Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 44

Hekalu kwa Ajili ya Yehova

Hekalu kwa Ajili ya Yehova

Sulemani alipokuwa mfalme wa Israeli, Yehova alimuuliza hivi: ‘Ungependa nikupe nini?’ Sulemani akasema: ‘Mimi ni kijana, na sijui ninafanya nini. Tafadhali nipe hekima ili niweze kuwaongoza watu wako.’ Yehova akasema: ‘Kwa sababu umeomba upate hekima, nitakufanya uwe mtu mwenye hekima zaidi duniani. Pia nitakufanya uwe tajiri sana. Na ikiwa utanitii, utaishi muda mrefu.’

Sulemani akaanza kujenga hekalu. Alitumia dhahabu, fedha, mbao, na mawe bora. Maelfu ya wanaume na wanawake wenye ustadi walifanya kazi ya kujenga hekalu. Baada ya miaka saba, hekalu lilikuwa tayari kuwekwa wakfu kwa Yehova. Lilikuwa na madhabahu. Juu ya madhabahu kulikuwa na dhabihu. Sulemani akapiga magoti mbele ya madhabahu hiyo na kusali: ‘Ee Yehova, hekalu hili si kubwa wala si maridadi vya kutosha kwa ajili yako, lakini tafadhali kubali ibada yetu na usikilize sala zetu.’ Unafikiri Yehova alikuwa na maoni gani kuhusu hekalu hilo na sala ya Sulemani? Mara tu Sulemani alipomaliza kutoa sala, moto ukashuka kutoka mbinguni na kuteketeza dhabihu zilizokuwa juu ya madhabahu. Yehova alikubali hekalu hilo. Waisraeli walipoona hilo, wakashangilia.

Mfalme Sulemani alijulikana kotekote katika Israeli na hata maeneo ya mbali zaidi kwa sababu ya hekima yake. Watu walikuja kumwomba Sulemani awasaidie kutatua matatizo yao. Hata malkia wa Sheba alikuja kumjaribu kwa kumuuliza maswali magumu. Aliposikia majibu ya Sulemani, malkia huyo akasema hivi: ‘Sikuamini mambo ambayo watu waliniambia kukuhusu, lakini sasa ninaona kwamba una hekima kuliko walivyoniambia. Mungu wako, Yehova, amekubariki.’ Maisha katika taifa la Israeli yalikuwa mazuri, na watu walikuwa na furaha. Lakini mambo yalikuwa karibu kubadilika.

“Tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Sulemani.”​—Mathayo 12:42