Mwanzo 26:1-35

  • Isaka na Rebeka wakiwa Gerari (1-11)

    • Mungu amhakikishia Isaka kwamba atatimiza ahadi yake (3-5)

  • Wagombania visima (12-25)

  • Agano kati ya Isaka na Abimeleki (26-33)

  • Wake wawili Wahiti wa Esau (34, 35)

26  Sasa kulikuwa na njaa kali nchini, mbali na ile njaa kali ya kwanza iliyotokea siku za Abrahamu,+ kwa hiyo Isaka akaenda Gerari kwa Abimeleki mfalme wa Wafilisti.  Kisha Yehova akamtokea Isaka na kumwambia: “Usishuke kwenda Misri. Kaa katika nchi nitakayokuonyesha.  Kaa kama mgeni katika nchi hii,+ nami nitaendelea kuwa pamoja nawe na kukubariki kwa sababu nitakupa wewe na uzao wako* nchi zote hizi,+ nami nitatimiza kiapo hiki nilichomwapia Abrahamu baba yako:+  ‘Nitaufanya uzao* wako uwe mwingi kama nyota za mbinguni;+ nami nitaupa uzao* wako nchi zote hizi;+ na kupitia uzao* wako mataifa yote ya dunia yatajipatia baraka,’+  kwa sababu Abrahamu aliisikiliza sauti yangu na kuendelea kutii matakwa yangu, amri zangu, maagizo yangu, na sheria zangu.”+  Kwa hiyo Isaka akaendelea kuishi Gerari.+  Wanaume wa huko walipomuuliza kuhusu mke wake, alikuwa akisema: “Huyu ni dada yangu.”+ Aliogopa kusema, “Ni mke wangu,” kwa kuwa alisema, “Huenda wanaume hawa wakaniua kwa sababu ya Rebeka,” kwa maana alikuwa mrembo sana.+  Baada ya muda kupita, Abimeleki mfalme wa Wafilisti alikuwa akiangalia nje dirishani, akamwona Isaka akimwonyesha mahaba* Rebeka mke wake.+  Mara moja Abimeleki akamwita Isaka na kumwambia: “Kumbe ni mke wako! Mbona ulisema, ‘Huyu ni dada yangu’?” Isaka akamwambia: “Nilisema hivyo kwa sababu niliogopa nitauawa kwa sababu yake.”+ 10  Lakini Abimeleki akamuuliza: “Ni jambo gani hili ulilotutendea?+ Ingekuwa rahisi kwa yeyote kulala na mke wako, nawe ungetuletea hatia!”+ 11  Ndipo Abimeleki akawaamuru watu wote akisema: “Yeyote atakayemgusa mtu huyu na mke wake hakika atauawa!” 12  Na Isaka akaanza kupanda mbegu katika nchi hiyo, na mwaka huo alivuna mara 100 zaidi ya mbegu alizopanda, kwa kuwa Yehova alikuwa akimbariki.+ 13  Mwanamume huyo akatajirika, naye akaendelea kupata ufanisi mpaka akawa tajiri sana. 14  Alipata makundi ya kondoo na makundi ya ng’ombe na kundi kubwa la watumishi,+ nao Wafilisti wakaanza kumwonea wivu. 15  Kwa hiyo Wafilisti wakachukua udongo na kuvifukia visima vyote ambavyo watumishi wa baba yake walikuwa wamechimba siku za Abrahamu.+ 16  Kisha Abimeleki akamwambia Isaka: “Ondoka katika eneo letu, kwa sababu umekuwa na nguvu nyingi kuliko sisi.” 17  Kwa hiyo Isaka akaondoka huko na kupiga kambi katika bonde* la Gerari+ na kuanza kuishi huko. 18  Na Isaka akavichimbua visima vilivyokuwa vimechimbwa katika siku za Abrahamu baba yake lakini ambavyo Wafilisti walivifukia baada ya Abrahamu kufa,+ akavipa majina yaleyale ambayo baba yake alivipa.+ 19  Watumishi wa Isaka walipokuwa wakichimba bondeni,* walipata kisima cha maji safi. 20  Nao wachungaji wa Gerari wakaanza kugombana na wachungaji wa Isaka, wakisema: “Maji haya ni yetu!” Basi akakiita kisima hicho Eseki,* kwa sababu walikuwa wamegombana naye. 21  Nao wakaanza kuchimba kisima kingine, wakaanza kukigombania pia. Basi akakiita Sitna.* 22  Baadaye akaondoka huko na kuchimba kisima kingine, lakini hawakukigombania. Basi akakiita Rehobothi* na kusema: “Ni kwa sababu sasa Yehova ametupa nafasi ya kutosha naye ametufanya tuongezeke nchini.”+ 23  Kisha akapanda kutoka huko na kwenda Beer-sheba.+ 24  Yehova akamtokea usiku huo na kumwambia: “Mimi ni Mungu wa Abrahamu baba yako.+ Usiogope,+ kwa maana niko pamoja nawe, nami nitakubariki na kufanya uzao* wako uwe mwingi kwa sababu ya Abrahamu mtumishi wangu.”+ 25  Basi akajenga madhabahu huko na kuliitia jina la Yehova.+ Na Isaka akapiga hema lake huko,+ na watumishi wake wakachimba kisima huko. 26  Baadaye Abimeleki akamtembelea kutoka Gerari akiwa pamoja na Ahuzathi mshauri wake na Fikoli mkuu wa jeshi lake.+ 27  Basi Isaka akawauliza: “Kwa nini mmenitembelea, ilhali mlinichukia na kunifukuza katika eneo lenu?” 28  Wakamwambia: “Tumeona wazi kwamba Yehova amekuwa pamoja nawe.+ Basi tukasema, ‘Tafadhali, na kuwe na kiapo cha wajibu kati yetu sisi na wewe, na tufanye agano pamoja nawe+ 29  kwamba hutatutendea jambo lolote baya kama vile ambavyo hatujakudhuru, kama ujuavyo tulikutendea mema tu na tulikuruhusu uende zako kwa amani. Sasa wewe ni mbarikiwa wa Yehova.’” 30  Kisha akawafanyia karamu, nao wakala na kunywa. 31  Asubuhi wakaamka mapema na kufanya kiapo kati yao.+ Kisha Isaka akawaruhusu waende zao, nao wakaondoka kwa amani. 32  Siku hiyo watumishi wa Isaka walikuja na kumwambia kuhusu kisima walichokuwa wamechimba,+ wakasema: “Tumepata maji!” 33  Kwa hiyo akakiita Shiba. Ndiyo sababu tangu siku hiyo jiji hilo linaitwa Beer-sheba.+ 34  Esau alipokuwa na umri wa miaka 40, alimwoa Yudithi binti ya Beeri Mhiti na pia Basemathi binti ya Eloni Mhiti.+ 35  Walikuwa chanzo cha huzuni kubwa* kwa Isaka na Rebeka.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu.”
Tnn., “mbegu.”
Tnn., “mbegu.”
Au “akimkumbatia.”
Au “korongo.”
Au “korongoni.”
Maana yake “Ugomvi.”
Maana yake “Shtaka.”
Maana yake “Maeneo Makubwa.”
Tnn., “mbegu.”
Tnn., “uchungu mkali wa rohoni.”