Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 55

Malaika wa Yehova Alimlinda Hezekia

Malaika wa Yehova Alimlinda Hezekia

Milki ya Ashuru ilikuwa imeushinda ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Sasa Senakeribu, mfalme wa Ashuru, alitaka kuushinda ufalme wa Yuda wa makabila mawili. Akaanza kuyateka majiji ya Yuda, moja baada ya lingine. Lakini jiji alilotaka zaidi kuliteka lilikuwa Yerusalemu. Senakeribu hakujua kwamba Yehova alikuwa akilinda Yerusalemu.

Hezekia, mfalme wa Yuda, akamlipa Senakeribu pesa nyingi ili asiliteke jiji la Yerusalemu. Ingawa Senakeribu alichukua pesa hizo, bado alituma jeshi lake lenye nguvu likashambulie Yerusalemu. Watu katika jiji la Yerusalemu waliogopa sana kwa sababu Waashuru walikuwa wakikaribia. Kisha Hezekia akawaambia hivi: ‘Msiogope. Waashuru wana nguvu, lakini Yehova atatufanya tuwe na nguvu nyingi kuliko wao.’

Senakeribu akamtuma mjumbe wake, Rabshake, kwenda Yerusalemu ili akawadhihaki watu. Rabshake akasimama nje ya jiji na kusema hivi kwa sauti: ‘Yehova hawezi kuwasaidia. Msimruhusu Hezekia awadanganye. Hakuna mungu anayeweza kuwalinda.’

Hezekia akamuuliza Yehova anachopaswa kufanya. Yehova akamjibu hivi: ‘Usiogopeshwe na maneno ya Rabshake. Senakeribu hataliteka jiji la Yerusalemu.’ Kisha, Hezekia akapokea barua kadhaa kutoka kwa Senakeribu. Barua hizo zilisema hivi: ‘Salimu amri. Yehova hawezi kuwakomboa.’ Hezekia akasali akisema hivi: ‘Tafadhali, Yehova, tukomboe, ili kila mtu ajue kwamba wewe ndiye Mungu wa pekee wa kweli.’ Yehova akamwambia hivi: ‘Mfalme wa Ashuru hataingia Yerusalemu. Nitalilinda jiji langu.’

Senakeribu alikuwa na uhakika kwamba angeteka jiji la Yerusalemu. Lakini usiku mmoja, Yehova akatuma malaika mahali ambapo askari-jeshi walikuwa wamepiga kambi nje ya jiji. Malaika huyo akawaua askari-jeshi 185,000! Mfalme Senakeribu akapoteza askari wake hodari zaidi. Hakuwa na la kufanya ila kurudi nyumbani akiwa ameshindwa. Yehova alimlinda Hezekia na jiji la Yerusalemu kama tu alivyokuwa ameahidi. Ikiwa ungekuwa Yerusalemu wakati huo, je, ungemtegemea Yehova?

“Malaika wa Yehova hupiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa Yeye, naye huwaokoa.”​—Zaburi 34:7