Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 15

Yehova Hakumsahau Yosefu Kamwe

Yehova Hakumsahau Yosefu Kamwe

Yosefu alipokuwa gerezani, Farao mfalme wa Misri aliota ndoto ambazo hakuna mtu aliyeweza kueleza maana yake. Mtumishi mmoja akamwambia Farao kwamba Yosefu angeweza kumweleza maana ya ndoto zake. Mara moja, Farao akaagiza Yosefu aletwe.

Farao akamwuliza hivi: ‘Unaweza kunieleza maana ya ndoto zangu?’ Yosefu akamwambia Farao hivi: ‘Nchi ya Misri itakuwa na chakula kingi kwa miaka saba, lakini miaka saba itakayofuata kutakuwa na njaa. Chagua mtu mwenye hekima ahifadhi chakula ili watu wako wasife njaa.’ Farao akajibu hivi: ‘Ninakuchagua wewe! Utakuwa mtu wa pili kwa mamlaka nchini Misri!’ Yosefu alijuaje maana ya ndoto za Farao? Yehova alimsaidia Yosefu.

Kwa miaka saba iliyofuata, Yosefu alihifadhi chakula. Na kama ambavyo Yosefu alikuwa amesema, kukawa na njaa duniani pote. Watu walitoka maeneo mbalimbali kuja kununua chakula kutoka kwa Yosefu. Yakobo, baba ya Yosefu, akasikia kwamba kuna chakula nchini Misri, kwa hiyo akawatuma wana wake kumi waende huko kununua chakula.

Wana wa Yakobo walienda kwa Yosefu, naye akawatambua mara moja. Lakini hawakumtambua Yosefu. Wakamwinamia kama alivyokuwa ameota akiwa mdogo. Yosefu alitaka kujua ikiwa kaka zake bado walikuwa na chuki. Kwa hiyo, akawaambia hivi: ‘Ninyi ni wapelelezi. Mnataka kuchunguza udhaifu wa nchi yetu.’ Wakasema, ‘Hapana! Tulizaliwa kaka 12 nchini Kanaani. Ndugu yetu mmoja amekufa, na yule mdogo zaidi yuko na baba yetu.’ Kisha Yosefu akawaambia hivi: ‘Nileteeni ndugu yenu mdogo, nami nitawaamini.’ Kwa hiyo wakarudi nyumbani kwao.

Chakula kilipoisha, Yakobo aliwatuma tena wana wake waende Misri. Pindi hii, walisafiri pamoja na Benyamini, ndugu yao mdogo. Ili kuwajaribu ndugu zake, Yosefu alificha kikombe cha fedha kwenye mfuko wa Benyamini na kusema kwamba walikuwa wamekiiba. Watumishi wa Yosefu walipopata kikombe hicho kwenye mfuko wa Benyamini, ndugu zake walishtuka. Wakamwomba Yosefu awaadhibu wao badala ya Benyamini.

Sasa Yosefu akatambua kwamba ndugu zake walikuwa wamebadilika. Yosefu akashindwa kujizuia. Akabubujikwa na machozi na kusema hivi: ‘Mimi ni ndugu yenu, Yosefu. Je, baba yangu yuko hai?’ Ndugu zake walishangaa sana. Akawaambia hivi: ‘Msihuzunike kwa sababu ya kile mlichonifanyia. Mungu alinituma huku ili niwaokoe. Sasa harakisheni mwende mkamlete baba yangu.’

Wakarudi nyumbani kumwambia baba yao habari hizo njema, na baadaye wakamleta Misri. Sasa Yosefu na baba yake wakakutana tena baada ya miaka mingi.

“Msipowasamehe watu makosa yao, naye Baba yenu hatawasamehe makosa yenu.”​—Mathayo 6:15