Matendo ya Mitume 19:1-41

  • Paulo huko Efeso; baadhi ya watu wabatizwa tena (1-7)

  • Paulo ajishughulisha na kazi ya kufundisha (8-10)

  • Mafanikio licha ya roho waovu (11-20)

  • Machafuko huko Efeso (21-41)

19  Apolo+ alipokuwa Korintho, Paulo alipita bara na kushuka mpaka Efeso.+ Aliwakuta wanafunzi fulani huko  akawauliza: “Mlipoanza kuamini, je, mlipokea roho takatifu?”+ Wakamjibu: “Hata hatujasikia kwamba kuna roho takatifu.”  Basi akawauliza: “Mlibatizwa katika nini?” Wakajibu: “Katika ubatizo wa Yohana.”+  Paulo akasema: “Yohana aliwabatiza watu ili kuonyesha kwamba wametubu,+ akiwaambia wamwamini yule ambaye angekuja baada yake,+ yaani, Yesu.”  Waliposikia hivyo, wakabatizwa katika jina la Bwana Yesu.  Paulo alipoweka mikono juu yao, wakapokea roho takatifu,+ nao wakaanza kuzungumza kwa lugha za kigeni na kutoa unabii.+  Wote walikuwa wanaume karibu 12.  Akaingia katika sinagogi,+ na kwa miezi mitatu akazungumza kwa ujasiri, akitoa hotuba na kujadiliana kwa ushawishi kuhusu Ufalme wa Mungu.+  Lakini baadhi yao wakawa wagumu* na wakakataa kuamini, huku wakizungumza vibaya kuhusu Ile Njia+ mbele ya umati. Basi akawaacha+ na kuwatenga wanafunzi kutoka kwao, na kila siku alikuwa akitoa hotuba katika ukumbi wa shule ya Tirano. 10  Aliendelea kufanya hivyo kwa miaka miwili, hivi kwamba wote walioishi katika mkoa wa Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia. 11  Na Mungu akaendelea kufanya matendo yenye nguvu yasiyo ya kawaida kupitia mikono ya Paulo,+ 12  hivi kwamba hata nguo na vitambaa vilivyogusa mwili wake vilipelekewa wagonjwa,+ nao wakaponywa magonjwa, na roho waovu wakatoka.+ 13  Lakini baadhi ya Wayahudi waliosafiri huku na huku wakifukuza roho waovu wakajaribu pia kutumia jina la Bwana Yesu kwa wale waliokuwa na roho waovu; wakisema: “Ninakuamuru kwa jina la Yesu ambaye Paulo humhubiri.”+ 14  Wana saba wa Skewa, mkuu wa makuhani wa Kiyahudi, walikuwa wakifanya hivyo. 15  Lakini yule roho mwovu akawaambia: “Ninamjua Yesu+ nami ninamfahamu Paulo;+ lakini ninyi ni nani?” 16  Ndipo mtu huyo aliyekuwa na roho mwovu akawarukia, akawazidi nguvu mmoja baada ya mwingine na kuwashinda, hivi kwamba wakatoka mbio katika nyumba hiyo wakiwa uchi na wakiwa wameumizwa. 17  Watu wote wakajua jambo hilo, Wayahudi na Wagiriki walioishi huko Efeso; na wote wakaogopa, nalo jina la Bwana Yesu likaendelea kutukuzwa. 18  Na wengi kati ya wale waliokuwa waamini walikuwa wakija na kuungama, wakieleza waziwazi kuhusu mazoea yao. 19  Kwa kweli, idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na kuviteketeza mbele ya kila mtu.+ Nao wakafanya hesabu na kupata vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya vipande 50,000 vya fedha. 20  Hivyo kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova* likazidi kukua na kusitawi.+ 21  Baada ya mambo hayo kutukia, Paulo akaazimia katika roho yake kwamba baada ya kupitia Makedonia+ na Akaya, atasafiri kwenda Yerusalemu.+ Akasema: “Baada ya kwenda huko, lazima pia nione Roma.”+ 22  Basi akawatuma wawili kati ya wale waliomhudumia, Timotheo+ na Erasto,+ waende Makedonia lakini yeye akakaa kwa muda fulani katika mkoa wa Asia. 23  Wakati huo kukatokea mvurugo+ mkubwa kuhusu Ile Njia.+ 24  Kwa maana mtu fulani aliyeitwa Demetrio, fundi wa fedha aliyetengeneza vihekalu vya fedha vya Artemi, aliwaletea mafundi faida kubwa.+ 25  Akawakusanya pamoja na wengine waliofanya kazi kama hiyo na kuwaambia: “Wanaume, mnajua vema kwamba tunapata mafanikio yetu kutokana na biashara hii. 26  Sasa mnaona na kusikia kwamba si katika Efeso tu,+ bali pia katika karibu mkoa wote wa Asia, Paulo huyu ameushawishi umati mkubwa na kuwafanya wawe na maoni tofauti, akisema kwamba miungu iliyotengenezwa kwa mikono, kwa kweli si miungu.+ 27  Isitoshe, kuna hatari kwamba biashara yetu itapata sifa mbaya na pia hekalu la Artemi mungu mkuu wa kike litaonwa kuwa si kitu, naye anayeabudiwa katika mkoa wote wa Asia na dunia inayokaliwa atakosa utukufu.” 28  Waliposikia jambo hilo wakajawa na hasira, nao wakaanza kusema kwa sauti kubwa: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” 29  Basi jiji likajaa mvurugo na wote pamoja wakakimbia na kuingia katika ukumbi wa maonyesho, wakiwakokota Gayo na Aristarko,+ Wamakedonia waliokuwa wakisafiri pamoja na Paulo. 30  Naye Paulo alitaka kuingia walimokuwa watu hao, lakini wanafunzi hawakumruhusu. 31  Hata baadhi ya wasimamizi wa sherehe na michezo waliomtendea kwa urafiki, wakamtumia ujumbe wakimsihi asijihatarishe kwa kuingia katika ukumbi wa maonyesho. 32  Kwa kweli, baadhi yao walikuwa wakisema kwa sauti kubwa jambo moja na wengine jambo tofauti; kwa maana kusanyiko hilo lilikuwa limevurugika, na wengi wao hawakujua kwa nini walikuwa wamekusanyika. 33  Basi wakamtoa Aleksanda kwenye umati, huku Wayahudi wakimsukuma mbele, naye Aleksanda akapunga mkono akitaka kujitetea mbele ya watu. 34  Lakini walipotambua kwamba alikuwa Myahudi, wote wakaanza kupaza sauti kwa pamoja kwa karibu saa mbili wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” 35  Mwishowe, karani wa jiji akaunyamazisha umati, kisha akasema: “Watu wa Efeso, kwa kweli ni nani kati ya wanadamu ambaye hajui kwamba jiji la Efeso ndilo mlinzi wa hekalu la Artemi mkuu na sanamu iliyoanguka kutoka mbinguni? 36  Kwa kuwa mambo haya hayawezi kukanushwa, tulieni na msitende haraka haraka. 37  Kwa maana mmewaleta hapa watu hawa ambao hawaibi katika mahekalu wala kumkufuru mungu wetu wa kike. 38  Basi ikiwa Demetrio+ na mafundi walio pamoja naye wana kesi dhidi ya mtu fulani, siku za mahakama hufanywa na kuna maliwali;* wanaweza kushtakiana huko. 39  Lakini ikiwa mnatafuta jambo lingine zaidi ya hilo, linapaswa kuamuliwa katika kusanyiko la kawaida. 40  Kwa kweli tunakabili hatari ya kushtakiwa kwa uchochezi kuhusu tukio la leo, kwa sababu hatuna msingi wa kuwa na kikundi hiki chenye machafuko.” 41  Baada ya kusema mambo hayo, akauagiza umati utawanyike.

Maelezo ya Chini

Au “wakawa wakaidi.”
Liwali alikuwa gavana Mroma aliyetawala mkoa. Angalia Kamusi.