Kumbukumbu la Torati 18:1-22

  • Fungu la makuhani na Walawi (1-8)

  • Mazoea ya kuwasiliana na roho waovu yakatazwa (9-14)

  • Nabii kama Musa (15-19)

  • Jinsi ya kuwatambua manabii wa uwongo (20-22)

18  “Makuhani Walawi, naam, kabila lote la Lawi, halitakuwa na fungu au urithi pamoja na Waisraeli. Watakula dhabihu zinazochomwa kwa moto zinazotolewa kwa Yehova, ambazo ni urithi wake.+  Kwa hiyo hawapaswi kuwa na urithi kati ya ndugu zao. Yehova ndiye urithi wao, kama alivyowaambia.  “Sasa hii ndiyo haki ambayo makuhani wanastahili kutoka kwa watu: Mtu yeyote anayetoa dhabihu, iwe ni ng’ombe dume au kondoo anapaswa kumpa kuhani mguu wa mbele, mataya, na tumbo.  Mnapaswa kumpa mazao ya kwanza ya nafaka yenu, divai yenu mpya, mafuta yenu, na manyoya ya kwanza yaliyokatwa ya kondoo wenu.+  Yehova Mungu wenu amewachagua wao pamoja na wana wao kutoka kati ya makabila yenu yote ili wahudumu katika jina la Yehova daima.+  “Lakini ikiwa Mlawi ataondoka katika mojawapo ya majiji yenu katika Israeli alimokuwa akiishi,+ naye angependa kwenda mahali ambapo Yehova anachagua,*+  anaweza kuhudumu huko katika jina la Yehova Mungu wake kama wanavyofanya ndugu zake wote, Walawi, wanaosimama huko mbele za Yehova.+  Atapokea kiasi kilekile cha chakula pamoja nao,+ mbali na malipo anayopata baada ya kuuza mali za mababu zake.  “Mtakapoingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, msijifunze kuiga mazoea yenye kuchukiza ya mataifa hayo.+ 10  Asipatikane miongoni mwenu mtu yeyote anayemteketeza* motoni+ mwanawe au binti yake, mtu yeyote anayefanya uaguzi,*+ mtu yeyote anayefanya uchawi,+ mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri,+ mlozi,+ 11  mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho,+ mpiga ramli,+ au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu.+ 12  Kwa maana mtu yeyote anayefanya mambo haya ni chukizo kwa Yehova, na kwa sababu ya mazoea haya yanayochukiza, Yehova Mungu wenu anayafukuza mataifa hayo kutoka mbele yenu. 13  Mnapaswa kudhihirisha kwamba hamna lawama mbele za Yehova Mungu wenu.+ 14  “Kwa maana mataifa haya mnayomiliki nchi yao yalikuwa yakiwasikiliza wale waliozoea uchawi+ na uaguzi,*+ lakini Yehova Mungu wenu hajawaruhusu mfanye jambo lolote kama hilo. 15  Yehova Mungu wenu atawainulia nabii kama mimi kutoka kati ya ndugu zenu. Ni lazima mumsikilize.+ 16  Kwa sababu hilo ndilo mlilomwomba Yehova Mungu wenu kule Horebu katika siku ya kusanyiko,*+ mliposema, ‘Usiache tusikie sauti ya Yehova Mungu wetu au kuona tena moto huu mkubwa, tusije tukafa.’+ 17  Kisha Yehova akaniambia, ‘Jambo walilosema ni sawa. 18  Nitawainulia nabii+ kama wewe kutoka kati ya ndugu zao, nami nitaweka maneno yangu katika kinywa chake,+ naye atawaambia mambo yote nitakayomwamuru.+ 19  Naam, nitamwadhibu kila mtu ambaye hatasikiliza maneno yangu ambayo nabii huyo atasema katika jina langu.+ 20  “‘Ikiwa nabii yeyote atasema kwa kimbelembele katika jina langu neno ambalo sikumwamuru aseme au kusema katika jina la miungu mingine, nabii huyo lazima afe.+ 21  Lakini huenda mkasema hivi mioyoni mwenu: “Tutajuaje Yehova hajasema neno hilo?” 22  Nabii akisema neno katika jina la Yehova na neno hilo lisitimie au kufanyika, basi Yehova hakusema neno hilo. Nabii huyo alilisema kwa kimbelembele. Hampaswi kumwogopa.’

Maelezo ya Chini

Yaani, mahali ambapo Yehova anachagua kuwa kitovu cha ibada.
Au “anayebashiri.”
Tnn., “anayempitisha.”
Au “ubashiri.”
Au “kukutanika.”