Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?

Uumbaji au Mageuzi?​—Sehemu ya 1: Kwa Nini Nimwamini Mungu?

 Uumbaji au mageuzi?

 Je, unaamini kwamba Mungu aliumba kila kitu? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayeamini hivyo; vijana wengi (na watu wazima) wanaamini jambo hilo. Lakini wengine husema kwamba uhai na ulimwengu wote ulijitokeza wenyewe​—bila msaada wa “Mtu Mkuu Kuliko Wote.”

 Je, ulijua? Mara nyingi watu wanaoamini uumbaji na wale wanaoamini mageuzi wote husema tu kile wanachoamini bila kujua kwa nini wanaamini jambo hilo.

  •   Watu fulani huamini uumbaji kwa sababu hivyo ndivyo wamefundishwa kanisani.

  •   Watu wengi huamini mageuzi kwa sababu hivyo ndivyo wamefundishwa shuleni.

 Mfululizo wa makala hizi utakusaidia kuimarisha msimamo wako na kuwaeleza wengine kile unachoamini kuhusu uumbaji. Hata hivyo, kwanza, unahitaji kujiuliza swali hili la msingi:

 Kwa nini ninamwamini Mungu?

 Kwa nini swali hilo ni muhimu? Kwa sababu Biblia inakutia moyo utumie ‘nguvu zako za kufikiri.’ (Waroma 12:1) Hilo linamaanisha kwamba imani yako kumwelekea Mungu haipaswi kutegemea tu

  •  hisia (Nahisi kwamba kuna mtawala mwenye mamlaka kuu)

  •  maoni ya wengine (Ninaishi katika jamii inayopenda mambo ya dini)

  •  kusukumwa (Wazazi wangu walinifundisha kumwamini Mungu​—siwezi kuwapinga)

 Badala yake, wewe mwenyewe unapaswa kusadiki kabisa kwamba Mungu yuko ukiwa na sababu za msingi za kukufanya uamini jambo hilo.

 Hivyo basi, ni nini kinachokusadikisha kwamba Mungu yuko? Daftari “Kwa Nini Ninamwamini Mungu?” litakusaidia upate usadikisho. Pia, unaweza kufaidika zaidi kwa kujua jinsi ambavyo vijana wengine walijibu swali hilo.

 “Ninapokuwa darasani nikimsikiliza mwalimu akieleza jinsi miili yetu inavyofanya kazi, ninakuwa na uhakika kuwa Mungu yuko. Kila sehemu ya mwili ina kazi yake, kutia ndani vitu vidogo sana, na mifumo mbalimbali hufanya kazi bila sisi wenyewe kujua. Kwa kweli mwili wa binadamu unastaajabisha sana!”​—Teresa.

 “Ninapoona jengo refu sana, meli, au gari, mimi hujiuliza, ‘Ni nani aliyetengeneza kitu hiki?’ Gari hutengenezwa na watu wenye akili nyingi sana kwa sababu vitu vidogo-vidogo sana lazima vifanye kazi vizuri ili gari liweze kusonga. Ikiwa lazima gari libuniwe na mtu fulani, basi lazima mwanadamu awe alibuniwa na mtu fulani pia.”​—Richard.

 “Unapogundua kuwa wanadamu wenye akili sana walitumia mamia ya miaka kuelewa sehemu ndogo ya ulimwengu, ni jambo lisilopatana na akili kufikiria kuwa ulimwengu mzima ulijitokeza wenyewe bila msaada wa mtu fulani mwenye akili!”​—Karen.

 “Kadiri nilivyojifunza sayansi, ndivyo nilivyoshindwa kuamini mageuzi. Kwa mfano, nimefikiria kuhusu vitu vya asili vilivyotengenezwa kwa hesabu zilizo sahihi na jinsi wanadamu walivyo tofauti sana na viumbe wengine, kutia ndani uhitaji wa kujua sisi ni nani, tumetokea wapi, na tunaelekea wapi. Mageuzi hukusudiwa kuelezea mambo hayo kwa njia inayohusisha wanyama, lakini fundisho hilo halijawahi kueleza kwa nini wanadamu ni tofauti na viumbe vingine vyote. Ninaona mtu anahitaji kuwa na ‘imani’ zaidi kuamini mageuzi kuliko kumwamini Muumba.”​—Anthony.

 Kuelezea msimamo wangu

 Vipi ikiwa wanafunzi wenzako wanakudhihaki kwa sababu unaamini kitu usichoweza kuona? Vipi ikiwa wanasema kuwa sayansi “imethibitisha” mageuzi?

 Kwanza, uwe na uhakika na unachoamini. Usiogope wala usiaibike. (Waroma 1:​16) Zaidi ya yote, kumbuka:

  1.   Hauko peke yako; bado kuna watu wengi wanaomwamini Mungu. Wanatia ndani wataalamu wenye akili nyingi. Kwa mfano, kuna wanasayansi wanaoamini kuna Mungu.

  2.   Watu wanaposema hawamwamini Mungu, wakati mwingine wanachomaanisha hasa ni kuwa hawamwelewi Mungu. Badala ya kutoa uthibitisho wa kuunga mkono maoni yao, wao hutokeza maswali kama vile, “Ikiwa Mungu yupo, kwa nini anaruhusu uovu na kuteseka?” Mwishowe suala hilo linahusisha hisia badala ya kutumia uwezo wa kufikiri.

  3.   Wanadamu wana “uhitaji wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Hilo linatia ndani uhitaji wa kumwamini Mungu. Hivyo ikiwa mtu anasema hakuna Mungu, mtu huyo​—na si wewe​—ndiye anayewajibika kueleza kwa nini amefikia mkataa huo.​—Waroma 1:​18-​20.

  4.   Ni jambo linalopatana na akili kumwamini Mungu. Jambo hilo linapatana na ukweli uliothibitishwa kwamba uhai hauwezi kujitokeza wenyewe. Hakuna uthibitisho unaoweza kuonyesha kwamba uhai ulitokana na kitu kisicho hai.

 Hivyo, unaweza kusema nini ikiwa mtu anatilia shaka imani yako kumwelekea Mungu? Fikiria mambo haya machache.

 Ikiwa mtu anasema: “Watu wasio na elimu tu ndiyo wanaomwamini Mungu.”

 Unaweza kujibu: “Je, kweli unakubaliana na maoni hayo ya watu wengi? Mimi sikubaliani nayo. Kwa kweli, utafiti mmoja uliohusisha maprofesa 1,600 wa sayansi kutoka vyuo vikuu mbalimbali vinavyoheshimika ulionyesha kuwa theluthi moja ya maprofesa hao hawakudai kuwa hawamwamini Mungu au kwamba mambo ya Mungu hayajulikani. a Je, utasema maprofesa hao hawana akili kwa sababu wanamwamini Mungu?”

 Ikiwa mtu anasema: “Ikiwa Mungu yuko, kwa nini kuna mateso mengi ulimwenguni?”

 Unaweza kujibu hivi: “Je, huenda unamaanisha kwamba huelewi jinsi Mungu anavyotenda​—au katika kisa hiki, haonyeshi kuwa atachukua hatua? [Mruhusu ajibu.] Nimepata sababu zenye kuridhisha kuhusu ni kwa nini kuna mateso mengi duniani. Lakini ili kuelewa jambo hilo ni lazima uchunguze mafundisho kadhaa ya Biblia. Je, ungependa kujua zaidi?”

 Makala inayofuata katika mfululizo huu itazungumzia sababu kwa nini fundisho la mageuzi halitoi maelezo yenye kuridhisha kuhusu chanzo chetu.

a Chanzo cha habari: Baraza la Utafiti Kuhusu Sayansi ya Kijamii, “Dini na Hali ya Kiroho Miongoni mwa Wanasayansi wa Vyuo Vikuu,” na Elaine Howard Ecklund , Februari 5, 2007.