Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kutumiaje Vizuri Muda Wangu?

Ninaweza Kutumiaje Vizuri Muda Wangu?

 Kwa nini utumie vizuri muda wako?

  •   Muda ni kama pesa. Ukiutumia vibaya, hutakuwa nao utakapouhitaji. Kwa upande mwingine, ukipangia vizuri muda wako, utakuwa na akiba ya kufanya mambo unayopenda!

     Kanuni ya Biblia: “Kuna vitu anavyotamani sana mtu mvivu, ingawa hana chochote, lakini mwenye bidii atatoshelezwa kikamili.”​—Methali 13:4.

     Jambo kuu ni hili: Kutumia vizuri muda wako kutakupa uhuru mwingi zaidi, si mdogo zaidi.

  •   Kutumia vizuri muda ni ustadi wenye thamani utakaokufaa ukiwa mtu mzima. Hata unaweza kukusaidia kudumisha kazi fulani au kuipoteza. Ikiwa ungekuwa na biashara, ungemruhusu mfanyakazi achelewe kuja kazini kwa ukawaida?

     Kanuni ya Biblia: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo ni mwaminifu katika lililo kubwa pia.”​—Luka 16:10.

     Jambo kuu ni hili: Uwezo wako wa kutumia muda vizuri unaonyesha wewe ni mtu wa aina gani.

 Hata hivyo, si rahisi kutumia muda vizuri. Chunguza changamoto kadhaa.

 Changamoto #1: Marafiki

 “Marafiki wakiniomba twende kwenye tafrija, sikuzote mimi hukubali hata ikiwa sina muda. Mimi hufikiri hivi, ‘Si nitafanya kazi haraka baada ya kurudi.’ Lakini haiwi hivyo, na mambo yameenda mrama kwa sababu hiyo.”​—Cynthia.

 Changamoto #2: Kukengeushwa

 “TV ni kama kifaa kinachotumiwa kufyonza vumbi. Maonyesho na sinema zake zinakunasa na si rahisi kuziacha.”​—Ivy.

 “Ninapoteza saa nyingi sana nikitumia kifaa changu cha kielektroni. Betri inapokwisha ndipo mimi huanza kujihisi vibaya kwamba nimekosa uwezo wa kujidhibiti.”​—Marie.

 Changamoto #3: Kuahirisha

 “Mimi huahirisha kazi za shuleni na kazi nyingine ninazohitaji kufanya. Ninajikuta nikipoteza muda nikifanya mambo yasiyo na maana hadi ninapolazimika kabisa kumaliza kazi zangu. Hiyo siyo njia nzuri ya kufanya mambo.”​—Beth.

Kutumia vizuri muda wako kutakupa uhuru mwingi zaidi, si mdogo zaidi

 Unachoweza kufanya

  1.   Orodhesha kazi unazopaswa kufanya. Kwa mfano, kazi za nyumbani na za shuleni. Andika muda unaohitaji kumaliza kila kazi katika juma moja.

     Kanuni ya Biblia: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”​—Wafilipi 1:​10.

  2.   Orodhesha mambo ambayo ungependa kufanya wakati wa ziada. Mambo hayo yanaweza kutia ndani kutumia mitandao ya kijamii na kutazama TV. Andika tena saa unazopanga kutumia katika kila jambo katika juma moja.

     Kanuni ya Biblia: “Endeleeni kutembea kwa hekima . . . , mkitumia vizuri kabisa wakati wenu.”​—Wakolosai 4:5.

  3.   Panga ratiba. Angalia orodha mbili ulizoandika. Je, umeacha muda wa kutosha kwa ajili ya kazi muhimu? Je, unahitaji kununua wakati kutoka kwa muda wako wa burudani?

     Dokezo: Andika orodha ya mambo ya kufanya kila siku na utie alama kila kazi unayomaliza.

     Kanuni ya Biblia: “Mipango ya wenye bidii hakika huleta mafanikio.”​—Methali 21:5.

  4.   Shikamana na ratiba. Ni kweli kwamba huenda ukahitaji kukataa mialiko mara kwa mara ili umalize kazi muhimu. Hata hivyo, kwa ujumla utakuta kwamba utakuwa na muda mwingi zaidi​—na utaufurahia zaidi.

     Kanuni ya Biblia: “Iweni wenye bidii, msiwe wavivu katika kazi zenu.”​—Waroma 12:11, maelezo ya chini.

  5.   Jithawabishe​—lakini kwa kiasi. Kijana anayeitwa Tara anasema hivi: “Pindi fulani ningekamilisha mambo mawili kwenye orodha yangu, kisha nijiambie ‘Sasa naweza kutazama TV kwa dakika 15, halafu nitaendelea na kazi.’ Dakika 15 zinageuka kuwa 30, na 30 kuwa saa nzima, na muda si muda najikuta nimepoteza saa mbili nikitazama TV!”

     Suluhisho ni nini? Ona burudani kuwa thawabu ya kukamilisha kazi​—si sehemu ya siku yako.

     Kanuni ya Biblia: “Hakuna jambo bora analoweza kufanya mtu kuliko . . . kufurahia kazi yake ngumu.”​—Mhubiri 2:​24.