Hesabu 30:1-16

  • Nadhiri za wanaume (1, 2)

  • Nadhiri za wanawake na mabinti (3-16)

30  Kisha Musa akawaambia hivi viongozi+ wa makabila ya Israeli: “Yehova ameamuru hivi:  Mwanamume akimwekea Yehova nadhiri+ au akiapa+ kuweka nadhiri ya kujinyima kitu fulani,* hapaswi kuvunja ahadi yake.+ Anapaswa kufanya kila jambo aliloapa kufanya.+  “Na binti anayeishi katika nyumba ya baba yake akimwekea Yehova nadhiri au akiweka nadhiri ya kujinyima kitu fulani  na baba yake akisikia nadhiri yake au nadhiri aliyoweka ya kujinyima lakini asimpinge, basi ni lazima atimize nadhiri zake zote, kutia ndani kila nadhiri aliyoweka ya kujinyima kitu fulani.  Lakini baba yake akimkataza baada ya kusikia kwamba binti yake ameweka nadhiri au nadhiri za kujinyima kitu fulani, basi hatatimiza nadhiri hizo. Yehova atamsamehe kwa sababu baba yake alimkataza.+  “Hata hivyo, binti huyo akiolewa baada ya kuweka nadhiri au kuahidi kujinyima kitu fulani bila kufikiri  na mume wake akisikia nadhiri yake lakini asimpinge siku anayosikia kuhusu nadhiri hiyo, basi ni lazima binti huyo atimize nadhiri zake au nadhiri alizoweka za kujinyima kitu fulani.  Lakini mume wake akimkataza siku anayosikia kuhusu nadhiri hiyo, mume huyo anaweza kufuta nadhiri hiyo au ahadi ambayo mke wake aliweka bila kufikiri,+ na Yehova atamsamehe mke huyo.  “Lakini mjane au mwanamke aliyetalikiwa akiweka nadhiri, atatimiza kila jambo ambalo aliahidi. 10  “Hata hivyo, ikiwa mwanamke aliweka nadhiri au nadhiri ya kujinyima kitu fulani akiwa katika nyumba ya mume wake 11  na mume wake alisikia nadhiri yake lakini hakumpinga wala kumkataza, basi ni lazima atimize nadhiri zake au nadhiri yoyote aliyoweka ya kujinyima kitu fulani. 12  Lakini ikiwa mume wake alifuta kabisa nadhiri zozote au nadhiri yoyote ya kujinyima ya mke wake siku aliposikia kuzihusu, mke wake hatatimiza nadhiri hizo.+ Mume wake alizifuta, na Yehova atamsamehe mke huyo. 13  Mume wake anapaswa kukubali au kufuta kiapo chochote au nadhiri yoyote ya kujinyima kitu fulani. 14  Lakini ikiwa mume wake hampingi siku baada ya siku, basi amekubali viapo vyote au nadhiri zote za kujinyima za mke wake. Anakubaliana nazo kwa sababu hakumpinga siku alipomsikia akiweka nadhiri hizo. 15  Lakini mume wake akizifuta baadaye, baada ya siku aliyozisikia, atakuwa na hatia kwa kosa la mke wake.+ 16  “Hizo ndizo sheria ambazo* Yehova alimwamuru Musa kuhusu mume na mke wake, na kuhusu baba na binti yake anayeishi nyumbani kwa baba yake.”

Maelezo ya Chini

Au “akijifunga wajibu.”
Au “Hayo ndiyo masharti ambayo.”