Hesabu 23:1-30
23 Kisha Balaamu akamwambia Balaki: “Jenga madhabahu saba mahali hapa,+ nawe unitayarishie ng’ombe dume saba na kondoo dume saba.”
2 Mara moja Balaki akafanya kama Balaamu alivyomwambia. Kisha Balaki na Balaamu wakatoa dhabihu ya ng’ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.+
3 Halafu Balaamu akamwambia Balaki: “Kaa hapa karibu na dhabihu yako ya kuteketezwa, nami nitaenda. Labda Yehova atawasiliana nami. Jambo lolote atakalonifunulia, nitakwambia.” Basi akaenda juu ya kilima kilicho wazi.
4 Ndipo Mungu akawasiliana na Balaamu,+ Balaamu akamwambia: “Nilijenga safu za madhabahu saba na kutoa dhabihu ya ng’ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.”
5 Yehova akatia maneno haya katika kinywa cha Balaamu:+ “Rudi kwa Balaki, na hili ndilo utakalosema.”
6 Basi akarudi na kumkuta Balaki na wakuu wote wa Moabu wakiwa wamesimama karibu na dhabihu yake ya kuteketezwa.
7 Kisha akasema maneno haya ya kishairi:+
“Balaki mfalme wa Moabu amenileta kutoka Aramu,+Kutoka katika milima ya mashariki:
‘Njoo umlaani Yakobo kwa niaba yangu.
Naam, njoo uwashutumu Waisraeli.’+
8 Ninawezaje kuwalaani watu ambao Mungu hajawalaani?
Ninawezaje kuwashutumu wale ambao Yehova hajawashutumu?+
9 Kutoka juu ya miamba ninawaona,Na kutoka vilimani ninawatazama.
Wanaishi peke yao kama taifa;+Hawajioni kuwa sawa na mataifa mengine.+
10 Ni nani anayeweza kuhesabu chembe za mavumbi ya Yakobo+Au hata kuhesabu robo ya Waisraeli?
Acha nife kifo cha watu wanyoofu,Na mwisho wangu uwe kama wao.”
11 Ndipo Balaki akamwambia Balaamu: “Kwa nini umenitendea hivi? Nilikuleta ili uwalaani maadui wangu, lakini badala yake umewabariki tu.”+
12 Balaamu akasema: “Je, sipaswi kusema neno lolote ambalo Yehova anatia kinywani mwangu?”+
13 Balaki akamwambia: “Tafadhali, twende mahali pengine ambapo unaweza kuwaona. Utaona baadhi yao; hutawaona wote. Ukiwa huko walaani kwa niaba yangu.”+
14 Kwa hiyo akampeleka kwenye uwanja wa Sofimu, juu ya Pisga,+ naye akajenga madhabahu saba na kutoa dhabihu ya ng’ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.+
15 Kisha Balaamu akamwambia Balaki: “Kaa hapa karibu na dhabihu yako ya kuteketezwa ninapoenda pale kuwasiliana Naye.”
16 Basi Yehova akawasiliana na Balaamu na kutia neno hili kinywani mwake:+ “Rudi kwa Balaki, na hili ndilo utakalosema.”
17 Basi akarudi na kumkuta Balaki akisubiri karibu na dhabihu yake ya kuteketezwa, na wakuu wa Moabu walikuwa pamoja naye. Balaki akamuuliza: “Yehova amesema nini?”
18 Kisha Balaamu akasema maneno haya ya kishairi:+
“Inuka, Balaki, usikilize.
Nisikilize, ewe mwana wa Sipori.
19 Mungu si mwanadamu anayesema uwongo,+Wala si binadamu anayebadili nia yake.*+
Akisema jambo, je, hatalitenda?
Akinena jambo, je, hatalitimiza?+
20 Tazama! Nimeletwa ili nibariki;Sasa Yeye amebariki,+ nami siwezi kubadili.+
21 Havumilii nguvu zozote za uchawi dhidi ya Yakobo,Wala haruhusu taabu yoyote impate Israeli.
Yehova Mungu wake yuko pamoja nao,+Nao humsifu kwa sauti kubwa kuwa mfalme wao.
22 Mungu anawatoa Misri.+
Yeye ni kama pembe za fahali mwitu.+
23 Kwa maana hakuna ishara za msiba dhidi ya Yakobo,+Wala hakuna uaguzi* wowote dhidi ya Israeli.+
Sasa inaweza kusemwa hivi kumhusu Yakobo na Israeli:
‘Tazameni mambo ambayo Mungu ametenda!’
24 Watu hawa watainuka kama simba,Na kama simba, watajiinua.+
Hawatalala chini mpaka wale mawindoNa kunywa damu ya waliouawa.”
25 Ndipo Balaki akamwambia Balaamu: “Ikiwa huwezi kamwe kuwalaani, basi usiwabariki pia.”
26 Balaamu akamwambia Balaki: “Je, sikukwambia, ‘Nitafanya mambo yote ambayo Yehova anasema’?”+
27 Ndipo Balaki akamwambia Balaamu: “Tafadhali njoo nikupeleke mahali pengine. Labda Mungu wa kweli atakubali uwalaani kwa niaba yangu kutoka mahali hapo.”+
28 Basi Balaki akampeleka Balaamu juu ya Mlima Peori, unaoelekeana na Yeshimoni.*+
29 Kisha Balaamu akamwambia Balaki: “Jenga madhabahu saba mahali hapa, nawe unitayarishie ng’ombe dume saba na kondoo dume saba.”+
30 Kwa hiyo Balaki akafanya kama Balaamu alivyomwambia, naye akatoa dhabihu ya ng’ombe dume mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.

