Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nitahitaji Kufanya Nini Baada ya Ubatizo?​—Sehemu ya 1: Dumisha Utendaji Wako wa Kiroho

Nitahitaji Kufanya Nini Baada ya Ubatizo?​—Sehemu ya 1: Dumisha Utendaji Wako wa Kiroho

 Mali zenye thamani, kama vile nyumba au gari, zinahitaji kudumishwa vizuri. Vivyo hivyo, unahitaji kudumisha urafiki wako na Mungu. Utadumishaje urafiki huo baada ya kubatizwa?

Katika makala hii

 Endelea kujifunza Neno la Mungu

 Andiko la msingi: “[Endelea] kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.”​—Wakolosai 1:10.

 Maana yake: Baada ya kubatizwa, utahitaji kuendelea kusoma Biblia na kutafakari mambo unayojifunza.​—Zaburi 25:4; 119:97.

 Mambo ya kutarajia: Huenda nyakati fulani utahisi kwamba hutaki kujifunza. Huenda ukajiambia kwamba wewe si mwanafunzi mzuri.

 Mambo unayoweza kufanya: Chimba zaidi ndani ya habari za Biblia zinazokupendeza. Panga ratiba yako mwenyewe ya kujifunza ambayo haitakulemea. Lengo lako ni kuongeza upendo wako kwa Yehova na Neno lake. Utanufaika na kufurahia mambo hayo unayojifunza.​—Zaburi 16:11.

 Dokezo: Ili kunufaika kikamili kutokana na funzo lako, tafuta mahali penye utulivu ambapo hutakengeushwa na mambo mengine.

 Je, unahitaji msaada zaidi?

 Endelea kusali kwa Yehova

 Andiko la msingi: “Msihangaike kuhusiana na jambo lolote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani, mjulisheni Mungu maombi yenu.”​—Wafilipi 4:6.

 Maana yake: Kuwasiliana na Mungu kunamaanisha wewe unamsikiliza unaposoma Neno lake, kisha unazungumza naye unaposali. Tambua kwamba sala zako zinaweza kutia ndani kuomba mahitaji yako na kutoa shukrani kwa baraka ambazo umepokea.

 Mambo ya kutarajia: Huenda sala zako zikaanza kuwa za kujirudia-rudia. Huenda hata ukaanza kuwa na shaka ikiwa kweli Yehova anasikiliza au ikiwa anataka uzungumze naye.​—Zaburi 10:1.

 Mambo unayoweza kufanya: Unapoendelea na shughuli zako za kila siku, fikiria kuhusu mambo unayoweza kusali kuyahusu. Ikiwa hali zako hazikuruhusu kutoa sala ndefu wakati huo, weka jambo hilo akilini na usali kulihusu baadaye. Mbali na mahangaiko yako, fikiria mahitaji ya wengine.​—Wafilipi 2:4.

 Dokezo: Sala zako zikianza kuwa za kujirudia-rudia, sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Anataka kusikia kuhusu mahangaiko yako yote, kutia ndani mahangaiko kuhusu sala zako.​—1 Yohana 5:14.

 Je, unahitaji msaada zaidi?

 Endelea kuwaeleza wengine mambo unayoamini

 Andiko la msingi: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. . . . Ukifanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.”​—1 Timotheo 4:16.

 Maana yake: Unapowaeleza wengine mambo unayoamini, unaimarisha imani yako pia. Hivyo, huenda utaokoa uhai wa wanaokusikiliza na uhai wako pia.

 Mambo ya kutarajia: Nyakati fulani huenda utahisi hutaki kuwaeleza wengine mambo unayoamini. Huenda hata ukaogopa kufanya hivyo, hasa shuleni.

 Mambo unayoweza kufanya: Azimia kutoruhusu hisia zisizofaa, kama vile woga, ziongoze maamuzi yako. Mtume Paulo aliandika hivi: “Hata [nikitangaza habari njema] bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.”​—1 Wakorintho 9:16, 17.

 Dokezo: Omba wazazi wako ruhusa ili usaidiwe na mtu mwingine. Anapaswa kuwa mwabudu mwenzako ambaye ni mfano mzuri katika huduma.​—Methali 27:17.

 Je, unahitaji msaada zaidi?

 Endelea kuhudhuria mikutano ya Kikristo

 Andiko la msingi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja.”​—Waebrania 10:24, 25.

 Maana yake: Sababu kuu ya kuhudhuria mikutano ni kumwabudu Yehova. Lakini kuna faida nyingine mbili za kuhudhuria mikutano. Kwanza, wewe utatiwa moyo na waabudu wenzako. Pili, unawatia moyo wengine unapohudhuria na kushiriki.​—Waroma 1:11, 12.

 Mambo ya kutarajia: Huenda pindi fulani akili yako ikatangatanga mkutano unapoendelea na hivyo ukakosa mambo muhimu yanayofundishwa. Au huenda ukaacha kuhudhuria mikutano kwa ukawaida au ukaruhusu mambo mengine, kama vile kazi za shule, zikuzuie.

 Mambo unayoweza kufanya: Bila kupuuza kazi za shule, azimia kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na ulifanye liwe lengo lako kujifunza mengi kadiri uwezavyo. Jihusishe kwa kunyoosha mkono kutoa maelezo. Baada ya mikutano, mpongeze angalau mtu mmoja kwa sehemu yake au maelezo aliyotoa.

 Dokezo: Jitayarishe mapema. Pakua programu ya JW Library® na utumie tabo ya “Mikutano” kuona mambo yatakayozungumziwa kwenye kila mkutano.

 Je, unahitaji msaada zaidi?