Matendo ya Mitume 14:1-28

  • Ongezeko na upinzani huko Ikoniamu (1-7)

  • Wadhaniwa kuwa miungu huko Listra (8-18)

  • Paulo aokoka kufa baada ya kupigwa mawe (19, 20)

  • Kuyaimarisha makutaniko (21-23)

  • Kurudi huko Antiokia ya Siria (24-28)

14  Basi huko Ikoniamu wakaingia pamoja katika sinagogi la Wayahudi, wakazungumza vizuri hivi kwamba umati mkubwa wa Wayahudi na pia Wagiriki wakawa waamini.  Lakini Wayahudi ambao hawakuamini wakawachochea watu* wa mataifa na kuwafanya wawachukie akina ndugu.+  Basi wakatumia muda mrefu wakizungumza kwa ujasiri kwa mamlaka ya Yehova,* aliyetoa ushahidi kuhusu neno la fadhili zake zisizostahiliwa kwa kuwaruhusu wafanye ishara na mambo ya ajabu.*+  Hata hivyo, umati wa jiji ulikuwa umegawanyika; baadhi yao walikuwa upande wa Wayahudi lakini wengine upande wa mitume.  Watu wa mataifa na Wayahudi, pamoja na watawala wao walipojaribu kuwatendea kwa dharau na kuwapiga mawe,+  wakajulishwa jambo hilo, nao wakakimbilia majiji ya Likaonia, Listra na Derbe, na maeneo yaliyokuwa karibu.+  Wakiwa huko, wakaendelea kutangaza habari njema.  Huko Listra, kulikuwa na mwanamume aliyekuwa ameketi akiwa amelemaa miguu. Alikuwa kiwete tangu kuzaliwa na hakuwa ametembea kamwe.  Mtu huyo alikuwa akimsikiliza Paulo alipokuwa akizungumza. Paulo alipomtazama kwa makini na kuona kwamba ana imani ya kuponywa,+ 10  akasema kwa sauti kubwa: “Simama kwa miguu yako.” Ndipo yule mwanamume akaruka na kuanza kutembea.+ 11  Umati ulipoona jambo alilofanya Paulo, wakasema kwa sauti kubwa katika lugha ya Kilikaonia: “Miungu imekuwa kama wanadamu nayo imeshuka kwetu!”+ 12  Wakaanza kumwita Barnaba Zeu, naye Paulo wakamwita Herme, kwa kuwa ndiye aliyeongoza katika mazungumzo. 13  Naye kuhani wa Zeu, ambaye hekalu lake lilikuwa kwenye mwingilio wa jiji, akawaleta ng’ombe dume na mashada ya maua kwenye malango, naye alitaka kutoa dhabihu pamoja na umati. 14  Hata hivyo, mitume Barnaba na Paulo waliposikia jambo hilo, wakayararua mavazi yao na kuruka ndani ya umati wakisema kwa sauti kubwa: 15  “Wanaume, kwa nini mnafanya mambo haya? Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu kama wenu.+ Nasi tunawatangazia habari njema, ili mgeuke kutoka katika mambo haya ya bure mje kwa Mungu aliye hai, aliyeumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.+ 16  Katika vizazi vilivyopita aliruhusu watu wa mataifa yote waendelee kutembea katika njia zao,+ 17  ingawa hakujiacha bila ushahidi+ kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira ya mavuno,+ akiwashibisha kwa chakula na kuijaza mioyo yenu furaha.”+ 18  Na ingawa walisema mambo hayo, haikuwa rahisi kwao kuuzuia umati kuwatolea dhabihu. 19  Lakini Wayahudi wakafika kutoka Antiokia na Ikoniamu wakaushawishi umati,+ nao wakampiga Paulo kwa mawe na kumkokota nje ya jiji, wakiwazia kwamba amekufa.+ 20  Hata hivyo, wanafunzi walipomzunguka, akasimama na kuingia jijini. Siku iliyofuata akaondoka pamoja na Barnaba kwenda Derbe.+ 21  Baada ya kulitangazia jiji hilo habari njema na kuwafanya watu wengi kuwa wanafunzi, wakarudi Listra, Ikoniamu, na Antiokia. 22  Wakiwa huko wakawatia nguvu wanafunzi*+ na kuwatia moyo wabaki katika imani wakisema: “Ni lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.”+ 23  Isitoshe, wakawaweka rasmi wazee kwa ajili yao katika kila kutaniko,+ wakatoa sala na kufunga,+ nao wakawakabidhi kwa Yehova* ambaye walikuwa wamemwamini. 24  Kisha wakapitia Pisidia wakaingia Pamfilia,+ 25  na baada ya kulitangaza neno huko Perga, wakashuka kwenda Atalia. 26  Kutoka huko wakasafiri baharini kwenda Antiokia, ambako walikuwa wamekabidhiwa kwenye fadhili zisizostahiliwa za Mungu kwa ajili ya kazi ambayo sasa walikuwa wamemaliza.+ 27  Walipofika na kulikusanya kutaniko pamoja, wakawasimulia mambo mengi ambayo Mungu alikuwa amefanya kupitia kwao, na kwamba alikuwa amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.+ 28  Basi wakakaa pamoja na wanafunzi kwa muda mrefu.

Maelezo ya Chini

Au “nafsi za watu.”
Au “miujiza.”
Au “wakazitia nguvu nafsi za wanafunzi.”