Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninawezaje Kujifunza Kukazia Fikira?

 Kwa nini Siwezi Kukazia Fikira?

 “Sisomi tena vitabu kama nilivyokuwa nikifanya zamani. Hata sifurahii kusoma mafungu marefu.”—Elaine.

 “Ninasogeza video mbele pindi ninapoanza kuhisi haishi haraka.”—Miranda.

 “Ninapokazia fikira jambo muhimu na mara simu yangu ilie, mimi huanza kufikiria tu, ‘Nani atakuwa amenitumia ujumbe?’”—Jane.

 Je, teknolojia inaweza kufanya iwe vigumu kukazia fikira? Baadhi ya watu husema ndiyo. Nicholas Carr mwandishi na mshauri wa masuala ya usimamizi anasema hivi: “Kadiri tunavyozidi kutumia Intaneti, ndivyo tunavyozidi kuzoeza ubongo wetu kukengeuka—kwa kupitia habari haraka sana na kwa ukamili lakini bila kukazia fikira.” a

 Ona hali tatu ambazo huenda teknolojia ikakukengeusha

  •   Unapokuwa unazungumza. Msichana anayeitwa Maria anasema: “Hata watu wanapozungumza uso kwa uso, bado wanatuma jumbe, wanacheza michezo au wanatumia mitandao ya kijamii—hawakazii fikira mtu wanayezungumza naye.”

  •   Unapokuwa darasani. Kitabu “Digital Kids” kinasema hivi: “Wanafunzi wengi wanasema kwamba wanatumia vifaa vyao vya kielektroni darasani kutuma jumbe, na kuangalia vitu vingine mtandaoni ambavyo havihusiani na wanachojifunza.”

  •   Unapokuwa unasoma. Kijana mwenye umri wa miaka 22 anayeitwa Chris anasema hivi: “Ninajitahidi sana kutotazama simu yangu kila mara inapolia, ikiwa wewe ni mwanafunzi anayesoma shule, unaweza kujikuta ukifanya kazi ya shule kwa saa tatu badala ya saa moja kwa sababu tu ya kukengeushwa.

 Jambo kuu: Utaona ni vigumu sana kukazia fikira ikiwa unaruhusu teknolojia ikukengeushe na kukutawala.

Kutokazia fikira ni kama farasi mwitu anayemwongoza mtu

 Jinsi ya Kuboresha Uwezo wa Kukazia Fikira

  •   Unapokuwa unazungumza. Biblia inasema hivi: ‘Angalieni, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.’ (Wafilipi 2:4) Onyesha ufikirio kwa kusikiliza kwa makini. Watazame wale unaoongea nao na hakikisha vifaa vyako havikukengeushi.

     “Unapozungumza na mtu, jitahidi kutoitazama simu yako. Mwonyeshe heshima mtu unayezungumza naye kwa kumsikiliza kwa makini.”—Thomas.

     DOKEZO: Unapokuwa unazungumza, jaribu kuweka simu yako mahali ambapo hutaiona. Watafiti wanasema kwamba kitendo tu cha kujua iko karibu kunaweza kukukengeusha kwa sababu unatazamia wakati wowote itaita.

  •   Unapokuwa darasani. Biblia inasema hivi: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.” (Luka 8:18) Ukiwa na kanuni hiyo akilini, ikiwa shule yenu inaruhusu wanafunzi kutumia intaneti darasani, epuka kusoma jumbe, kucheza michezo ya simu, au kutuma jumbe wakati ambao unapaswa kukazia fikira masomo.

     “Jitahidi kukazia fikira zaidi darasani. Andika mambo anayofundisha mwalimu. Ikiwezekana, kaa mbele darasani ili kuepuka vikengeusha fikira.”—Karen.

     DOKEZO: Andika mambo makuu kwa mkono badala ya kuandika katika kompyuta. Utafiti unaonyesha kwamba hautakengeushwa sana na utakumbuka unachojifunza.

  •   Unapokuwa unasoma. Biblia inasema hivi: “Jipatie hekima, jipatie uelewaji.” (Methali 4:5) Hilo linatia ndani kufikiria mambo kwa undani badala ya kupitia tu ili kufaulu mtihani.

     “Ninaposoma, ninaweka kifaa changu cha mkononi katika mfumo ambao mtandao hauwezi kushika, nami hukazia fikira ninachofanya. Sichunguzi ikiwa kuna jumbe zilizoingia. Nikikumbuka jambo ambalo ninapaswa kufanya katika simu, ninaliandika pembeni.”—Chris.

     DOKEZO: Hakikisha kwamba unasoma katika mazingira yanayokusaidia kukazia fikira. Yawe safi na yenye mpangilio.

a Kutoka kitabu The Shallows—What the Internet Is Doing to Our Brains.