Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kufanya Nini Ili Kupinga Shinikizo la Kufanya Ngono?

Ninaweza Kufanya Nini Ili Kupinga Shinikizo la Kufanya Ngono?

 “Nilipokuwa shuleni, mtu alipodai kwamba alifanya ngono, wengine wote walihisi walihitaji kufanya hivyo pia. Hakuna mtu anayetaka kuachwa nyuma na kuonekana kuwa tofauti.”—Elaine, mwenye umri wa miaka 21.

 Je, umewahi kuhisi kwamba unashinikizwa kufanya ngono—kwa sababu inaonekana kila mtu anafanya hivyo?

 Je, umewahi kushinikizwa kufanya ngono na mtu unayempenda?

 Ikiwa ndivyo, makala hii inaweza kukusaidia kupinga shinikizo hilo—iwe ni kutoka kwa wengine au kutokana na tamaa zako—ili ufanye maamuzi mazuri zaidi.

 Maoni yasiyo sahihi na mambo hakika

 MAONI YASIYO SAHIHI: Kila mtu anafanya ngono (isipokuwa mimi).

 JAMBO HAKIKA: Katika uchunguzi mmoja, vijana wawili kati ya watatu wenye umri wa miaka 18 walidai kwamba walikuwa wamefanya ngono. Hilo linamaanisha kwamba idadi kubwa sana—zaidi ya asilimia 30—hawakuwa wamefanya ngono. Si “kila mtu” anayefanya ngono.

 MAONI YASIYO SAHIHI: Ngono itaimarisha uhusiano wenu.

 JAMBO HAKIKA: Ingawa wavulana fulani husema hivyo ili kujaribu kuwasadikisha wasichana wafanye ngono nao, hilo si kweli. Mara nyingi, mvulana atavunja uhusiano wake na msichana baada ya kufanya ngono naye—jambo ambalo humshtua na kumkasirisha msichana, ambaye alifikiri kijana huyo alimpenda au alikuwa mshikamanifu kwake. a

 MAONI YASIYO SAHIHI: Biblia inapinga ngono.

 JAMBO HAKIKA: Biblia inataka watu wawe na maoni yanayofaa kuhusu ngono lakini inasema kuwa mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa ndio tu wanaoweza kufurahia tendo hilo.—Mwanzo 1:28; 1 Wakorintho 7:3.

 MAONI YASIYO SAHIHI: Kuishi kupatana na Biblia kutafanya maisha yako yachoshe.

 JAMBO HAKIKA: Ukisubiri hadi utakapofunga ndoa ili ufanye ngono, utakuwa na furaha zaidi kwa sababu utaepuka wasiwasi, majuto, na mahangaiko ambayo mara nyingi hutokea mtu anapofanya ngono kabla ya ndoa.

 Jambo kuu: Hakuna mtu ambaye amewahi kuharibu maisha yake kwa sababu ya kusubiri hadi anapofunga ndoa ili afanye ngono. Lakini kufanya ngono kabla ya ndoa kumeharibu maisha ya watu fulani.

 Jinsi ya kupinga shinikizo la kufanya ngono

  •   Imarisha usadikisho wako wa kimaadili. Biblia inasema kwamba watu wakomavu “wamezoeza nguvu zao za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.” (Waebrania 5:14) Wana usadikisho na hivyo si rahisi kwao kushindwa na shinikizo.

     “Nilijitahidi sana kufanya kilicho sawa na kuwa na sifa nzuri, na nilikataa kufanya chochote ambacho kingeharibu sifa hiyo nzuri.”—Alicia, mwenye umri wa miaka 16.

     Jambo la kufikiria: Unataka kuwa na sifa gani? Je, kumpendeza mtu mwingine ni muhimu sana kiasi cha kuharibu sifa hiyo?

  •   Fikiria madhara. Biblia inasema hivi: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.” (Wagalatia 6:7) Wazia kuhusu hali za wakati ujao na ufikirie jinsi maisha yako—na maisha ya mwenzako—yanavyoweza kubadilika unapokubali kushinikizwa kufanya ngono. b

     “Mara nyingi, kufanya ngono kabla ya ndoa hufuatiwa na hisia za hatia, majuto, na pia hisia za kutopendwa—bila kutaja uwezekano wa kupata mimba zisizotarajiwa au ugonjwa wa zinaa.”—Sienna, mwenye umri wa miaka 16.

     Jambo la kufikiria: Kitabu Sex Smart kinauliza: “Ikiwa rafiki zako wanakuchochea kufanya mambo yatakayokuumiza, je, wao ndio aina ya watu unaopaswa kushirikiana nao na kufuata ushauri wao kuhusu masuala muhimu maishani?”

  •   Uwe na maoni yaliyosawazika. Ngono si adui. Biblia inaonyesha kwamba wenzi wa ndoa wanapaswa kufurahia sehemu hiyo ya uhusiano wao.—Methali 5:18, 19.

     “Ngono ni sehemu muhimu ya uumbaji. Mungu anataka tuifurahie, lakini chini ya mpango ambao aliukusudia, yaani, ndoa.”—Jeremy, mwenye umri wa miaka 17.

     Jambo la kufikiria: Siku moja utakapofunga ndoa, utafanya ngono. Wakati huo utaweza kuifurahia, bila kuwa na madhara tuliyotaja awali.

a Bila shaka, si pindi zote ambazo mvulana hujaribu kufanya ngono na msichana. Katika visa vingi, wasichana hujaribu kuwashinikiza wavulana wafanye ngono nao.

b Kati ya madhara unayoweza kupata ni mimba zisizotakikana na—kwa kutegemea umri wa wahusika—matatizo ya kisheria yanayohusu kufanya ngono na watoto.