Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Nikisumbuliwa Kingono?

Nifanye Nini Nikisumbuliwa Kingono?

 Kusumbuliwa kingono kunahusisha nini?

 Kusumbuliwa kingono kunatia ndani kutendewa mambo ya kingono bila idhini​—kutia ndani kumshika-shika mtu au hata kumwambia maneno ya kingono. Lakini nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu kutofautisha kati ya kumtania mtu, kumchezea kimapenzi, na kumsumbua kingono.

 Je, unajua tofauti kati ya mambo hayo matatu? Jibu  maswali kuhusu kusumbuliwa kingono ili ujue tofauti!

 Kwa kusikitisha, kusumbuliwa kingono hakukomi unapomaliza shule. Hata hivyo, ukijua jinsi ya kutenda sasa unaposumbuliwa kingono, utajua jinsi ya kukabiliana nao unapoanza kufanya kazi. Huenda hata ukamzuia yule anayekusumbua asiwaumize wengine!

 Ninapaswa kufanya nini ikiwa ninasumbuliwa kingono?

 Ili kumkomesha mtu anayekusumbua kingono, kwanza ni lazima ujue jambo hilo linahusisha tabia gani zisizofaa. Fikiria visa vitatu vifuatavyo na jinsi unavyoweza kukabiliana na kila moja.

 KISA:

“Nikiwa kazini, wanaume fulani walionizidi umri walikuwa wakiniambia kwamba mimi ni mrembo na kwamba wangetamani sana kupunguza umri wao kwa miaka 30. Pindi fulani, mmoja wao alisimama nyuma yangu na kunusa nywele zangu!’​—Tabitha, mwenye umri wa miaka 20.

 Huenda Tabitha akajiambia: ‘Nikimpuuza na kuvumilia hali hii, huenda akaacha.’

 Kwa nini huenda hilo lisimsaidie: Wataalamu wanasema kwamba mtu akipuuza tendo lolote la kusumbuliwa kingono, mara nyingi hali hiyo huendelea na hata kuwa mbaya zaidi.

 Jaribu kufanya hivi: Mwambie yule anayekusumbua​—kwa utulivu lakini waziwazi​—kwamba hutavumilia usemi wake au tabia yake. Taryn, mwenye umri wa miaka 22 anasema: “Mtu akinishika kwa njia isiyofaa, mimi hugeuka na kumwambia asithubutu kufanya hivyo tena. Hilo humshtua.” Msumbuaji akiendelea na tabia yake, uwe thabiti na usikate tamaa. Ili udumishe viwango vya juu vya maadili, Biblia inashauri, ‘Simama imara, komaa, na uwe thabiti.’​—Wakolosai 4:12, Biblia Habari Njema.

 Vipi ikiwa msumbuaji anatisha kwamba atakudhuru? Basi usimwambie jambo lolote. Ondoka haraka iwezekanavyo, na umwombe msaada mtu mzima anayetegemeka.

 KISA:

“Nilipokuwa na umri wa miaka 11, wasichana wawili walinishika nje ya darasa. Mmoja wao alikuwa shoga, na alitaka niwe rafiki yake. Ingawa nilikataa, waliendelea kunisumbua kila siku wakati wa mapumziko. Pindi moja hata walinisukuma ukutani!”​—Victoria, mwenye umri wa miaka 18.

 Huenda Victoria akajiambia: ‘Nikimwambia mtu yeyote kuhusu jambo hili, nitaonekana kuwa mwoga na huenda hakuna mtu atakayeniamini.’

 Kwa nini huenda hilo lisimsaidie: Usipomwambia mtu jambo hilo, huenda anayekusumbua akaendelea kufanya hivyo na hata kuwasumbua wengine.​—Mhubiri 8:11.

 Jaribu kufanya hivi: Tafuta msaada. Wazazi na walimu wanaweza kukupa msaada unaohitaji ili kumkomesha msumbuaji. Lakini vipi ikiwa watu hawachukui malalamiko yako kwa uzito unapowaambia? Jaribu kufanya hivi: Kila mara unaposumbuliwa, andika kila jambo. Andika tarehe, saa, na mahali uliposumbuliwa, na pia yale ambayo msumbuaji alisema. Kisha mpe mzazi au mwalimu karatasi hiyo. Watu wengi huchukua kwa uzito malalamiko yaliyoandikwa kuliko yaliyosemwa.

 KISA:

“Nilimwogopa sana kijana mmoja aliyekuwa katika timu ya raga. Alikuwa na kimo cha karibu futi 6.5, na uzito wa kilogramu 135 hivi! Alijiambia kwamba lazima atafanya ngono pamoja nami. Alinisumbua karibu kila siku​—kwa kipindi cha mwaka mzima. Siku moja, tulipokuwa mimi na yeye tu darasani, akaanza kunikaribia. Niliruka na kukimbia nje.”​—Julieta, mwenye umri wa miaka 18.

 Huenda Julieta angejiambia: ‘Ni kawaida kwa wavulana kutenda hivyo.’

 Kwa nini huenda hilo lisimsaidie: Yule anayekusumbua hatabadilika ikiwa kila mtu anaona tabia yake kuwa jambo la kawaida.

 Jaribu kufanya hivi: Epuka kupuuza jambo hilo kwa kuliona kuwa mzaha au kwa kutabasamu. Badala yake, mwonyeshe msumbuaji​—kwa maneno na ishara za uso kwamba hutavumilia kamwe tabia hiyo.

 Ningefanya nini?

 SIMULIZI HALISI LA 1:

“Sipendi kuwa mkaidi kwa njia yoyote. Kwa hiyo, vijana waliponisumbua, niliwaambia waache​—lakini sikusema kwa uthabiti, na mara nyingi nilitabasamu nilipowaambia. Walifikiri nilikuwa nikiwachezea kimapenzi.”—Tabitha.

  •   Kama ungekuwa Tabitha, ungewatendeaje wasumbuaji hao? Kwa nini?

  •   Ni mambo gani yanayoweza kumfanya msumbuaji afikiri unamchezea kimapenzi?

 SIMULIZI HALISI LA 2:

“Wavulana fulani walianza tu kwa kuniambia maneno fulani machafu wakati wa somo la mazoezi. Niliwapuuza kwa majuma kadhaa, lakini mambo yalizidi kuwa mabaya. Kisha wavulana hao wakaanza kuketi kando yangu na kuniwekelea mikono begani. Niliwasukuma, lakini hawakuacha tabia hiyo. Mwishowe, mmoja wa wavulana hao alinipa karatasi iliyokuwa na maneno machafu sana. Nilimpa mwalimu wangu karatasi hiyo. Mvulana huyo alifukuzwa kutoka shuleni. Nilitambua kwamba afadhali ningemwambia mwalimu mara tu vijana hao walipoanza kunisumbua!”—Sabina.

  •   Unadhani ni kwa nini Sabina hakumweleza mwalimu wake jambo hilo mapema? Unafikiri huo ulikuwa uamuzi mzuri? Kwa nini unajibu hivyo?

 SIMULIZI HALISI LA 3:

“Mvulana fulani alimfikia Greg, ndugu yangu mdogo, walipokuwa msalani. Mvulana huyo alimkaribia sana Greg na kumwambia, ‘Nibusu.’ Greg alikataa, lakini mvulana huyo hakumwacha. Ilibidi Greg amsukume kando.”—Suzanne.

  •   Unafikiri Greg alikuwa amesumbuliwa kingono? Kwa nini unajibu hivyo?

  •   Unafikiri ni kwa nini wavulana fulani husita kusema wanaposumbuliwa kingono na mvulana mwenzao?

  •   Unadhani Greg alikabiliana na hali hiyo kwa njia inayofaa? Wewe ungefanya nini?