeni kusali ili mtakapokimbia isiwe wakati wa majira ya baridi kali wala siku ya Sabato; 21  kwa maana wakati huo kutakuwa na dhiki kuu+ ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatokea tena.+ 22  Kwa kweli, kama siku hizo hazingefupishwa, hakuna mwili wowote ambao ungeokolewa; lakini kwa sababu ya wale waliochaguliwa, siku hizo zitafupishwa.+ 23  “Na ikiwa mtu yeyote atawaambia, ‘Tazama! Kristo yuko hapa,’+ au, ‘Yuko pale!’ msiamini.+ 24  Kwa maana Kristo wengi wa uwongo na manabii wa uwongo+ watatokea na kufanya ishara kubwa na maajabu ili kuwapotosha,+ ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa. 25  Tazama! Nimewaonya mapema. 26  Basi, watu wakiwaambia, ‘Tazama! Yuko nyikani,’ msiende; ‘Tazama! Yumo katika vyumba vya ndani,’ msiamini.+ 27  Kwa maana kama radi inavyotokea mashariki na kuangaza mpaka magharibi, ndivyo kuwapo* kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.+ 28  Popote palipo na mzoga, hapo ndipo tai watakapokusanyika.+ 29  “Mara tu baada ya dhiki ya siku hizo jua litatiwa giza,+ mwezi hautatoa nuru yake, nyota zitaanguka kutoka mbinguni, na nguvu za mbingu zitatikiswa.+ 30  Ndipo ishara ya Mwana wa binadamu itakapoonekana mbinguni, na makabila yote ya dunia yatajipigapiga kwa huzuni,+ nayo yatamwona Mwana wa binadamu+ akija juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi.+ 31  Kisha atawatuma malaika zake pamoja na sauti kubwa ya tarumbeta, nao watawakusanya watu wake waliochaguliwa kutoka kwenye zile pepo nne za dunia, kuanzia mwisho mmoja wa mbingu mpaka mwisho mwingine.+ 32  “Basi jifunzeni mfano huu kutokana na mtini: Mara tu matawi yake machanga yanapokuwa laini na kuchipua majani, mnajua kwamba kiangazi kinakaribia.+ 33  Vivyo hivyo, ninyi pia mtakapoona mambo yote hayo, jueni kwamba yuko karibu milangoni.+ 34  Kwa kweli ninawaambia kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo haya yote yatukie. 35  Mbingu na dunia zitapitilia mbali, lakini maneno yangu hayatapitilia mbali kamwe.+ 36  “Kuhusu siku hiyo na saa hiyo, hakuna mtu anayejua,+ hata malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.+ 37  Kwa maana kama siku za Noa zilivyokuwa,+ ndivyo kuwapo* kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.+ 38  Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya Gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina,+ 39  nao hawakujali mpaka Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote,+ ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. 40  Kisha wanaume wawili watakuwa shambani; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa. 41  Wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe la kusagia; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.+ 42  Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui Bwana wenu atakuja siku gani.+ 43  “Lakini jueni jambo hili: Ikiwa mwenye nyumba angejua mwizi atakuja katika kesha gani,*+ angekaa macho na hangeruhusu nyumba yake ivunjwe.+ 44  Kwa hiyo ninyi pia iweni tayari,+ kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia. 45  “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara* ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa?+ 46  Mwenye furaha ni mtumwa huyo ikiwa bwana wake atakapokuja atamkuta akifanya hivyo!+ 47  Kwa kweli ninawaambia, atamweka rasmi asimamie mali zake zote. 48  “Lakini ikiwa mtumwa huyo mwovu atasema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia,’+ 49  naye aanze kuwapiga watumwa wenzake na kula na kunywa pamoja na walevi wa kupindukia, 50  bwana wa mtumwa huyo atakuja siku asiyotazamia na katika saa asiyoijua,+ 51  naye atamwadhibu kwa ukali sana na kumweka pamoja na wanafiki. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.+

Maelezo ya Chini

Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “anayevumilia.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “wakati gani wa usiku.”
Au “hekima.”