Kitabu cha Pili cha Samweli 12:1-31

  • Nathani amkaripia Daudi (1-15a)

  • Mwana wa Bath-sheba afa (15b-23)

  • Bath-sheba amzaa Sulemani (24, 25)

  • Jiji la Raba la Waamoni latekwa (26-31)

12  Kwa hiyo Yehova akamtuma Nathani+ kwa Daudi. Akafika kwake+ na kumwambia: “Kulikuwa na wanaume wawili katika jiji moja, mmoja alikuwa tajiri na mwingine maskini.  Yule mwanamume tajiri alikuwa na kondoo wengi sana na ng’ombe;+  lakini yule mwanamume maskini hakuwa na chochote isipokuwa mwanakondoo mmoja jike mdogo aliyekuwa amemnunua.+ Alimtunza mwanakondoo huyo, naye akakua nyumbani mwake pamoja na wanawe. Mwanakondoo huyo alikuwa akila chakula kidogo alichokuwa nacho mtu huyo na kunywea kikombe chake, naye alikuwa akilala mikononi mwake. Mwanakondoo huyo akawa kama binti kwake.  Baadaye mgeni alimtembelea yule mwanamume tajiri, lakini mwanamume huyo hakutaka kuchukua mmoja wa kondoo wake mwenyewe au ng’ombe wake ili amchinjie msafiri aliyemtembelea. Badala yake alimchukua mwanakondoo wa yule mwanamume maskini na kumchinjia mgeni aliyemtembelea.”+  Daudi aliposikia hayo, alikasirika sana kwa sababu ya mwanamume huyo, akamwambia Nathani: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi,+ mwanamume aliyefanya hivyo anastahili kufa!  Naye anapaswa kulipa mara nne zaidi kwa ajili ya mwanakondoo huyo,+ kwa sababu alifanya jambo hilo na hakuwa na huruma.”  Ndipo Nathani akamwambia Daudi: “Mwanamume huyo ni wewe! Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mimi mwenyewe nilikutia mafuta uwe mfalme wa Israeli,+ nami nilikuokoa kutoka mikononi mwa Sauli.+  Nilikuwa tayari kukupa nyumba ya bwana wako+ na kuwaweka mikononi mwako wake za+ bwana wako, nami nikakupa nyumba ya Israeli na ya Yuda.+ Na kana kwamba hayo hayatoshi, nilikuwa tayari kukufanyia mengi zaidi.+  Kwa nini ulilidharau neno la Yehova, kwa kutenda lililo ovu machoni pake? Ulimuua Uria Mhiti kwa upanga!+ Kisha ukamchukua mke wake awe mke wako+ baada ya kumuua Uria kwa upanga wa Waamoni.+ 10  Sasa upanga hautaondoka nyumbani mwako,+ kwa sababu ulinidharau kwa kumchukua mke wa Uria Mhiti awe mke wako.’ 11  Yehova anasema hivi: ‘Tazama, ninakuletea msiba kutoka katika nyumba yako mwenyewe;+ na mbele ya macho yako mwenyewe, nami nitawachukua wake zako na kumpa mwanamume mwingine,+ naye atalala na wake zako kweupe kabisa wakati wa mchana.*+ 12  Ingawa ulifanya jambo hilo kwa siri,+ mimi nitafanya jambo hili mbele ya Waisraeli wote kweupe kabisa wakati wa mchana.’”* 13  Ndipo Daudi akamwambia Nathani: “Nimemtendea Yehova dhambi.”+ Nathani akamwambia Daudi: “Yehova naye amekusamehe dhambi uliyotenda.*+ Hutakufa.+ 14  Hata hivyo, kwa sababu hukumheshimu Yehova kamwe katika jambo hili, mwana wako aliyezaliwa hivi punde, hakika atakufa.” 15  Kisha Nathani akaenda nyumbani kwake. Basi Yehova akamletea pigo mtoto ambaye mke wa Uria alikuwa amemzalia Daudi, akawa mgonjwa. 16  Daudi akamsihi sana Mungu wa kweli kwa ajili ya mvulana huyo. Daudi akafunga kabisa, naye alikuwa akiingia chumbani mwake na kulala chini usiku kucha.+ 17  Basi wazee wa nyumbani mwake wakasimama karibu naye na kujaribu kumwinua kutoka sakafuni, lakini alikataa, wala hakula pamoja nao. 18  Siku ya saba yule mtoto akafa, lakini watumishi wa Daudi wakaogopa kumwambia kwamba mtoto amekufa. Walisema: “Mtoto alipokuwa hai tulizungumza naye lakini hakutusikiliza. Sasa tutamwambiaje kwamba mtoto amekufa? Huenda akatenda jambo baya sana.” 19  Daudi alipowaona watumishi wake wakinong’onezeana, alitambua kwamba yule mtoto amekufa. Daudi akawauliza: “Mtoto amekufa?” Wakajibu: “Amekufa.” 20  Basi Daudi akainuka kutoka sakafuni. Akaoga, akajipaka mafuta,+ akabadili nguo zake, akaenda katika nyumba ya Yehova+ na kusujudu. Kisha akaenda nyumbani kwake* na kuomba aletewe chakula, naye akala. 21  Watumishi wake wakamuuliza: “Kwa nini umefanya hivi? Mtoto alipokuwa hai, ulifunga na kulia daima; lakini mara tu mtoto alipokufa ukainuka na kula chakula.” 22  Akajibu: “Mtoto alipokuwa hai, nilifunga+ na kulia daima kwa sababu nilisema moyoni, ‘Ni nani ajuaye kama Yehova atanionyesha kibali na kumwacha mtoto aishi?’+ 23  Sasa kwa kuwa amekufa, kwa nini nifunge? Je, naweza kumrudisha tena?+ Mimi nitamfuata,+ lakini yeye hatanirudia mimi.”+ 24  Kisha Daudi akamfariji Bath-sheba mke wake.+ Akaingia kwake na kulala naye. Baada ya muda akazaa mwana, akapewa jina Sulemani.*+ Yehova akampenda mwana huyo,+ 25  akamtuma nabii Nathani+ amwite mtoto huyo Yedidia,* kwa ajili ya Yehova. 26  Yoabu akaendelea kupigana na jiji la Raba+ la Waamoni,+ akaliteka jiji hilo la kifalme.*+ 27  Basi Yoabu akawatuma wajumbe kwa Daudi akisema: “Nimepigana na Raba,+ nami nimeliteka jiji lenye maji.* 28  Sasa wakusanye wanajeshi waliobaki, upige kambi dhidi ya jiji hilo na kuliteka. La sivyo, mimi ndiye nitakayeliteka jiji hilo, na kusifiwa kwa kuliteka.”* 29  Basi Daudi akawakusanya wanajeshi wote na kwenda Raba, akapigana nalo na kuliteka. 30  Kisha akachukua taji lililokuwa kwenye kichwa cha Malkamu. Uzito wa taji hilo ulikuwa talanta moja* ya dhahabu, nalo lilikuwa na mawe yenye thamani, Daudi akavishwa taji hilo kichwani. Alichukua pia nyara nyingi sana+ kutoka katika jiji hilo.+ 31  Akawatoa nje watu waliokuwa ndani yake, akawapa kazi ya kukata mawe kwa misumeno, vifaa vya chuma vyenye ncha kali na mashoka ya chuma, na kazi ya kufyatua matofali. Hivyo ndivyo alivyofanya katika majiji yote ya Waamoni. Hatimaye Daudi na wanajeshi wote wakarudi Yerusalemu.

Maelezo ya Chini

Au “juani.”
Au “juani.”
Au “amefutilia mbali dhambi yako.”
Au “katika jumba lake la mfalme.”
Jina hilo linatokana na neno la Kiebrania linalomaanisha “Amani.”
Maana yake “Mpendwa wa Yah.”
Au “jiji la ufalme huo.”
Huenda maneno haya yanarejelea vyanzo vya maji vya jiji hilo.
Tnn., “nalo litaitwa kwa jina langu.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.