Ayubu 1:1-22

  • Utimilifu wa Ayubu na mali zake (1-5)

  • Shetani atilia shaka nia ya Ayubu (6-12)

  • Ayubu apoteza mali na watoto wake (13-19)

  • Ayubu hamlaumu Mungu (20-22)

1  Palikuwa na mtu katika nchi ya Usi aliyeitwa Ayubu.*+ Alikuwa mtu mnyoofu na mtimilifu;*+ alimwogopa Mungu na kuepuka uovu.+  Alikuwa na wana saba na mabinti watatu.  Mifugo yake ilikuwa kondoo 7,000, ngamia 3,000, ng’ombe 1,000,* na punda 500, naye alikuwa na watumishi wengi sana, na hivyo akawa mkuu kuliko watu wote wa Mashariki.  Kila mmoja wa wanawe alikuwa akifanya karamu katika nyumba yake siku yake iliyopangwa.* Nao walikuwa wakiwaalika dada zao watatu ili wale na kunywa pamoja nao.  Baada ya vipindi vya siku za karamu kwisha, Ayubu alikuwa akiwaita ili awatakase. Naye alikuwa akiamka asubuhi na mapema na kutoa dhabihu za kuteketezwa+ kwa ajili ya kila mmoja wao. Kwa maana Ayubu alisema: “Labda wanangu wametenda dhambi na kumtukana Mungu moyoni mwao.” Hivyo ndivyo Ayubu alivyofanya sikuzote.+  Basi siku ilifika ambayo wana wa Mungu*+ wa kweli waliingia na kusimama mbele za Yehova,+ Shetani+ pia akaingia kati yao.+  Ndipo Yehova akamuuliza Shetani: “Umetoka wapi?” Shetani akamjibu Yehova: “Nimetoka kuzururazurura na kutembeatembea duniani.”+  Yehova akamwambia Shetani: “Je, umemwona* mtumishi wangu Ayubu? Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani. Yeye ni mtu mnyoofu na mtimilifu,*+ anayemwogopa Mungu na kuepuka uovu.”  Ndipo Shetani akamjibu Yehova: “Je, Ayubu anamwogopa Mungu bure?+ 10  Je, wewe hukuweka ukuta wa ulinzi kumzunguka yeye+ na nyumba yake na kila kitu alicho nacho? Umeibariki kazi ya mikono yake,+ na mifugo yake imeenea nchini. 11  Lakini, ili mambo yabadilike, nyoosha mkono wako na upige kila kitu alicho nacho, na kwa hakika atakutukana mbele za uso wako mwenyewe.” 12  Kisha Yehova akamwambia Shetani: “Tazama! Kila kitu alicho nacho kimo mikononi mwako.* Ila tu usimguse mwanamume huyo!” Kwa hiyo Shetani akaondoka mbele za* Yehova.+ 13  Sasa siku ambayo wanawe na mabinti zake walikuwa wakila na kunywa divai katika nyumba ya ndugu yao mkubwa,+ 14  mjumbe akaja kwa Ayubu na kusema: “Ng’ombe walikuwa wakilima na punda walikuwa wakilisha kando yao 15  Wasabea walipotushambulia na kuwachukua, wakawaua watumishi kwa upanga. Nimeponyoka mimi peke yangu, nami nimekuletea habari.” 16  Alipokuwa bado anaongea, mwingine akaja na kusema: “Moto kutoka kwa Mungu ulianguka kutoka mbinguni ukawateketeza* kabisa kondoo na watumishi! Nimeponyoka mimi peke yangu, nami nimekuletea habari.” 17  Alipokuwa bado anaongea, mwingine akaja na kusema: “Wakaldayo+ walijipanga katika makundi matatu, wakavamia ngamia na kuwachukua, nao wakawaua watumishi kwa upanga. Nimeponyoka mimi peke yangu, nami nimekuletea habari.” 18  Alipokuwa bado anaongea, mwingine akaja na kusema: “Wana wako na mabinti wako walikuwa wakila na kunywa divai katika nyumba ya ndugu yao mkubwa. 19  Kwa ghafla upepo mkali ukaja kutoka nyikani, ukapiga pembe nne za nyumba hiyo, ikawaangukia vijana hao, nao wakafa. Nimeponyoka mimi peke yangu, nami nimekuletea habari.” 20  Ndipo Ayubu akasimama, akararua vazi lake na kunyoa nywele za kichwa chake; kisha akaanguka chini, akainama 21  na kusema: “Nilitoka tumboni mwa mama yangu nikiwa uchi,Nami nitarudi nikiwa uchi.+ Yehova ametoa,+ na Yehova amechukua. Jina la Yehova na liendelee kusifiwa.” 22  Katika hayo yote, Ayubu hakutenda dhambi wala hakumlaumu Mungu kwa kutenda jambo lolote baya.*

Maelezo ya Chini

Huenda jina hili linamaanisha “Kitu Kinachochukiwa.”
Au “mtu asiye na lawama na mnyoofu.”
Tnn., “jozi 500 za ng’ombe.”
Au “katika nyumba ya kila mmoja kwa zamu yake.”
Msemo wa Kiebrania unaorejelea malaika, wana wa Mungu.
Tnn., “umeuweka moyo wako juu ya.”
Au “mtu asiye na lawama na mnyoofu.”
Au “kiko chini ya mamlaka yako.”
Tnn., “mbele za uso wa.”
Au labda, “Radi ilianguka kutoka mbinguni ikawateketeza.”
Au “hakusema kwamba Mungu ametenda jambo lolote lisilofaa.”