Hesabu 14:1-45
14 Basi Waisraeli wote wakalia kwa sauti na kutokwa na machozi usiku kucha.+
2 Waisraeli wote wakaanza kumnung’unikia Musa na Haruni,+ na wote wakawalalamikia wakisema: “Laiti tungalifia katika nchi ya Misri, au laiti tungalifia hapa nyikani!
3 Kwa nini Yehova anatuleta kwenye nchi hii ili tuuawe kwa upanga?+ Wake zetu na watoto wetu watakuwa mateka.+ Je, si afadhali turudi Misri?”+
4 Hata waliambiana: “Na tuchague kiongozi, turudi Misri!”+
5 Ndipo Musa na Haruni wakaanguka chini kifudifudi mbele ya Waisraeli wote waliokuwa wamekusanyika.
6 Yoshua+ mwana wa Nuni na Kalebu+ mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwa watu walioipeleleza nchi, wakayararua mavazi yao,
7 na kuwaambia hivi Waisraeli wote: “Nchi tuliyoenda kuipeleleza ni nchi nzuri sana, nzuri kwelikweli.+
8 Ikiwa Yehova amependezwa nasi, kwa hakika atatuingiza katika nchi hii na kutupatia iwe yetu, nchi inayotiririka maziwa na asali.+
9 Lakini msimwasi Yehova, nanyi msiwaogope watu wa nchi hiyo,+ kwa maana tutawashinda kwa urahisi.* Ulinzi wao umeondolewa, na Yehova yuko pamoja nasi.+ Msiwaogope.”
10 Hata hivyo, Waisraeli wote wakasema wapigwe mawe.+ Lakini utukufu wa Yehova ukatokea juu ya hema la mkutano machoni pa Waisraeli wote.+
11 Kisha Yehova akamwambia Musa: “Watu hawa wataendelea kunidharau mpaka lini,+ watakataa kuniamini mpaka lini licha ya miujiza yote niliyofanya miongoni mwao?+
12 Acha niwapige kwa ugonjwa hatari* na kuwafukuza, na acha nikufanye wewe kuwa taifa kubwa zaidi na lenye nguvu zaidi kuliko wao.”+
13 Lakini Musa akamwambia Yehova: “Kisha Wamisri, ambao kati yao uliwatoa watu hawa kwa nguvu zako, watasikia habari hizo,+
14 nao watawaambia wakaaji wa nchi hii. Wakaaji hao pia wamesikia kwamba wewe, Yehova, uko miongoni mwa watu hawa,+ nawe umewatokea uso kwa uso.+ Wewe ni Yehova, na wingu lako limesimama juu yao, nawe unawatangulia katika nguzo ya wingu wakati wa mchana na katika nguzo ya moto wakati wa usiku.+
15 Ukiwaua watu hawa wote mara moja, mataifa ambayo yamesikia sifa zako yatasema,
16 ‘Yehova alishindwa kuwapeleka watu hawa katika nchi ambayo aliapa kuwa angewapa ndiyo sababu aliwachinja nyikani.’+
17 Sasa, Ee Yehova, tafadhali, acha nguvu zako kuu zionekane, kama ulivyoahidi uliposema,
18 ‘Mimi Yehova, si mwepesi wa hasira, nina upendo mwingi mshikamanifu,*+ ninasamehe makosa na uovu, lakini sikosi kamwe kuwaadhibu wenye hatia, ninawaadhibu wana na wajukuu kufikia kizazi cha tatu na cha nne kwa sababu ya makosa ya baba zao.’+
19 Tafadhali, wasamehe watu hawa dhambi zao kulingana na upendo wako mwingi mshikamanifu, kama ambavyo umekuwa ukiwasamehe tangu walipotoka Misri mpaka sasa.”+
20 Basi Yehova akasema: “Nimewasamehe kama ulivyoomba.+
21 Lakini, kwa hakika kama niishivyo, dunia yote itajaa utukufu wa Yehova.+
22 Hata hivyo, hakuna mtu hata mmoja aliyeona utukufu wangu na miujiza+ niliyofanya nchini Misri na nyikani ambaye bado ananijaribu+ mara hizi kumi na kukataa kusikiliza sauti yangu+
23 ataiona nchi niliyoapa kwamba nitawapa baba zao. Hakuna mtu hata mmoja anayenidharau atakayeiona.+
24 Lakini kwa sababu mtumishi wangu Kalebu+ alikuwa na roho tofauti naye aliendelea kunifuata kwa moyo wote, kwa hakika nitamwingiza katika nchi aliyoenda kuipeleleza, na wazao wake wataimiliki.+
25 Kwa kuwa Waamaleki na Wakanaani+ wanaishi bondeni, kesho geukeni mwelekee nyikani kupitia njia ya Bahari Nyekundu.”+
26 Kisha Yehova akamwambia Musa na Haruni:
27 “Umati huu wa watu waovu utaendelea kuninung’unikia mpaka lini?+ Nimesikia manung’uniko ya Waisraeli juu yangu.+
28 Waambie, ‘“Kwa hakika kama ninavyoishi,” asema Yehova, “nitawatendea mambo yaleyale niliyosikia mkisema!+
29 Maiti zenu zitaanguka katika nyika hii,+ naam, ninyi nyote mlioninung’unikia, kila mtu aliyeandikishwa mwenye umri wa kuanzia miaka 20 na zaidi.+
30 Hakuna hata mmoja wenu atakayeingia katika nchi niliyoapa kwamba mtaishi ndani yake,+ isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune na Yoshua mwana wa Nuni.+
31 “‘“Na watoto wenu ambao mlisema kwamba watakuwa mateka,+ nitawaingiza katika nchi ambayo mmeikataa, nao wataijua.+
32 Lakini maiti zenu zitaanguka katika nyika hii.
33 Wana wenu watakuwa wachungaji nyikani kwa miaka 40,+ nao lazima wateseke kwa sababu ya matendo yenu ya kukosa uaminifu* mpaka mtu wenu wa mwisho atakapofia nyikani.+
34 Mtateseka kwa sababu ya makosa yenu kwa miaka 40,+ sawa na siku 40+ ambazo mliipeleleza nchi, yaani, siku moja kwa mwaka mmoja, siku moja kwa mwaka mmoja, kwa maana mtajionea matokeo ya kunipinga mimi.*
35 “‘“Mimi, Yehova, nimesema. Hivi ndivyo nitakavyoutendea umati huu wa watu waovu, ambao umekusanyika pamoja dhidi yangu: Wataishia humu nyikani, naam, watafia humu.+
36 Wanaume ambao Musa aliwatuma kuipeleleza nchi, wakaleta habari mbaya kuhusu nchi hiyo na kufanya Waisraeli wote wamnung’unikie Musa,+
37 naam, wanaume hao walioleta habari mbaya kuhusu nchi hiyo watauawa mbele za Yehova.+
38 Lakini Yoshua mwana wa Nuni na Kalebu mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwa wanaume walioenda kuipeleleza nchi, ndio watakaoendelea kuishi.”’”+
39 Musa alipowaambia Waisraeli wote maneno hayo, watu walianza kuomboleza kwa uchungu mwingi.
40 Hata waliamka asubuhi na mapema na kujaribu kupanda juu mlimani, wakisema: “Tuko tayari kupanda mpaka mahali ambapo Yehova alituambia, kwa maana tumetenda dhambi.”+
41 Lakini Musa akawaambia: “Kwa nini mnakiuka agizo la Yehova? Hamtafanikiwa.
42 Msipande kwenda huko, kwa sababu Yehova hayuko pamoja nanyi; mtashindwa na maadui wenu.+
43 Kwa maana Waamaleki na Wakanaani watakabiliana nanyi huko,+ nao watawaangamiza kwa upanga. Kwa sababu mliacha kumfuata Yehova, Yehova hatakuwa pamoja nanyi.”+
44 Hata hivyo, kwa kimbelembele wakapanda kuelekea mlimani,+ lakini sanduku la agano la Yehova lilibaki katikati ya kambi, na Musa pia alibaki.+
45 Ndipo Waamaleki na Wakanaani walioishi kwenye mlima huo wakashuka na kuanza kuwashambulia, wakawatawanya mpaka Horma.+
Maelezo ya Chini
^ Tnn., “wao ni mkate kwetu.”
^ Au “tauni.”
^ Au “fadhili nyingi zenye upendo.”
^ Tnn., “ya ukahaba.”
^ Au “ya kuwa maadui wangu.”