Mwanzo 28:1-22

  • Isaka amtuma Yakobo Padan-aramu (1-9)

  • Ndoto ya Yakobo akiwa Betheli (10-22)

    • Mungu amhakikishia Yakobo kwamba atatimiza ahadi yake (13-15)

28  Basi Isaka akamwita Yakobo, akambariki na kumwamuru hivi: “Usioe mke kutoka kwa mabinti wa Kanaani.+  Nenda Padan-aramu katika nyumba ya Bethueli, baba ya mama yako, na uoe mke kutoka kwa mabinti wa Labani,+ ndugu ya mama yako.  Mungu Mweza-Yote atakubariki na kukufanya uwe na wazao wengi na kuongezeka, nawe hakika utakuwa kusanyiko la mataifa.+  Naye atakupa wewe na uzao wako* baraka ambayo alimwahidi Abrahamu,+ ili uimiliki nchi ambamo umekuwa ukiishi kama mgeni, nchi ambayo Mungu alimpa Abrahamu.”+  Kwa hiyo Isaka akamruhusu Yakobo aondoke, naye akaenda Padan-aramu kwa Labani mwana wa Bethueli Mwaramu,+ ndugu ya Rebeka,+ mama ya Yakobo na Esau.  Esau akaona kwamba Isaka alikuwa amembariki Yakobo na kumwambia aende Padan-aramu kuoa mke kutoka huko na kwamba alipombariki, alimwamuru, “Usioe mke kutoka kwa mabinti wa Kanaani,”+  na kwamba Yakobo alimtii baba yake na mama yake na kwenda Padan-aramu.+  Ndipo Esau akatambua kwamba Isaka baba yake hakupendezwa na mabinti wa Kanaani,+  kwa hiyo Esau akaenda kwa Ishmaeli mwana wa Abrahamu na kumwoa Mahalathi binti ya Ishmaeli, dada ya Nebayothi, kuongezea wake wengine aliokuwa nao.+ 10  Yakobo akaondoka Beer-sheba na kuendelea na safari kuelekea Harani.+ 11  Baada ya muda akafika mahali fulani, akajitayarisha kulala hapo kwa sababu jua lilikuwa limetua. Kwa hiyo akachukua jiwe moja la mahali pale na kuliweka chini ili apumzishe kichwa chake juu yake, akalala hapo.+ 12  Kisha akaota ndoto, na tazama! Kulikuwa na ngazi iliyosimamishwa duniani, na kilele chake kilifika mpaka mbinguni; na kulikuwa na malaika wa Mungu waliokuwa wakipanda na kushuka kwenye ngazi hiyo.+ 13  Na tazama! Yehova alikuwa amesimama juu yake, naye akasema: “Mimi ni Yehova Mungu wa Abrahamu baba yako na Mungu wa Isaka.+ Nchi unayoilalia, nitakupa wewe na uzao wako.*+ 14  Na hakika uzao wako utakuwa kama chembe za mavumbi ya ardhi,+ nawe utaenea mpaka upande wa magharibi na upande wa mashariki na upande wa kaskazini na upande wa kusini, na kupitia kwako na kupitia uzao wako familia zote duniani hakika zitabarikiwa.*+ 15  Niko pamoja nawe, nami nitakulinda popote utakapokwenda, nami nitakurudisha kwenye nchi hii.+ Sitakuacha mpaka nitakapofanya mambo niliyokuahidi.”+ 16  Kisha Yakobo akaamka kutoka usingizini na kusema: “Kwa kweli Yehova yuko mahali hapa, nami sikujua.” 17  Naye akaogopa na kusema: “Mahali hapa panaogopesha kwelikweli! Bila shaka hapa ni nyumba ya Mungu,+ na hili ndilo lango la mbingu.”+ 18  Kwa hiyo Yakobo akaamka asubuhi na mapema na kuchukua lile jiwe alilokuwa amepumzisha kichwa chake juu yake, akalisimamisha kama nguzo na kumimina mafuta juu yake.+ 19  Basi akapaita mahali hapo Betheli,* lakini hapo awali jiji hilo liliitwa Luzi.+ 20  Kisha Yakobo akaweka nadhiri hii: “Ikiwa Mungu ataendelea kuwa pamoja nami na kunilinda katika safari yangu na kunipa mkate wa kula na mavazi ya kuvaa 21  nami nirudi kwa amani katika nyumba ya baba yangu, kwa hakika Yehova atakuwa amethibitika kuwa Mungu wangu. 22  Na jiwe hili ambalo nimelisimamisha kama nguzo litakuwa nyumba ya Mungu,+ nami sitakosa kukupa sehemu ya kumi ya vitu vyote utakavyonipa.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “mbegu yako.”
Au “zitajipatia baraka.”
Maana yake “Nyumba ya Mungu.”