Mwanzo 33:1-20

  • Yakobo akutana na Esau (1-16)

  • Yakobo asafiri kwenda Shekemu (17-20)

33  Sasa Yakobo akainua macho yake na kumwona Esau akija pamoja na wanaume 400.+ Kwa hiyo akawagawa watoto kati ya Lea, Raheli, na wale vijakazi wawili.+  Akawaweka vijakazi na watoto wao mbele,+ kisha Lea na watoto wake,+ halafu Raheli+ na Yosefu nyuma yao.  Kisha yeye mwenyewe akaenda mbele yao, akainama mpaka chini mara saba huku akimkaribia ndugu yake.  Lakini Esau akakimbia kukutana naye, akamkumbatia na kumbusu, nao wakatokwa na machozi.  Alipoinua macho yake na kuona wanawake na watoto, akauliza: “Ni nani hawa walio pamoja nawe?” Yakobo akamwambia: “Ni watoto ambao Mungu amenipa kwa fadhili mimi mtumishi wako.”+  Ndipo wale vijakazi wakaja mbele na watoto wao na kuinama chini,  Lea pia akaja mbele na watoto wake, nao wakainama chini. Kisha Yosefu akaja mbele na Raheli, nao wakainama chini.+  Esau akauliza: “Msafara huu wote ni wa nini?”+ Yakobo akamjibu: “Nimekuja ili kupata kibali machoni pako, bwana wangu.”+  Esau akasema: “Nina mali nyingi sana, ndugu yangu.+ Usinipe mali zako.” 10  Lakini Yakobo akasema: “Hapana, tafadhali nakusihi. Ikiwa nimepata kibali machoni pako, pokea zawadi yangu kutoka mkononi mwangu, kwa sababu nimekuletea ili niuone uso wako. Nami nimeona uso wako kana kwamba nimeona uso wa Mungu, kwa maana umenipokea kwa furaha.+ 11  Tafadhali pokea zawadi yangu ya baraka uliyoletewa,+ kwa sababu Mungu amenibariki, nami nina kila kitu ninachohitaji.”+ Basi akaendelea kumsihi apokee zawadi hiyo, naye akaichukua. 12  Baadaye Esau akasema: “Tuondoke, tufunge safari, acha nikutangulie.” 13  Lakini Yakobo akamwambia: “Bwana wangu unajua kwamba watoto ni dhaifu+ nami nina kondoo na ng’ombe wanaonyonyesha. Wakipelekwa haraka-haraka kwa siku moja, wanyama wote watakufa. 14  Tafadhali, bwana wangu, nitangulie mimi mtumishi wako, lakini nitaendelea na safari polepole kulingana na mwendo wa mifugo na watoto mpaka nitakapofika kwako bwana wangu huko Seiri.”+ 15  Esau akasema: “Tafadhali, naomba niwaache baadhi ya watu wangu pamoja nawe.” Yakobo akasema, “Kwa nini ufanye hivyo? Naomba tu nipate kibali machoni pako, bwana wangu.” 16  Basi siku hiyo Esau akasafiri kurudi Seiri. 17  Naye Yakobo akaenda Sukothi,+ naye akajijengea nyumba na mabanda ya mifugo yake. Ndiyo sababu alipaita mahali hapo Sukothi.* 18  Baada ya kuondoka Padan-aramu,+ Yakobo akafika salama salimini kwenye jiji la Shekemu+ katika nchi ya Kanaani,+ naye akapiga kambi karibu na jiji hilo. 19  Kisha akanunua kisehemu fulani cha shamba kutoka kwa wana wa Hamori, baba ya Shekemu, kwa vipande 100 vya fedha, akapiga hema lake hapo.+ 20  Akajenga madhabahu huko na kuiita Mungu, Mungu wa Israeli.+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Mabanda; Vibanda.”