Mwanzo 29:1-35

  • Yakobo akutana na Raheli (1-14)

  • Yakobo ampenda Raheli (15-20)

  • Yakobo amwoa Lea na pia Raheli (21-29)

  • Wana wanne wa Yakobo waliozaliwa na Lea: Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda (30-35)

29  Baada ya hayo Yakobo akaendelea na safari yake, akafika katika nchi ya watu wa Mashariki.  Basi akaona kisima shambani na makundi matatu ya kondoo yakiwa yamelala kando yake, kwa sababu kwa kawaida wachungaji waliwanywesha kondoo wao maji ya kisima hicho. Kulikuwa na jiwe kubwa lililofunika kisima hicho.  Makundi yote ya kondoo yalipokusanywa hapo, wachungaji walilibingirisha jiwe lililofunika kisima hicho, nao wakawanywesha kondoo, kisha wakakifunika tena kisima kwa jiwe hilo.  Basi Yakobo akawauliza: “Ndugu zangu, mmetoka wapi?” wakamjibu: “Tumetoka Harani.”+  Akawauliza: “Je, mnamjua Labani+ mjukuu wa Nahori?”+ wakamjibu: “Ndio, tunamjua.”  Ndipo akawauliza: “Je, hajambo?” wakamjibu: “Hajambo. Ndiye yule Raheli+ binti yake anakuja na kondoo!”  Kisha akasema: “Bado ni adhuhuri. Si wakati wa kukusanya kondoo. Wanywesheni kondoo, kisha wapelekeni malishoni.”  Wakamwambia: “Haturuhusiwi kufanya hivyo mpaka makundi yote ya kondoo yakusanywe kisha jiwe libingirishwe kutoka juu ya kisima. Ndipo tutakapowanywesha kondoo.”  Alipokuwa akizungumza nao, Raheli akaja na kondoo wa baba yake, kwa maana alikuwa mchungaji. 10  Yakobo alipomwona Raheli binti ya Labani, ndugu ya mama yake, na kondoo wa Labani, mara moja Yakobo akakaribia na kulibingirisha jiwe linalofunika kisima, akawanywesha kondoo wa Labani ndugu ya mama yake. 11  Kisha Yakobo akambusu Raheli, akalia kwa sauti kubwa na kububujikwa na machozi. 12  Na Yakobo akaanza kumwambia Raheli kwamba yeye ni mtu wa ukoo wa* baba yake na kwamba yeye ni mwana wa Rebeka. Basi Raheli akakimbia na kwenda kumwambia baba yake. 13  Mara tu Labani+ aliposikia kuhusu Yakobo mwana wa dada yake, akakimbia kwenda kumpokea. Akamkumbatia na kumbusu na kumleta nyumbani kwake. Naye akaanza kumwambia Labani mambo hayo yote. 14  Labani akamwambia: “Kwa kweli wewe ni mfupa wangu na nyama yangu.”* Basi akakaa naye kwa mwezi mzima. 15  Kisha Labani akamwambia Yakobo: “Je, unitumikie bure kwa sababu tu wewe ni mtu wangu wa ukoo?*+ Niambie, ungependa mshahara wako uwe nini?”+ 16  Sasa Labani alikuwa na mabinti wawili. Yule mkubwa aliitwa Lea, na mdogo aliitwa Raheli.+ 17  Lakini macho ya Lea hayakuwa yaking’aa, lakini Raheli alikuwa mwanamke mwenye kuvutia sana, tena mrembo. 18  Yakobo alikuwa amempenda Raheli, kwa hiyo akasema: “Niko tayari kukutumikia kwa miaka saba ili nimpate Raheli binti yako mdogo.”+ 19  Labani akasema: “Ni afadhali nikupe wewe binti huyo kuliko kumpa mwanamume mwingine. Endelea kukaa nami.” 20  Basi Yakobo akamtumikia Labani kwa miaka saba ili ampate Raheli,+ lakini machoni pake miaka hiyo ilikuwa kama siku chache tu kwa sababu ya upendo aliokuwa nao kwa Raheli. 21  Kisha Yakobo akamwambia Labani: “Nipe mke wangu nilale naye kwa sababu siku zangu zimekwisha.” 22  Ndipo Labani akawakusanya wakaaji wote wa eneo hilo na kufanya karamu. 23  Lakini wakati wa jioni, akamchukua Lea binti yake na kumleta kwa Yakobo ili alale naye. 24  Pia, Labani akamchukua Zilpa kijakazi wake na kumpa Lea binti yake ili awe kijakazi wake.+ 25  Asubuhi Yakobo akagundua kwamba alipewa Lea! Kwa hiyo akamuuliza Labani: “Ni jambo gani hili ulilonitendea? Je, sikukutumikia ili nimpate Raheli? Kwa nini umenitendea hila?”+ 26  Labani akamjibu: “Si desturi yetu hapa kumwoza binti mdogo kabla ya yule aliyezaliwa kwanza. 27  Sherehekea juma la mwanamke huyu. Kisha utapewa mwanamke huyu mwingine ukinitumikia kwa miaka mingine saba.”+ 28  Yakobo akafanya hivyo, akasherehekea juma la mwanamke huyo, kisha akampa Raheli binti yake awe mke wake. 29  Isitoshe, Labani alimchukua Bilha+ kijakazi wake na kumpa Raheli binti yake ili awe kijakazi wake.+ 30  Kisha Yakobo akalala pia na Raheli, naye alimpenda Raheli kuliko Lea, akamtumikia Labani kwa miaka mingine saba.+ 31  Yehova alipoona kwamba Lea hapendwi,* alimwezesha kupata mimba,*+ lakini Raheli alikuwa tasa.+ 32  Kwa hiyo Lea akapata mimba na kuzaa mwana, akampa jina Rubeni,*+ kwa maana alisema: “Ni kwa sababu Yehova ameyaona mateso yangu,+ kwa maana sasa mume wangu ataanza kunipenda.” 33  Akapata mimba tena na kuzaa mwana, kisha akasema: “Ni kwa sababu Yehova amesikiliza, kwa maana sikupendwa, kwa hiyo amenipa huyu pia.” Basi akampa jina Simeoni.*+ 34  Akapata mimba tena na kuzaa mwana, kisha akasema: “Mara hii mume wangu ataungana nami, kwa sababu nimemzalia wana watatu.” Kwa hiyo mwana huyo akapewa jina Lawi.*+ 35  Akapata mimba tena na kuzaa mwana, akasema: “Wakati huu nitamsifu Yehova.” Kwa hiyo akampa jina Yuda.*+ Kisha akaacha kuzaa.

Maelezo ya Chini

Tnn., “ndugu ya.”
Au “mtu wangu wa ukoo niliye na uhusiano wa damu naye.”
Tnn., “ndugu yangu?”
Tnn., “anachukiwa.”
Tnn., “alifungua tumbo lake la uzazi.”
Maana yake “Tazama, Mwana!”
Maana yake “Kusikia.”
Maana yake “Kushikamana; Ungana.”
Maana yake “Aliyesifiwa; Kitu cha Kusifiwa.”