Kulingana na Mathayo 15:1-39

  • Yesu afunua mapokeo ya wanadamu (1-9)

  • Mtu huchafuliwa na kinachotoka moyoni (10-20)

  • Imani kubwa ya mwanamke Mfoinike (21-28)

  • Yesu aponya magonjwa mengi (29-31)

  • Yesu alisha wanaume 4,000 (32-39)

15  Ndipo Mafarisayo na waandishi kutoka Yerusalemu wakamjia Yesu+ wakisema:  “Kwa nini wanafunzi wako huvunja mapokeo ya mababu zetu? Kwa mfano, hawanawi* mikono kabla ya kula.”+  Akawajibu: “Kwa nini ninyi pia huvunja amri ya Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu?+  Kwa mfano, Mungu alisema, ‘Mheshimu baba yako na mama yako,’+ na, ‘Yeyote anayemtukana* baba yake au mama yake anapaswa kuuawa.’+  Lakini ninyi mnasema, ‘Yeyote anayemwambia baba yake au mama yake: “Chochote nilicho nacho ambacho kingekusaidia ni zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu,”+  anakosa kabisa kumheshimu baba yake.’ Kwa hiyo, mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu.+  Ninyi wanafiki, kwa kufaa Isaya alitabiri kuwahusu aliposema:+  ‘Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali nami.  Wao huniabudu bure, kwa maana wanafundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.’”+ 10  Ndipo akauita umati ukaribie na kuwaambia: “Sikilizeni na kuelewa maneno haya:+ 11  Mtu hachafuliwi na kile kinachoingia kinywani mwake, bali huchafuliwa na kile kinachotoka kinywani mwake.”+ 12  Ndipo wanafunzi wakaja na kumwambia: “Unajua kwamba Mafarisayo walikwazika waliposikia mambo uliyosema?”+ 13  Akawajibu: “Kila mmea ambao Baba yangu wa mbinguni hakuupanda utang’olewa. 14  Waacheni. Wao ni viongozi vipofu. Basi, kipofu akimwongoza kipofu, wote wawili watatumbukia ndani ya shimo.”+ 15  Petro akamwambia: “Tufafanulie mfano huo.” 16  Ndipo akasema: “Je, ninyi pia bado hamwelewi?+ 17  Je, hamjui kwamba chochote kinachoingia kinywani hupita tumboni kisha hutoka na kuingia chooni? 18  Hata hivyo, mambo yanayotoka kinywani hutoka moyoni, nayo ndiyo yanayomchafua mtu.+ 19  Kwa mfano, moyoni hutoka mawazo mabaya,+ mauaji, uzinzi, uasherati,* wizi, ushahidi wa uwongo, na makufuru. 20  Hayo ndiyo mambo yanayomchafua mtu; lakini kula bila kunawa* mikono hakumchafui mtu.” 21  Yesu akatoka hapo na kwenda katika eneo la Tiro na Sidoni.+ 22  Na tazama! mwanamke fulani Mfoinike kutoka eneo hilo akamjia, akapaza sauti: “Nihurumie,* Bwana, Mwana wa Daudi. Binti yangu anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.”+ 23  Lakini Yesu hakumjibu mwanamke huyo. Kwa hiyo wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mwambie aende, kwa sababu anaendelea kutufuata akipaza sauti.” 24  Yesu akajibu: “Sikutumwa kwa yeyote isipokuwa kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.”+ 25  Lakini mwanamke huyo akaja na kumsujudia* akisema: “Bwana, nisaidie!” 26  Yesu akamjibu: “Haifai kuuchukua mkate wa watoto na kuwatupia mbwa wadogo.” 27  Mwanamke huyo akasema: “Ndiyo Bwana, lakini hata hao mbwa wadogo hula makombo yanayoanguka kutoka kwenye meza ya mabwana wao.”+ 28  Ndipo Yesu akamwambia: “Ewe mwanamke, imani yako ni kubwa; na itendeke kama unavyotaka.” Na kuanzia saa hiyo binti yake akapona. 29  Yesu akaondoka hapo na kwenda karibu na Bahari ya Galilaya,+ kisha akapanda mlimani, akaketi huko. 30  Ndipo umati mkubwa ukamjia, na kuwaleta watu waliokuwa viwete, vilema, vipofu, mabubu, na wengine wengi, nao wakawaweka miguuni pake, naye akawaponya.+ 31  Basi umati ukashangaa ulipoona mabubu wakiongea, vilema wakiponywa, viwete wakitembea, na vipofu wakiona, nao wakamsifu Mungu wa Israeli.+ 32  Lakini Yesu akawaita wanafunzi wake na kuwaambia: “Ninausikitikia umati,+ kwa sababu tayari wamekaa pamoja nami siku tatu nao hawajala chochote. Sitaki kuwaacha waende wakiwa na njaa,* wasije wakazimia njiani.”+ 33  Hata hivyo, wanafunzi wakamwambia: “Tutapata wapi mikate ya kutosha kuushibisha umati huu mkubwa mahali hapa pasipo na watu?”+ 34  Ndipo Yesu akawauliza: “Mna mikate mingapi?” Wakajibu: “Saba, na samaki wachache wadogo.” 35  Kwa hiyo, baada ya kuuagiza umati uketi chini, 36  akachukua ile mikate saba na wale samaki, na baada ya kutoa shukrani, akamega na kuanza kuwagawia wanafunzi, nao wanafunzi wakaugawia umati.+ 37  Na wote wakala wakashiba, kisha wakakusanya vipande vilivyobaki, wakajaza vikapu saba vikubwa.+ 38  Sasa wale waliokula walikuwa wanaume 4,000, na pia wanawake na watoto wadogo. 39  Mwishowe, baada ya kuuaga umati, akaingia kwenye mashua na kwenda katika eneo la Magadani.+

Maelezo ya Chini

Yaani, hawajisafishi kisherehe.
Au “anayesema mambo mabaya kumhusu.”
Wingi wa neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.
Yaani, bila kujisafisha kisherehe.
Au “Nionyeshe rehema.”
Au “kumwinamia.”
Au “wamefunga.”