VIJANA HUULIZA
Je, Tuvunje Urafiki Wetu? (Sehemu ya 1)
Nyakati nyingine, kuna faida kuvunja uhusiano. Fikiria kisa cha Jill. Anasema, “Mwanzoni nilifurahi kwamba mpenzi wangu alikuwa akitaka kujua niko wapi, ninafanya nini, na niko na nani. Lakini ilifikia hatua ya kwamba singeweza kuwa na mtu mwingine yeyote isipokuwa yeye. Hata aliona wivu nilipokuwa pamoja na watu wa familia yetu—hasa baba yangu. Nilipovunja uhusiano huo, nilihisi ni kana kwamba nimejiondolea mzigo mzito sana!”
Sarah alikuwa katika hali kama hiyo pia. Alianza kutambua kwamba John ni mwenye dhihaka mwenye kudai mno, na asiye na heshima. Sarah anakumbuka hivi: “Siku moja alikuja kwetu akiwa amechelewa kwa saa tatu! Alimpuuza mama yangu aliyemfungulia mlango, kisha akasema: ‘Twende. Tumechelewa.’ Si kwamba yeye amechelewa, bali ‘Tumechelewa.’ Alipaswa kuomba msamaha au kueleza sababu ya kuchelewa. Isitoshe, alipaswa kumwonyesha heshima mama yangu!”
Ni kweli kwamba kisa kimoja chenye kuvunja moyo au tabia fulani isiyopendeza haimaanishi kwamba uhusiano wenu hautadumu. (Zaburi 130:3) Hata hivyo, Sarah alipotambua kwamba John alikuwa na mazoea ya kukosa heshima, aliamua kuuvunja uhusiano wao.
Kama ilivyokuwa katika visa vya Jill na Sarah, ungefanya nini ukitambua kwamba mpenzi wako hastahili kuwa mwenzi wako wa ndoa? Ikiwa ndivyo ilivyo, usipuuze hisia zako! Ijapokuwa ni vigumu kukubali ukweli wa mambo, huenda ikafaa kuvunja uhusiano wenu. Andiko la Methali 22:3 linasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.”
Ni kweli, huenda isiwe rahisi kuvunja uhusiano. Lakini ndoa ni muungano wa kudumu. Afadhali kuumia kwa muda mfupi sasa kuliko kujuta maisha yako yote baadaye!