Hesabu 28:1-31

  • Taratibu za kutoa dhabihu mbalimbali (1-31)

    • Dhabihu ya kila siku (1-8)

    • Kwa ajili ya Sabato (9, 10)

    • Dhabihu ya kila mwezi (11-15)

    • Kwa ajili ya Pasaka (16-25)

    • Kwa ajili ya Sherehe ya Majuma (26-31)

28  Kisha Yehova akamwambia Musa,  “Waamuru hivi Waisraeli: ‘Hakikisheni kwamba mnanitolea toleo langu, chakula changu.* Ni lazima mnitolee kwa wakati uliowekwa dhabihu zangu zinazoteketezwa zenye harufu inayonipendeza.’*+  “Nawe uwaambie, ‘Hii ndiyo dhabihu inayochomwa kwa moto ambayo mtamtolea Yehova: mtatoa kwa ukawaida kila siku wanakondoo dume wawili wasio na kasoro wenye umri wa mwaka mmoja kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa.+  Mtamtoa mwanakondoo dume mmoja asubuhi, na mwanakondoo dume wa pili mtamtoa jioni kabla ya giza kuingia,*+  pamoja na toleo la nafaka la sehemu ya kumi ya kipimo cha efa moja* ya unga laini uliochanganywa na robo ya hini* ya mafuta ya zeituni zilizopondwa.+  Ni dhabihu ya kuteketezwa inayotolewa kwa ukawaida,+ iliyoanzishwa kwenye Mlima Sinai, dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova,  pamoja na toleo lake la kinywaji la robo ya hini kwa ajili ya kila mwanakondoo dume.+ Mimineni kileo mahali patakatifu kikiwa toleo la kinywaji mbele za Yehova.  Nanyi mtamtoa mwanakondoo dume wa pili jioni kabla ya giza kuingia.* Mtamtoa pamoja na toleo la nafaka kama lile lililotolewa asubuhi pamoja na toleo lake la kinywaji. Mtamtoa akiwa dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+  “‘Hata hivyo, siku ya Sabato,+ mnapaswa kutoa wanakondoo dume wawili wasio na kasoro wenye umri wa mwaka mmoja pamoja na toleo la nafaka la sehemu mbili za kumi za kipimo cha efa ya unga laini uliochanganywa na mafuta, pamoja na toleo lake la kinywaji. 10  Hiyo ndiyo dhabihu ya kuteketezwa ya Sabato, pamoja na dhabihu ya kuteketezwa inayotolewa kwa ukawaida pamoja na toleo lake la kinywaji.+ 11  “‘Mwanzoni mwa kila mwezi* mtamtolea Yehova dhabihu ya kuteketezwa ya ng’ombe dume wawili wachanga, kondoo dume mmoja, wanakondoo dume saba wasio na kasoro wote wa umri wa mwaka mmoja,+ 12  na toleo la nafaka la sehemu tatu za kumi za vipimo vya unga laini uliochanganywa na mafuta+ kwa ajili ya kila ng’ombe dume na toleo la nafaka la sehemu mbili za kumi za vipimo vya unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya kondoo dume mmoja,+ 13  na toleo la nafaka la sehemu moja ya kumi ya kipimo cha unga laini uliochanganywa na mafuta kwa ajili ya kila mwanakondoo dume; mtavitoa vitu hivyo vikiwa dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza*+ Yehova. 14  Na matoleo ya kinywaji ya dhabihu hiyo yanapaswa kuwa nusu ya hini ya divai kwa ajili ya ng’ombe dume+ na sehemu ya tatu ya hini kwa ajili ya kondoo dume+ na robo ya hini kwa ajili ya mwanakondoo dume.+ Hiyo ndiyo dhabihu ya kuteketezwa inayopaswa kutolewa kila mwezi kwa mwaka mzima. 15  Pia, mwanambuzi mmoja anapaswa kutolewa kwa Yehova ili kuwa dhabihu ya dhambi; atatolewa na dhabihu ya kuteketezwa inayotolewa kwa ukawaida pamoja na toleo lake la kinywaji. 16  “Siku ya 14 ya mwezi wa kwanza, itakuwa Pasaka ya Yehova.+ 17  Na siku ya 15 ya mwezi huo, kutakuwa na sherehe. Mikate isiyo na chachu italiwa kwa siku saba.+ 18  Katika siku ya kwanza kutakuwa na kusanyiko takatifu. Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu. 19  Nanyi mtamtolea Yehova dhabihu ya kuteketezwa inayochomwa kwa moto ya ng’ombe dume wawili wachanga, kondoo dume mmoja, na wanakondoo dume saba wote wa umri wa mwaka mmoja. Mnapaswa kutoa wanyama wasio na kasoro.+ 20  Mnapaswa kuwatoa pamoja na matoleo ya nafaka ya unga laini uliochanganywa na mafuta;+ sehemu tatu za kumi kwa ajili ya ng’ombe dume na sehemu mbili za kumi kwa ajili ya kondoo dume mmoja. 21  Mtatoa sehemu moja ya kumi kwa ajili ya kila mwanakondoo dume kati ya wale wanakondoo dume saba, 22  na pia mbuzi mmoja ili kuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya kufunika dhambi zenu. 23  Mtatoa vitu hivyo pamoja na dhabihu ya kuteketezwa inayotolewa asubuhi kwa ukawaida. 24  Mtatoa vitu hivyo kama chakula* kwa njia ileile kila siku kwa siku saba, ni dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova. Inapaswa kutolewa na dhabihu ya kuteketezwa inayotolewa kwa ukawaida pamoja na toleo lake la kinywaji. 25  Siku ya saba mtakuwa na kusanyiko takatifu.+ Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu.+ 26  “‘Siku ya mavuno ya kwanza yaliyokomaa,+ mnapomtolea Yehova nafaka iliyotoka kuvunwa+ katika sherehe yenu ya majuma,+ mnapaswa kuwa na kusanyiko takatifu. Hampaswi kufanya kazi yoyote ngumu.+ 27  Mtatoa ng’ombe dume wawili wachanga, kondoo dume mmoja, na wanakondoo dume saba wote wa umri wa mwaka mmoja kuwa dhabihu ya kuteketezwa yenye harufu inayompendeza* Yehova,+ 28  pamoja na toleo la nafaka la unga laini uliochanganywa na mafuta; sehemu tatu za kumi kwa ajili ya kila ng’ombe dume, na sehemu mbili za kumi kwa ajili ya kondoo dume mmoja, 29  sehemu moja ya kumi kwa ajili ya kila mwanakondoo dume kati ya wale wanakondoo dume saba, 30  na pia mwanambuzi mmoja kwa ajili ya kufunika dhambi zenu.+ 31  Mtatoa vitu hivyo pamoja na dhabihu ya kuteketezwa inayotolewa kwa ukawaida pamoja na toleo lake la nafaka. Mtatoa wanyama wasio na kasoro,+ pamoja na matoleo yao ya kinywaji.

Maelezo ya Chini

Au “inayonituliza.”
Au “mkate wangu.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Hini ilikuwa sawa na lita 3.67. Angalia Nyongeza B14.
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “katikati ya zile jioni mbili.”
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “miezi yenu.”
Au “inayomtuliza.”
Au “inayomtuliza.”
Tnn., “mkate.”
Au “inayomtuliza.”