Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 1)

Nifanye Nini Ikiwa Nina Tatizo la Afya? (Sehemu ya 1)

 Je, unamfahamu kijana anayekabiliana na tatizo la afya? Je, wewe una ugonjwa au udhaifu unaokuzuia kufurahia utendaji ambao wengine walio na umri wako hufurahia?

 Ikiwa ndivyo, ni jambo la kawaida kuvunjika moyo. Hata hivyo, Biblia inataja mambo mawili yenye kufariji sana.

  •   Muumba wako, Yehova Mungu, anafahamu hali yako. Zaidi ya hilo, ‘yeye anakujali wewe.’—1 Petro 5:7.

  •   Yehova Mungu anakusudia kuondoa magonjwa yote! Unaweza kusoma kuhusu jambo hilo katika Isaya 33:24 na Ufunuo 21:1-4.

 Vijana wengi sana wanaokabili matatizo ya afya wameona kwamba imani yao katika Mungu na ahadi zake inawasaidia kuvumilia. Fikiria mifano minne.

 YEIMY

 Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka 11, nililazimika kutumia kiti cha magurudumu. Siwezi kufanya kazi ndogondogo, kama vile kuinua vitu vyepesi.

 Nilipokuwa na umri wa miaka mitano, iligunduliwa kwamba nilikuwa na ugonjwa unaofanya misuli iharibike, na unanizuia nisifanye mengi. Nyakati nyingine mimi huvunjika moyo sana kwa sababu siwezi kufanya mambo ambayo watu wengine wa umri wangu wanaweza kufanya. Lakini wazazi wangu na wengine kutanikoni wananitegemeza kimwili, kihisia, na kiroho. Mimi ni mhudumu wa wakati wote, na mara nyingi Wakristo wenzangu huandamana nami ninapojifunza Biblia pamoja na watu wanaopendezwa.

 Yesu alisema kwamba kila siku ina mahangaiko yake. (Mathayo 6:34) Kwa hiyo, mimi hujaribu kukazia fikira mambo ya leo si ya kesho, nami hujiwekea miradi inayopatana na akili na ninayoweza kufikia. Ninatazamia siku ambayo nitakuwa na “uzima ulio wa kweli,” bila kuwa na ugonjwa wenye kudhoofisha.—1 Timotheo 6:19.

 Jambo la kufikiria: Yeimy ameona inafaa zaidi ‘kujiwekea miradi inayopatana na akili.’ Wewe unawezaje kufanya hivyo?—1 Wakorintho 9:26.

 MATTEO

 Maumivu yangu ya mgongo yalianza nilipokuwa na umri wa miaka sita, na mwanzoni madaktari walisema ni maumivu yanayosababishwa na ukuzi. Hata hivyo, mwaka mmoja baadaye waligundua kwamba nina uvimbe kwenye uti wa mgongo.

 Nilifanyiwa upasuaji, lakini daktari alifaulu tu kutoa asilimia 40 hivi ya uvimbe huo. Kisha—baada ya miezi miwili tu—uvimbe huo ulirudia tena ukubwa wa zamani! Tangu wakati huo, nimefanyiwa uchunguzi mara nyingi, nikafanyiwa matibabu mengi, na nimekatishwa tamaa mara nyingi.

 Nyakati nyingine, uvimbe huo huniletea maumivu makali kana kwamba ninadungwa kwa kisu, hasa mgongoni na kifuani. Hata hivyo, mimi siruhusu hali yangu inilemee. Mimi hujikumbusha kwamba wengine wamefaulu kuvumilia hali ngumu pia, nao wamedumisha mtazamo mzuri. Kile kinachonisaidia zaidi kudumisha mtazamo mzuri ni uhakika wa kwamba siku moja Yehova Mungu atatimiza ahadi yake ya kukomesha kuteseka kote.—Ufunuo 21:4.

 Jambo la kufikiria: Kufikiria kuhusu ahadi ya Mungu ya kukomesha kuteseka kote inawezaje kukusaidia kuvumilia, kama inavyomsaidia Matteo?—Isaya 65:17.

 BRUNA

 Kwa nje sionekani kama mimi ni mgonjwa, kwa hiyo watu fulani hufikiri mimi ni mvivu. Hata hivyo, ni vigumu kwangu kufanya jambo lolote, kutia ndani, kazi za nyumbani, kujifunza, au hata kutoka kitandani.

 Nilipokuwa na umri wa miaka 16, iligunduliwa kuwa nina ugonjwa wa mfumo wa neva, ugonjwa unaomdhoofisha mtu hatua kwa hatua na ambao umeathiri uwezo wangu wa kufanya kazi na pia uwezo wa kushiriki katika utendaji wa Kikristo kwa kadiri ambayo ningependa. Nilisoma mara nyingi maneno ya 1 Petro 5:7: ‘Mtupie Mungu mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali wewe.’ Kujiambia kwamba Yehova anatujali sisi sote mmojammoja kumenipa nguvu. Wazo hilo linaendelea kuniimarisha hadi leo.

 Jambo la kufikiria: Unaweza kunufaikaje kwa kumtupia Yehova mahangaiko yako, kama Bruna anavyofanya?—Zaburi 55:22.

 ANDRÉ

 Watu fulani hunitendea kana kwamba mimi ni mtoto mwenye umri wa miaka 10. Siwezi kuwalaumu; mimi huonekana hivyo.

 Nilipokuwa na umri wa miaka miwili, iligunduliwa kuwa nina aina ya kansa isiyojulikana sana, ambayo iliniathiri kuanzia kwenye uti wa mgongo halafu ikahamia kwenye ubongo. Madaktari walifaulu kudhibiti ugonjwa huo, lakini matibabu hayo yaliathiri ukuzi wangu. Leo nina kimo cha mita 1.37 (futi 4 inchi 6) tu. Watu wengi hufikiri ninawadanganya ninapowaambia kuwa nina umri wa miaka 18!

 Katika kutaniko la Kikristo, watu hunitendea kwa heshima. Hawanisumbui kwa njia za kitoto, kama watoto niliokuwa nao shuleni. Mimi hujaribu kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu hali yangu. Kwa kweli, nimepata jambo bora zaidi ambalo mwanadamu yeyote anaweza kupata—ninamjua Yehova! Nina hakika kwamba Yehova atanisaidia kuvumilia jambo lolote ninalohitaji kukabiliana nacho. Kufikiria kuhusu ulimwengu mpya ambao Yehova Mungu ameahidi kunanisaidia kuendelea kuwa na mtazamo mzuri.—Isaya 33:24.

 Jambo la kufikiria: Kwa nini kumjua Yehova, ndilo “jambo bora zaidi ambalo mwanadamu yeyote anaweza kupata,” kama André alivyosema?—Yohana 17:3.