Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

Je, Niko Tayari Kuondoka Nyumbani?

 Wazo la kuondoka nyumbani linaweza kusisimua na wakati huohuo kuogopesha. Unaweza kutambuaje ikiwa uko tayari kujitegemea?

 Chunguza sababu zako

 Kuna sababu nyingi zinazoweza kufanya uamue kuondoka nyumbani lakini baadhi ya sababu hizo si za hekima. Kwa mfano, mvulana anayeitwa Mario alisema hivi: “Nilitaka kuondoka nyumbani ili niepuke majukumu niliyokuwa nayo.”

 Ukweli ni kwamba huenda uhuru wako ukapungua unapoondoka nyumbani. Kijana mwenye umri wa miaka 18 anayeitwa Onya alisema hivi: “Unapoondoka nyumbani, utahitaji kutunza mahali unapoishi, kujitayarishia chakula, kulipia gharama zako​—na wazazi hawatakuwa karibu ili kukusaidia!”

 Jambo kuu: Unahitaji kujua kwa nini unataka kuondoka nyumbani ili utambue ikiwa uko tayari kuondoka.

 Hesabu gharama

 Yesu alisema hivi: “Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?” (Luka 14:28) Unaweza “kuhesabu gharama” jinsi gani kabla ya kuondoka nyumbani? Jichunguze katika mambo yafuatayo.

  UNATUMIAJE PESA?

 Biblia inasema: ‘Pesa ni ulinzi.’​—Mhubiri 7:​12.

  •  Je, ni vigumu kwako kuhifadhi pesa?

  •  Je, unatumia pesa bila kupanga?

  •  Je, kila mara unakopa pesa kutoka kwa watu wengine?

 Ikiwa umejibu ndiyo kwa mojawapo ya maswali hayo, basi kuondoka nyumbani kunaweza kuwa na matokeo mabaya kuliko ulivyotarajia!

 “Kaka yangu aliondoka nyumbani akiwa na umri wa miaka 19. Kwa muda wa mwaka mmoja, alikuwa ametumia pesa zake zote za akiba, akashindwa kulipa mkopo wa gari kwa hiyo likachukuliwa, benki zikakataa kumkopesha pesa, kwa hiyo akaanza kuomba wazazi wamruhusu kurudi nyumbani.”​—Danielle.

 Unachoweza kufanya sasa: Waulize wazazi wako kuhusu gharama halisi za mwezi mzima. Wanalipia nini, na wanatayarishaje bajeti yao ili waweze kulipia gharama zote? Na wanahifadhi pesa jinsi gani?

 Jambo kuu: Kujifunza jinsi ya kutumia pesa kwa usawaziko ukiwa bado nyumbani kutakutayarisha kuwa na uwezo wa kukabiliana na hali ngumu ya kiuchumi katika maisha yako utakapojitegemea.

  JE, UNAWAJIBIKA?

 Biblia inasema: “Kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.”​—Wagalatia 6:5.

  •  Je, unaahirisha mambo?

  •  Je, kila wakati wazazi wako wanakukumbusha ufanye kazi zako za nyumbani?

  •  Je, mara nyingi unarudi nyumbani baada ya saa ambazo wazazi wako wamekuruhusu?

 Ikiwa umejibu ndiyo kwa mojawapo ya maswali hayo, inawezekana itakuwa vigumu zaidi kwako kuwajibika unapoishi peke yako.

 “Unapojitegemea, kuna mambo fulani ambayo kwa kawaida hufurahii kuyafanya lakini ambayo ni lazima utenge wakati wa kuyafanya. Hakuna atakayekukumbusha kufanya mambo hayo, utahitaji kujikumbusha na kufuata ratiba kikamili.”​—Jessica.

 Unachoweza kufanya sasa: Kwa mwezi mzima, jaribu kutimiza majukumu mengi ya nyumbani kadiri uwezavyo. Kwa mfano, safisha nyumba nzima, fua nguo zako, nunua chakula, pika chakula cha jioni kila siku, na baada ya kupika, osha vyombo. Hilo litakusaidia kuelewa mambo utakayohitaji kutimiza utakapojitegemea.

 Jambo kuu: Kuwajibika ni muhimu sana ikiwa utahitaji kuishi peke yako.

Kuhama nyumbani bila kujitayarisha ni kama kuruka kutoka katika ndege bila kujifunza kwanza jinsi ya kutumia parachuti

  JE UNAWEZA KUDHIBITI HISIA ZAKO?

 Biblia inasema hivi: “Myaondoe mambo haya yote kutoka kwenu: ghadhabu, hasira, ubaya, matusi, na maneno machafu.”​—Wakolosai 3:8.

  •  Je, vigumu kwako kuishi kwa amani na wengine?

  •  Je, unashindwa kudhibiti hasira?

  •  Je, sikuzote unapenda mambo yafanywe kulingana na njia yako?

 Ikiwa umejibu ndiyo kwa mojawapo ya maswali hayo, huenda ikawa vigumu sana kwako kuishi katika chumba kimoja na mtu mwingine​—huenda ikawa vigumu kuishi na mwenzi wa ndoa.

 “Kuishi na mtu mwingine katika chumba kimoja kulifunua udhaifu wangu. Niligundua kwamba sipaswi kutarajia watu wengine wavumilie matatizo yangu ya kihisia yaliyosababishwa na mkazo. Nilihitaji kutafuta njia inayofaa ya kukabiliana na hisia zangu.”​—Helena.

 Unachoweza kufanya sasa: Jifunze jinsi ya kuwa na uhusiano mzuri na wazazi wako na ndugu zako. Kwa kweli, jinsi unavyoshughulikia hali ya kutokamilika ya wale unaoishi nao sasa, inaweza kuonyesha jinsi utakavyoshughulika na hali ya kutokamilika ya wale utakaoishi nao wakati ujao.

 Jambo kuu: Kuishi peke yako si njia ya kukwepa majukumu yako—ni ustadi unaohitaji matayarisho. Kwa nini usizungumze na wale waliofanikiwa? Waulize ni mambo gani ambayo wangeweza kufanya tofauti na walivyoyafanya au ni mambo gani ambayo wanatamani wangeyajua mapema lakini wameyajua sasa. Utanufaika ukifanya hivyo kuhusiana na uamuzi wowote muhimu unaohitaji kufanya!