Mwanzo 12:1-20

  • Abramu ahama Harani na kwenda Kanaani (1-9)

    • Ahadi ya Mungu kwa Abramu (7)

  • Abramu na Sarai katika nchi ya Misri (10-20)

12  Yehova akamwambia Abramu: “Ondoka katika nchi yako na kutoka kwa watu wako wa ukoo na nyumba ya baba yako uende katika nchi nitakayokuonyesha;+  Nitakufanya kuwa taifa kubwa, nami nitakubariki, nami nitalifanya jina lako liwe kuu, nawe utakuwa baraka.+  Nitawabariki wale wanaokubariki, nami nitawalaani wale wanaokulaani,+ na familia zote duniani hakika zitabarikiwa* kupitia kwako.”+  Basi Abramu akaondoka kama Yehova alivyokuwa amemwambia, na Loti akaondoka pamoja naye. Abramu alikuwa na umri wa miaka 75 alipoondoka Harani.+  Abramu akamchukua Sarai+ mke wake na Loti mwana wa ndugu yake+ na mali zote ambazo walikuwa wamekusanya+ na watu ambao walikuwa wamejipatia huko Harani, nao wakaanza safari ya kwenda katika nchi ya Kanaani.+ Walipofika nchi ya Kanaani,  Abramu akasafiri nchini mpaka eneo la Shekemu,+ karibu na miti mikubwa ya More.+ Wakati huo Wakanaani walikuwa katika nchi hiyo.  Kisha Yehova akamtokea Abramu na kumwambia: “Nitaupa uzao wako*+ nchi hii.”+ Basi akamjengea Yehova madhabahu huko, aliyekuwa amemtokea.  Baadaye akatoka huko na kwenda katika eneo lenye milima upande wa mashariki wa Betheli+ na kupiga hema lake, jiji la Betheli likiwa upande wa magharibi na Ai+ upande wa mashariki. Huko, akamjengea Yehova+ madhabahu na kuanza kuliitia jina la Yehova.+  Baadaye, Abramu akavunja kambi na kusafiri kuelekea Negebu,+ akihamisha kambi yake kutoka sehemu moja hadi nyingine. 10  Sasa njaa kali ikatokea nchini, na Abramu akateremka kuelekea Misri ili akae huko kwa muda fulani,*+ kwa sababu njaa hiyo ilikuwa kali sana.+ 11  Alipokaribia kuingia Misri, akamwambia Sarai mke wake: “Tafadhali sikiliza! Ninajua kwamba wewe ni mwanamke mrembo sana.+ 12  Kwa hiyo Wamisri watakapokuona, hakika watasema, ‘Huyu ni mke wake.’ Halafu wataniua, lakini wewe watakuacha hai. 13  Tafadhali waambie wewe ni dada yangu, ili mambo yaniendee vema kwa sababu yako, nao hawataniua.”*+ 14  Mara tu Abramu alipoingia Misri, Wamisri waliona kwamba mwanamke huyo alikuwa mrembo sana. 15  Na maofisa wa Farao walimwona pia, nao wakaanza kumsifu mbele ya Farao, kwa hiyo mwanamke huyo akapelekwa katika nyumba ya Farao. 16  Farao alimtendea Abramu vema kwa sababu ya Sarai, naye akapata kondoo, ng’ombe, punda madume na majike, watumishi wa kiume na wa kike, na ngamia.+ 17  Ndipo Yehova akampiga Farao na watu wa nyumbani mwake kwa mapigo makali kwa sababu ya Sarai, mke wa Abramu.+ 18  Basi Farao akamwita Abramu na kumuuliza: “Kwa nini umenitendea hivi? Kwa nini hukuniambia kwamba yeye ni mke wako? 19  Kwa nini ulisema, ‘Huyu ni dada yangu,’+ hivi kwamba nilikuwa karibu kumchukua awe mke wangu? Mke wako ndiye huyu. Mchukue uende zako!” 20  Kwa hiyo Farao akawapa maofisa wake maagizo kumhusu, nao wakamwacha aende zake pamoja na mke wake na vyote alivyokuwa navyo.+

Maelezo ya Chini

Au “zitajipatia baraka.”
Tnn., “Nitaipa mbegu yako.”
Au “aishi huko akiwa mgeni.”
Au “na nafsi yangu itaendelea kuishi.”