Kumbukumbu la Torati 3:1-29

  • Wamshinda Mfalme Ogu wa Bashani (1-7)

  • Kugawanywa kwa nchi upande wa mashariki wa Yordani (8-20)

  • Yoshua aambiwa asiogope (21, 22)

  • Musa hataingia katika nchi hiyo (23-29)

3  “Kisha tuligeuka na kupanda kupitia njia ya Bashani. Ndipo Ogu, mfalme wa Bashani, akatoka pamoja na watu wake wote ili kupigana vita nasi kule Edrei.+  Basi Yehova akaniambia, ‘Usimwogope, kwa maana nitamtia mikononi mwako pamoja na watu wake wote na nchi yake, nawe utamtendea kama ulivyomtendea Sihoni mfalme wa Waamori, aliyeishi Heshboni.’  Basi Yehova Mungu wetu akamtia pia mikononi mwetu Mfalme Ogu wa Bashani pamoja na watu wake wote, nasi tukaendelea kumshambulia hivi kwamba hakuna mtu yeyote kati ya watu wake aliyeokoka.  Kisha tukateka majiji yake yote. Hakuna mji wao hata mmoja ambao hatukuuteka, tuliteka majiji 60 katika eneo lote la Argobu, yaani, ufalme wa Ogu kule Bashani.+  Majiji hayo yote yalikuwa na kuta ndefu zenye ngome, malango, na makomeo, tuliteka pia miji mingi sana ya mashambani.  Hata hivyo, tuliwaangamiza,+ kama tulivyomwangamiza Mfalme Sihoni wa Heshboni, tuliangamiza kila jiji, kutia ndani wanaume, wanawake, na watoto.+  Nasi tukajichukulia mifugo yote na nyara za majiji hayo.  “Wakati huo tulichukua nchi ya wafalme wawili wa Waamori+ waliokuwa katika eneo la Yordani, kuanzia Bonde* la Arnoni mpaka Mlima Hermoni+  (Wasidoni walikuwa wakiuita mlima huo Sirioni, nao Waamori walikuwa wakiuita Seniri), 10  majiji yote yaliyokuwa katika nchi tambarare, nchi yote ya Gileadi, nchi yote ya Bashani mpaka Saleka na Edrei,+ majiji ya ufalme wa Ogu kule Bashani. 11  Kwa maana Mfalme Ogu wa Bashani ndiye Mrefaimu pekee aliyekuwa amebaki. Jeneza lake lilitengenezwa kwa chuma,* na bado liko katika jiji la Waamoni la Raba. Lina urefu wa mikono tisa* na upana wa mikono minne, kulingana na kipimo cha kawaida cha mkono. 12  Wakati huo tulimiliki nchi hii: kuanzia Aroeri,+ karibu na Bonde* la Arnoni, na nusu ya eneo lenye milima la Gileadi, na majiji yake nimewapa watu wa kabila la Rubeni na kabila la Gadi.+ 13  Kisha nusu ya kabila la Manase+ nimewapa sehemu inayobaki ya Gileadi na eneo lote la Bashani la ufalme wa Ogu. Eneo lote la Argobu, la Bashani, lilijulikana kuwa nchi ya Warefaimu. 14  “Yairi+ mwana wa Manase alichukua eneo lote la Argobu+ hadi kwenye mpaka wa Wageshuri na Wamaakathi,+ akaviita vijiji hivyo vya Bashani kwa jina lake mwenyewe, Hawoth-yairi,*+ mpaka leo. 15  Naye Makiri nimempa Gileadi.+ 16  Na watu wa kabila la Rubeni na kabila la Gadi+ nimewapa kuanzia Gileadi mpaka kwenye Bonde* la Arnoni, katikati ya bonde ulikuwa ndio mpaka, hadi Bonde la Yaboki, ambalo ni mpaka wa Waamoni, 17  na Araba na Yordani na ule mpaka, kuanzia Kinerethi hadi Bahari ya Araba, Bahari ya Chumvi, chini ya mteremko wa Pisga kuelekea upande wa mashariki.+ 18  “Kisha nikawaamuru hivi: ‘Yehova Mungu wenu amewapa nchi hii mwimiliki. Wanaume wenu wote mashujaa watachukua silaha na kuvuka mbele ya ndugu zenu, Waisraeli.+ 19  Lakini wake zenu, watoto wenu, na wanyama wenu tu (najua vizuri kwamba mna wanyama wengi sana) ndio watakaoendelea kukaa katika majiji ambayo nimewapa, 20  mpaka Yehova atakapowapumzisha ndugu zenu, kama anavyowapumzisha ninyi, nao pia waimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ng’ambo ya Yordani. Ndipo mtakaporudi, kila mmoja atarudi kwenye miliki yake ambayo nimempa.’+ 21  “Wakati huo nilimwamuru hivi Yoshua:+ ‘Umeona kwa macho yako mwenyewe mambo ambayo Yehova Mungu wako amewatendea wafalme hao wawili. Hivyo ndivyo Yehova atakavyozitendea falme zote huko mnakovuka kwenda.+ 22  Msiwaogope, kwa maana Yehova Mungu wenu ndiye anayewapigania ninyi.’+ 23  “Wakati huo nilimsihi hivi Yehova: 24  ‘Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, umeanza kumwonyesha mtumishi wako ukuu wako na mkono wako wenye nguvu,+ kwa maana ni mungu gani mbinguni au duniani anayetenda mambo makuu kama wewe?+ 25  Tafadhali niruhusu nivuke na kuona nchi nzuri iliyo ng’ambo ya Yordani, eneo hili zuri lenye milima na Lebanoni.’+ 26  Lakini bado Yehova alikuwa amenikasirikia vikali kwa sababu yenu,+ naye hakutaka kunisikiliza. Badala yake Yehova aliniambia, ‘Imetosha! Usizungumze nami tena kamwe kuhusu jambo hili. 27  Panda juu ya kilele cha Pisga,+ utazame magharibi na kaskazini na kusini na mashariki, uone nchi hiyo kwa macho yako, kwa maana hutavuka mto huu wa Yordani.+ 28  Nawe umweke Yoshua+ kuwa kiongozi, umtie moyo na kumwimarisha, kwa sababu yeye ndiye atakayewaongoza watu hawa kuvuka+ na kuwawezesha kuirithi nchi utakayoiona.’ 29  Mambo hayo yote yalitendeka tulipokuwa tukikaa katika bonde lililo mbele ya Beth-peori.+

Maelezo ya Chini

Au “Korongo.”
Au “jiwe jeusi la volkano.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “Korongo.”
Maana yake “Vijiji vya Mahema vya Yairi.”
Au “Korongo.”