Hesabu 10:1-36
10 Kisha Yehova akamwambia Musa:
2 “Jitengenezee tarumbeta mbili+ za fedha; zitengeneze kwa kutumia nyundo, nawe uzitumie kuwakusanya watu na kuvunja kambi.
3 Tarumbeta zote mbili zikipigwa, ni lazima Waisraeli wote wakusanyike mbele yako kwenye mlango wa hema la mkutano.+
4 Tarumbeta moja tu ikipigwa, ni wakuu peke yao watakaokusanyika mbele yako, yaani, viongozi wa maelfu katika Israeli.+
5 “Mkipiga tarumbeta kwa mlio unaobadilika-badilika, wale wanaopiga kambi upande wa mashariki+ wanapaswa kuanza safari.
6 Mkipiga tarumbeta mara ya pili kwa mlio unaobadilika-badilika, wale wanaopiga kambi upande wa kusini+ wanapaswa kuanza safari. Tarumbeta inapaswa kupigwa kwa njia hiyo kila mara kambi moja inapoanza safari.
7 “Mnapowakusanya watu wote, mnapaswa kuzipiga tarumbeta+ kwa mlio usiobadilika-badilika.
8 Wana wa Haruni, makuhani, wanapaswa kuzipiga tarumbeta;+ na hiyo itakuwa sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote.
9 “Ikiwa maadui wanaowakandamiza watawashambulia katika nchi yenu, mnapaswa kupiga mwito wa vita kwa tarumbeta hizo,+ na Yehova Mungu wenu atawakumbuka na kuwaokoa kutoka kwa maadui wenu.
10 “Pia, katika siku zenu za kushangilia+—wakati wa sherehe zenu+ na mwanzoni mwa miezi yenu—mtazipiga tarumbeta hizo mnapotoa* dhabihu zenu za kuteketezwa+ na dhabihu zenu za ushirika;+ zitanifanya mimi Mungu wenu niwakumbuke. Mimi ni Yehova Mungu wenu.”+
11 Basi katika mwaka wa pili, mwezi wa pili, siku ya 20 ya mwezi huo,+ lile wingu liliinuka kutoka juu ya hema+ la Ushahidi.
12 Kwa hiyo Waisraeli wakaanza kuondoka katika nyika ya Sinai kulingana na utaratibu uliowekwa wa kuondoka,+ na wingu hilo likasimama katika nyika ya Parani.+
13 Hiyo ilikuwa mara ya kwanza kwao kuondoka kama Yehova alivyokuwa amewaagiza kupitia Musa.+
14 Kwa hiyo kundi la makabila matatu katika kambi ya wana wa Yuda liliondoka kwanza kulingana na vikosi vyake,* na kiongozi wa kundi hilo alikuwa Nashoni+ mwana wa Aminadabu.
15 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Isakari alikuwa Nethaneli+ mwana wa Zuari.
16 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Zabuloni alikuwa Eliabu+ mwana wa Heloni.
17 Hema la ibada lilipofunguliwa,+ wana wa Gershoni+ na wana wa Merari,+ waliobeba hema hilo, walianza safari.
18 Kisha kundi la makabila matatu katika kambi ya Rubeni liliondoka kulingana na vikosi vyake,* na kiongozi wa kundi hilo alikuwa Elisuri+ mwana wa Shedeuri.
19 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Simeoni alikuwa Shelumieli+ mwana wa Zurishadai.
20 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Gadi alikuwa Eliasafu+ mwana wa Deueli.
21 Kisha Wakohathi, waliobeba vyombo vya mahali patakatifu,+ wakaondoka. Hema la ibada lilipaswa kusimamishwa kabla hawajafika.
22 Kisha kundi la makabila matatu katika kambi ya wana wa Efraimu liliondoka kulingana na vikosi vyake,* na kiongozi wa kundi hilo alikuwa Elishama+ mwana wa Amihudi.
23 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Manase alikuwa Gamalieli+ mwana wa Pedazuri.
24 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Benjamini alikuwa Abidani+ mwana wa Gidioni.
25 Kisha kundi la makabila matatu katika kambi ya wana wa Dani liliondoka kulingana na vikosi vyake,* nao walikuwa kikosi cha nyuma cha kulinda kambi zote, na kiongozi wa kundi hilo alikuwa Ahiezeri+ mwana wa Amishadai.
26 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Asheri alikuwa Pagieli+ mwana wa Okrani.
27 Kiongozi wa kikosi cha kabila la wana wa Naftali alikuwa Ahira+ mwana wa Enani.
28 Huo ndio utaratibu ambao Waisraeli na vikosi vyao walifuata* kila mara walipoanza safari.+
29 Kisha Musa akamwambia Hobabu mwana wa Reueli,*+ Mmidiani, baba mkwe wake: “Tunaenda mahali ambapo Yehova alisema, ‘Nitawapa ninyi mahali hapo.’+ Basi twende pamoja,+ nasi tutakutendea mema, kwa sababu Yehova ameahidi kuwapa Waisraeli mambo mema.”+
30 Lakini akamwambia: “Sitaenda. Nitarudi katika nchi yangu na kwa watu wangu wa ukoo.”
31 Musa akamwambia: “Tafadhali usituache, kwa maana unajua mahali tunapopaswa kupiga kambi nyikani, nawe unaweza kutuonyesha njia.*
32 Ukienda pamoja nasi,+ jambo lolote jema ambalo Yehova atatutendea, bila shaka tutakutendea wewe pia.”
33 Basi wakasafiri kwa siku tatu kutoka kwenye mlima wa Yehova,+ na sanduku+ la agano la Yehova lilisafirishwa mbele yao kwa siku hizo tatu ili kuwatafutia mahali pa kupumzika.+
34 Nalo wingu la Yehova+ lilikuwa juu yao wakati wa mchana walipoondoka mahali walipokuwa wamepiga kambi.
35 Kila mara Sanduku hilo lilipoanza kusafirishwa, Musa alisema: “Inuka, Ee Yehova,+ acha maadui wako watawanyike, na wale wanaokuchukia wakimbie kutoka mbele zako.”
36 Na lilipowekwa chini, alisema: “Rudi, Ee Yehova, kwa maelfu yasiyohesabika* ya Waisraeli.”+
Maelezo ya Chini
^ Tnn., “juu ya.”
^ Tnn., “majeshi yake.”
^ Tnn., “majeshi yake.”
^ Tnn., “majeshi yake.”
^ Tnn., “majeshi yake.”
^ Tnn., “majeshi yao yalifuata.”
^ Yaani, Yethro.
^ Tnn., “kuwa macho yetu.”
^ Au “makumi ya maelfu kwa maelfu.”