Kumbukumbu la Torati 15:1-23

  • Madeni yafutwa kila mwaka wa saba (1-6)

  • Kuwasaidia maskini (7-11)

  • Kuwaachilia huru watumwa kila mwaka wa saba (12-18)

    • Kutoboa sikio la mtumwa kwa msumari (16, 17)

  • Wazaliwa wa kwanza wa wanyama watakaswa (19-23)

15  “Mwishoni mwa kila miaka saba mnapaswa kufuta madeni.+  Hivi ndivyo mtakavyoyafuta: Kila mtu aliyemkopesha jirani yake atafuta deni hilo. Hapaswi kudai malipo kutoka kwa jirani au ndugu yake, kwa maana yatatangazwa yamefutwa kwa agizo la Yehova.+  Mnaweza kudai malipo kutoka kwa mgeni,+ lakini mnapaswa kufuta deni lolote la ndugu yenu.  Hata hivyo, hakuna yeyote kati yenu anayepaswa kuwa maskini, kwa sababu hakika Yehova atawabariki+ katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa mwimiliki kama urithi,  lakini ikiwa tu mtatii kabisa sauti ya Yehova Mungu wenu na kushika kwa uangalifu amri yote hii ninayowapa leo.+  Kwa maana Yehova Mungu wenu atawabariki kama alivyowaahidi, nanyi mtayakopesha mataifa mengi, lakini ninyi hamtahitaji kukopa;+ nanyi mtatawala mataifa mengi, lakini hayatawatawala.+  “Ikiwa mmoja wa ndugu zenu atakuwa maskini miongoni mwenu katika mojawapo ya majiji yaliyo katika nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa, msiifanye mioyo yenu iwe migumu au kumfumbia mkono ndugu yenu maskini.+  Kwa maana mnapaswa kumfumbulia mkono wenu kwa ukarimu+ na kufanya yote mwezayo kumkopesha* chochote anachohitaji au alichopungukiwa.  Jihadharini wazo hili ovu lisiingie mioyoni mwenu: ‘Mwaka wa saba, mwaka wa kufuta madeni, umekaribia,’+ na hivyo mkatae kumtendea kwa ukarimu ndugu yenu aliye maskini na kukosa kumpa chochote. Akimlilia Yehova kuwahusu ninyi, mtakuwa mmetenda dhambi.+ 10  Mnapaswa kumpa kwa ukarimu,+ nanyi hampaswi* kumpa huku mkinung’unika, kwa sababu hiyo Yehova Mungu wenu atabariki kila kazi na kila jambo mnalofanya.+ 11  Kwa maana sikuzote kutakuwa na maskini nchini.+ Ndiyo sababu ninawaamuru hivi: ‘Mnapaswa kumfumbulia mkono wenu kwa ukarimu ndugu yenu anayeteseka na maskini katika nchi yenu.’+ 12  “Ikiwa uliuziwa ndugu yako, mwanamume au mwanamke Mwebrania, naye amekutumikia kwa miaka sita, basi katika mwaka wa saba unapaswa kumwachilia huru.+ 13  Na ikiwa utamwachilia huru, usimwache aende mikono mitupu. 14  Mpe kwa ukarimu kitu fulani kutoka katika mifugo yako, uwanja wako wa kupuria, na shinikizo lako la mafuta na divai. Unapaswa kumpa kama vile ambavyo Yehova Mungu wako amekubariki. 15  Kumbuka kwamba ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri na Yehova Mungu wako akakukomboa. Ndiyo sababu leo ninakuamuru ufanye hivyo. 16  “Lakini akikuambia, ‘Sitakuacha!’ kwa sababu anakupenda wewe na familia yako, kwa maana amefurahia kuwa pamoja nawe,+ 17  utachukua msumari na kutoboa sikio lake kwa msumari huo mpaka upenye mlangoni, naye atakuwa mtumwa wako daima. Utamfanyia kijakazi wako vivyo hivyo. 18  Usione vigumu kumwachilia huru, naye aondoke, kwa sababu thamani ya utumishi wake kwa miaka sita aliyokutumikia ni mara mbili ya thamani ya utumishi wa mfanyakazi aliyeajiriwa, na Yehova Mungu wako amekubariki katika kila jambo ambalo lilifanywa. 19  “Unapaswa kumtakasa kila mzaliwa wa kwanza wa kiume wa ng’ombe wako na kondoo wako kwa ajili ya Yehova Mungu wako.+ Usimtumie mzaliwa wa kwanza wa ng’ombe dume wako kufanya kazi yoyote wala usimkate manyoya mzaliwa wa kwanza wa kondoo wako. 20  Wewe na familia yako mnapaswa kumla mbele za Yehova Mungu wenu mwaka baada ya mwaka mahali ambapo Yehova Mungu wenu atachagua.+ 21  Lakini ikiwa ana kasoro, yaani, ni mlemavu, ni kipofu, au ana kasoro nyingine kubwa, usimtoe dhabihu kwa Yehova Mungu wako.+ 22  Mnapaswa kumla ndani ya majiji* yenu, mtu asiye safi na aliye safi watamla, kama mnavyokula swala au paa.+ 23  Lakini hampaswi kula damu yake;+ mtaimwaga ardhini kama maji.+

Maelezo ya Chini

Au “kumkopesha kwa rehani.”
Tnn., “moyo wenu haupaswi.”
Tnn., “malango.”