Mwanzo 25:1-34

  • Abrahamu aoa tena (1-6)

  • Kifo cha Abrahamu (7-11)

  • Wana wa Ishmaeli (12-18)

  • Yakobo na Esau wazaliwa (19-26)

  • Esau auza haki yake ya mzaliwa wa kwanza (27-34)

25  Kisha Abrahamu akaoa mke mwingine, naye aliitwa Ketura.  Baada ya muda Ketura akamzalia Abrahamu watoto hawa: Zimrani, Yokshani, Medani, Midiani,+ Ishbaki, na Shua.+  Yokshani akamzaa Sheba na Dedani. Wana wa Dedani walikuwa Ashurimu, Letushimu, na Leumimu.  Wana wa Midiani walikuwa Efa, Eferi, Hanoki, Abida, na Eldaa. Hao wote walikuwa wana wa Ketura.  Baadaye Abrahamu alimpa Isaka+ kila kitu alichokuwa nacho,  lakini Abrahamu akawapa zawadi wana wa masuria wake. Alipokuwa bado hai, akawaagiza waende upande wa mashariki, mbali na Isaka mwanawe,+ katika nchi ya Mashariki.  Abrahamu aliishi miaka 175.  Kisha Abrahamu akakata pumzi na kufa baada ya kuishi maisha marefu, akiwa amezeeka na kuridhika, naye akazikwa pamoja na watu wake.*  Isaka na Ishmaeli wanawe wakamzika katika pango la Makpela kwenye shamba la Efroni mwana wa Zohari Mhiti, lililo mbele ya Mamre,+ 10  shamba ambalo Abrahamu alinunua kutoka kwa wana wa Hethi. Abrahamu alizikwa huko pamoja na Sara mke wake.+ 11  Baada ya kifo cha Abrahamu, Mungu aliendelea kumbariki Isaka mwanawe,+ na Isaka alikuwa akikaa karibu na Beer-lahai-roi.+ 12  Hii ndiyo historia ya Ishmaeli+ mwana wa Abrahamu ambaye Hagari+ Mmisri, kijakazi wa Sara, alimzalia Abrahamu. 13  Haya ndiyo majina ya wana wa Ishmaeli, kulingana na asili za koo zao: Nebayothi+ mzaliwa wa kwanza wa Ishmaeli, kisha Kedari,+ Adbeeli, Mibsamu,+ 14  Mishma, Duma, Masa, 15  Hadadi, Tema, Yeturi, Nafishi, na Kedema. 16  Hao ndio wana wa Ishmaeli, na hayo ndiyo majina yao kulingana na makao yao na kulingana na kambi zao,* wakuu 12 kulingana na koo zao.+ 17  Na Ishmaeli aliishi miaka 137. Kisha akakata pumzi na kufa, naye akazikwa pamoja na watu wake.* 18  Nao wakaanza kuishi katika nchi ya Havila+ karibu na Shuri,+ karibu na Misri, mpaka Ashuru. Aliishi karibu na ndugu zake wote.*+ 19  Na hii ndiyo historia ya Isaka mwana wa Abrahamu.+ Abrahamu alimzaa Isaka. 20  Isaka alikuwa na umri wa miaka 40 alipomwoa Rebeka, binti ya Bethueli,+ Mwaramu wa Padan-aramu, dada ya Labani yule Mwaramu. 21  Naye Isaka akaendelea kumsihi Yehova kumhusu mke wake kwa sababu alikuwa tasa; kwa hiyo Yehova akasikiliza ombi lake, na Rebeka mke wake akapata mimba. 22  Na wana waliokuwa tumboni mwake wakaanza kupambana,+ akasema: “Ikiwa hivi ndivyo mambo yalivyo, kwa nini niendelee kuishi?” Basi akamuuliza Yehova kuhusu jambo hilo. 23  Yehova akamwambia: “Mataifa mawili yamo tumboni mwako,+ na mataifa mawili yatatenganishwa kutoka ndani yako;+ na taifa moja litakuwa na nguvu kuliko lingine,+ na mkubwa atamtumikia mdogo.”+ 24  Wakati wake wa kuzaa ulipofika, tazama! mapacha walikuwa tumboni mwake. 25  Kisha wa kwanza akatoka, mwili wake wote ulikuwa mwekundu kama vazi la manyoya,+ kwa hiyo wakampa jina Esau.*+ 26  Kisha ndugu yake akatoka na mkono wake ulikuwa umeshika kisigino cha Esau,+ kwa hiyo akampa jina Yakobo.*+ Isaka alikuwa na umri wa miaka 60 Rebeka alipowazaa. 27  Wavulana hao walipoendelea kukua, Esau akawa mwindaji stadi,+ mtu wa mbugani, lakini Yakobo akawa mtu asiye na lawama, anayekaa katika mahema.+ 28  Na Isaka alimpenda Esau kwa sababu alikuwa akimletea nyama za porini, lakini Rebeka alimpenda Yakobo.+ 29  Siku moja Yakobo alipokuwa akichemsha mchuzi, Esau alirudi kutoka mbugani akiwa amechoka. 30  Kwa hiyo Esau akamwambia Yakobo: “Fanya haraka, tafadhali, nipe kiasi kidogo cha mchuzi huo mwekundu,* kwa maana nimechoka sana!”* Ndiyo sababu alipewa jina Edomu.*+ 31  Ndipo Yakobo akamwambia: “Kwanza niuzie haki yako ya mzaliwa wa kwanza!”+ 32  Esau akasema: “Ninakaribia kufa! Haki ya kuzaliwa ina faida gani kwangu?” 33  Yakobo akamwambia: “Niapie kwanza!” Basi akamwapia na kumuuzia Yakobo haki yake ya mzaliwa wa kwanza.+ 34  Ndipo Yakobo akampa Esau mkate na mchuzi wa dengu, akala na kunywa, kisha akainuka na kwenda zake. Hivyo, Esau akaidharau haki yake ya kuzaliwa.

Maelezo ya Chini

Tnn., “akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Au “kambi zao zilizozingirwa na kuta.”
Tnn., “akakusanywa kwa watu wake.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
Au labda, “Aliishi kwa uhasama na ndugu zake wote.”
Maana yake “Mwenye Nywele Nyingi.”
Maana yake “Anayeshika Kisigino; Anayechukua Nafasi ya Mwingine.”
Tnn., “chekundu, hiki chekundu.”
Au “nina njaa kali.”
Maana yake “Mwekundu.”