Hesabu 14:1-45

  • Watu wataka kurudi Misri (1-10)

    • Yoshua na Kalebu waleta habari nzuri (6-9)

  • Yehova akasirika; Musa aingilia kati (11-19)

  • Adhabu: miaka 40 nyikani (20-38)

  • Waisraeli washindwa na Waamaleki (39-45)

14  Basi Waisraeli wote wakalia kwa sauti na kutokwa na machozi usiku kucha.+  Waisraeli wote wakaanza kumnung’unikia Musa na Haruni,+ na wote wakawalalamikia wakisema: “Laiti tungalifia katika nchi ya Misri, au laiti tungalifia hapa nyikani!  Kwa nini Yehova anatuleta kwenye nchi hii ili tuuawe kwa upanga?+ Wake zetu na watoto wetu watakuwa mateka.+ Je, si afadhali turudi Misri?”+  Hata waliambiana: “Na tuchague kiongozi, turudi Misri!”+  Ndipo Musa na Haruni wakaanguka chini kifudifudi mbele ya Waisraeli wote waliokuwa wamekusanyika.  Yoshua+ mwana wa Nuni na Kalebu+ mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwa watu walioipeleleza nchi, wakayararua mavazi yao,  na kuwaambia hivi Waisraeli wote: “Nchi tuliyoenda kuipeleleza ni nchi nzuri sana, nzuri kwelikweli.+  Ikiwa Yehova amependezwa nasi, kwa hakika atatuingiza katika nchi hii na kutupatia iwe yetu, nchi inayotiririka maziwa na asali.+  Lakini msimwasi Yehova, nanyi msiwaogope watu wa nchi hiyo,+ kwa maana tutawashinda kwa urahisi.* Ulinzi wao umeondolewa, na Yehova yuko pamoja nasi.+ Msiwaogope.” 10  Hata hivyo, Waisraeli wote wakasema wapigwe mawe.+ Lakini utukufu wa Yehova ukatokea juu ya hema la mkutano machoni pa Waisraeli wote.+ 11  Kisha Yehova akamwambia Musa: “Watu hawa wataendelea kunidharau mpaka lini,+ watakataa kuniamini mpaka lini licha ya miujiza yote niliyofanya miongoni mwao?+ 12  Acha niwapige kwa ugonjwa hatari* na kuwafukuza, na acha nikufanye wewe kuwa taifa kubwa zaidi na lenye nguvu zaidi kuliko wao.”+ 13  Lakini Musa akamwambia Yehova: “Kisha Wamisri, ambao kati yao uliwatoa watu hawa kwa nguvu zako, watasikia habari hizo,+ 14  nao watawaambia wakaaji wa nchi hii. Wakaaji hao pia wamesikia kwamba wewe, Yehova, uko miongoni mwa watu hawa,+ nawe umewatokea uso kwa uso.+ Wewe ni Yehova, na wingu lako limesimama juu yao, nawe unawatangulia katika nguzo ya wingu wakati wa mchana na katika nguzo ya moto wakati wa usiku.+ 15  Ukiwaua watu hawa wote mara moja, mataifa ambayo yamesikia sifa zako yatasema, 16  ‘Yehova alishindwa kuwapeleka watu hawa katika nchi ambayo aliapa kuwa angewapa ndiyo sababu aliwachinja nyikani.’+ 17  Sasa, Ee Yehova, tafadhali, acha nguvu zako kuu zionekane, kama ulivyoahidi uliposema, 18  ‘Mimi Yehova, si mwepesi wa hasira, nina upendo mwingi mshikamanifu,*+ ninasamehe makosa na uovu, lakini sikosi kamwe kuwaadhibu wenye hatia, ninawaadhibu wana na wajukuu kufikia kizazi cha tatu na cha nne kwa sababu ya makosa ya baba zao.’+ 19  Tafadhali, wasamehe watu hawa dhambi zao kulingana na upendo wako mwingi mshikamanifu, kama ambavyo umekuwa ukiwasamehe tangu walipotoka Misri mpaka sasa.”+ 20  Basi Yehova akasema: “Nimewasamehe kama ulivyoomba.+ 21  Lakini, kwa hakika kama niishivyo, dunia yote itajaa utukufu wa Yehova.+ 22  Hata hivyo, hakuna mtu hata mmoja aliyeona utukufu wangu na miujiza+ niliyofanya nchini Misri na nyikani ambaye bado ananijaribu+ mara hizi kumi na kukataa kusikiliza sauti yangu+ 23  ataiona nchi niliyoapa kwamba nitawapa baba zao. Hakuna mtu hata mmoja anayenidharau atakayeiona.+ 24  Lakini kwa sababu mtumishi wangu Kalebu+ alikuwa na roho tofauti naye aliendelea kunifuata kwa moyo wote, kwa hakika nitamwingiza katika nchi aliyoenda kuipeleleza, na wazao wake wataimiliki.+ 25  Kwa kuwa Waamaleki na Wakanaani+ wanaishi bondeni, kesho geukeni mwelekee nyikani kupitia njia ya Bahari Nyekundu.”+ 26  Kisha Yehova akamwambia Musa na Haruni: 27  “Umati huu wa watu waovu utaendelea kuninung’unikia mpaka lini?+ Nimesikia manung’uniko ya Waisraeli juu yangu.+ 28  Waambie, ‘“Kwa hakika kama ninavyoishi,” asema Yehova, “nitawatendea mambo yaleyale niliyosikia mkisema!+ 29  Maiti zenu zitaanguka katika nyika hii,+ naam, ninyi nyote mlioninung’unikia, kila mtu aliyeandikishwa mwenye umri wa kuanzia miaka 20 na zaidi.+ 30  Hakuna hata mmoja wenu atakayeingia katika nchi niliyoapa kwamba mtaishi ndani yake,+ isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune na Yoshua mwana wa Nuni.+ 31  “‘“Na watoto wenu ambao mlisema kwamba watakuwa mateka,+ nitawaingiza katika nchi ambayo mmeikataa, nao wataijua.+ 32  Lakini maiti zenu zitaanguka katika nyika hii. 33  Wana wenu watakuwa wachungaji nyikani kwa miaka 40,+ nao lazima wateseke kwa sababu ya matendo yenu ya kukosa uaminifu* mpaka mtu wenu wa mwisho atakapofia nyikani.+ 34  Mtateseka kwa sababu ya makosa yenu kwa miaka 40,+ sawa na siku 40+ ambazo mliipeleleza nchi, yaani, siku moja kwa mwaka mmoja, siku moja kwa mwaka mmoja, kwa maana mtajionea matokeo ya kunipinga mimi.* 35  “‘“Mimi, Yehova, nimesema. Hivi ndivyo nitakavyoutendea umati huu wa watu waovu, ambao umekusanyika pamoja dhidi yangu: Wataishia humu nyikani, naam, watafia humu.+ 36  Wanaume ambao Musa aliwatuma kuipeleleza nchi, wakaleta habari mbaya kuhusu nchi hiyo na kufanya Waisraeli wote wamnung’unikie Musa,+ 37  naam, wanaume hao walioleta habari mbaya kuhusu nchi hiyo watauawa mbele za Yehova.+ 38  Lakini Yoshua mwana wa Nuni na Kalebu mwana wa Yefune, waliokuwa miongoni mwa wanaume walioenda kuipeleleza nchi, ndio watakaoendelea kuishi.”’”+ 39  Musa alipowaambia Waisraeli wote maneno hayo, watu walianza kuomboleza kwa uchungu mwingi. 40  Hata waliamka asubuhi na mapema na kujaribu kupanda juu mlimani, wakisema: “Tuko tayari kupanda mpaka mahali ambapo Yehova alituambia, kwa maana tumetenda dhambi.”+ 41  Lakini Musa akawaambia: “Kwa nini mnakiuka agizo la Yehova? Hamtafanikiwa. 42  Msipande kwenda huko, kwa sababu Yehova hayuko pamoja nanyi; mtashindwa na maadui wenu.+ 43  Kwa maana Waamaleki na Wakanaani watakabiliana nanyi huko,+ nao watawaangamiza kwa upanga. Kwa sababu mliacha kumfuata Yehova, Yehova hatakuwa pamoja nanyi.”+ 44  Hata hivyo, kwa kimbelembele wakapanda kuelekea mlimani,+ lakini sanduku la agano la Yehova lilibaki katikati ya kambi, na Musa pia alibaki.+ 45  Ndipo Waamaleki na Wakanaani walioishi kwenye mlima huo wakashuka na kuanza kuwashambulia, wakawatawanya mpaka Horma.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “wao ni mkate kwetu.”
Au “tauni.”
Au “fadhili nyingi zenye upendo.”
Tnn., “ya ukahaba.”
Au “ya kuwa maadui wangu.”