Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma au Kutumiwa Picha Mtandaoni?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kutuma au Kutumiwa Picha Mtandaoni?

 Umefurahia sana likizo yako, na ungependa kuwaeleza rafiki zako wote kuihusu! Lakini utatumia njia gani? Labda,

  1.   utamtumia kila mtu kadi?

  2.   utawaandikia barua pepe rafiki zako wote?

  3.   utaweka picha kwenye mtandao wa kijamii?

 Babu au bibi (nyanya) yako walipokuwa na umri kama wako huenda njia pekee ambayo wangetumia ni “A”.

 Wazazi wako walipokuwa na umri kama wako huenda wangetumia njia ya “B”.

 Leo, vijana wengi wanaweza kutuma picha mtandaoni, hivyo wangetumia njia ya “C.” Je, wewe ungetumia njia hiyo? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kuepuka hatari fulani zisizoonekana.

 Ina faida gani?

 Ni ya haraka. “Ninapofurahia matembezi au nikifurahia kuwa pamoja na marafiki wangu, ninaweza kutuma picha kuhusu mambo hayo mara moja.”​—Melanie.

 Ni rahisi kutumia. “Ni rahisi zaidi kuangalia picha mpya ambazo marafiki zangu wameweka mtandaoni kuliko kutafuta habari katika barua pepe ili kujua mambo wanayofanya.”​—Jordan.

 Inakusaidia kuwasiliana na wengine. “Baadhi ya marafiki na watu wa familia wanaishi mbali. Wanapoweka picha mtandaoni na ninapozichunguza mara kwa mara, ni kana kwamba ninawaona kila siku!”​—Karen.

 Kuna hatari gani?

 Unaweza kuhatarisha usalama wako. Ikiwa kamera yako ina mfumo wa kutambua mahali ambapo picha ilipigwa, huenda picha ulizoweka mtandaoni zikafunua mengi kukuhusu kuliko unavyofikiri. Tovuti ya Digital Trends iliripoti hivi: “Kuweka picha na vitu vingine mtandaoni na kuonyesha mahali hususa picha hiyo ilipopigwa kunawaruhusu watu mbalimbali ambao wana programu ya kupekua mtandaoni na walio na nia mbaya kutafuta eneo analoishi mtu aliyepiga picha hiyo.”

 Bila shaka, baadhi ya wahalifu wanachunguza kwa makini wajue wakati ambao utaondoka nyumbani kwako. Katika kisa kimoja kilichoripotiwa na Digital Trends, wezi watatu walivunja nyumba 18 wakati ambapo hakukuwa na mtu yeyote nyumbani. Walijuaje kwamba wenye nyumba walikuwa wameondoka? Waliangalia mtandaoni na kuchunguza safari za wakazi wa eneo hilo​—waliiba vitu vyenye thamani ya zaidi ya dola 100,000 za Marekani.

 Unaweza kuona mambo yasiyofaa. Baadhi ya watu hawana aibu ya kuweka mtandaoni picha yoyote ili ulimwengu mzima uione. Tineja anayeitwa Sarah anasema hivi: “Tatizo linakuwa unapoingia katika akaunti ya mtandao wa kijamii ya watu ambao huwajui. Ni sawa na kutembea katika jiji usilolijua bila kuwa na ramani. Mwishowe utafika katika eneo ambalo hukutaka kwenda.”

 Unaweza kupoteza muda wako. Msichana anayeitwa Yolanda anasema hivi: “Ni rahisi kunaswa na mtego wa kuangalia kila picha na maelezo ya kila mtu. Inafikia hatua unataka kuichukua simu yako kila wakati ili tu uangalie kama kuna mambo mapya.”

Unahitaji kujizuia ukiwa na akaunti ya mtandao wa kijamii inayoweza kutuma na kupokea picha

 Tineja anayeitwa Samantha anakubaliana naye. Anasema hivi: “Ninahitaji kupanga wakati wa kutumia mtandao wa kijamii. Unahitaji kujidhibiti sana ikiwa unataka kuwa na akaunti ya mtandao wa kijamii itakayokuwezesha kuangalia na kutuma picha.”

 Unaweza kufanya nini?

  •   Azimia kuepuka mambo yasiyofaa. Biblia inasema hivi: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.”​—Zaburi 101:3.

     “Kila mara ninachunguza mambo waliyoweka watu ninaowafuatilia mtandaoni, nikiona wameweka mambo yasiyofaa ninaacha mara moja kuwafuatilia.”​—Steven.

  •   Epuka kuwasiliana na watu ambao viwango vyao ni tofauti na vyako, kwa kuwa wanaweza kufanya iwe vigumu kwako kudumisha maadili safi. Biblia inasema hivi: “Msipotoshwe. Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”​—1 Wakorintho 15:33.

     “Usifuatilie picha mtandaoni eti kwa sababu watu wengi wanaziangalia. Mara nyingi, kwenye akaunti kama hizo utakuta maneno machafu, picha za watu wakiwa uchi, na mambo mengine yasiyofaa.”​—Jessica.

  •   Jiwekee mipaka ya muda utakaotumia mtandaoni na utatuma picha mara nyingi kadiri gani. Biblia inasema hivi: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa.”​—Waefeso 5:​15, 16.

     “Sifuatilii picha za watu wanaotuma picha mtandaoni kupita kiasi. Kwa mfano, mtu anakwenda ufukweni na kutuma mtandaoni picha 20 za tukio hilohilo moja. Kweli? Unapoteza muda mwingi sana kuangalia picha zote hizo!”​—Rebekah.

  •   Hakikisha picha unazotuma zisifanye wengine wahisi unajionyesha. Mwandikaji wa Biblia Paulo alisema hivi: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” (Waroma 12:3) Usifikiri kwamba ni lazima rafiki zako watavutiwa tu na picha zako au utendaji wako.

     “Baadhi ya watu hutuma picha nyingi walizojipiga. Ikiwa sisi ni marafiki, ninajua jinsi unavyoonekana​—Sihitaji kukumbushwa kila wakati!”​—Allison.