Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 21:1-29

  • Ahabu atamani shamba la mizabibu la Nabothi (1-4)

  • Yezebeli apanga njama ya kumuua Nabothi (5-16)

  • Ujumbe wa Eliya dhidi ya Ahabu (17-26)

  • Ahabu ajinyenyekeza (27-29)

21  Baada ya hayo, jambo fulani lilitendeka kuhusiana na shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli; lilikuwa Yezreeli,+ kando ya jumba la Mfalme Ahabu, mfalme wa Samaria.  Ahabu akamwambia Nabothi: “Nipe shamba lako la mizabibu ili nilifanye kuwa shamba la mboga, kwa sababu liko karibu na nyumba yangu. Badala ya shamba hilo, nitakupa shamba bora zaidi la mizabibu. Au ukipenda, nitakulipa pesa zinazolingana na thamani yake.”  Lakini Nabothi akamwambia Ahabu: “Ni jambo nisiloweza kamwe kuwazia, kulingana na maoni ya Yehova, kukupa urithi wa mababu zangu.”+  Basi Ahabu akaingia nyumbani mwake, akiwa amesononeka na kuvunjika moyo kwa sababu ya jibu ambalo Nabothi Myezreeli alimpa aliposema: “Sitakupa urithi wa mababu zangu.” Kisha akalala kitandani mwake, akaugeuzia mbali uso wake, na kukataa kula.  Yezebeli mke wake+ akaingia ndani kumwona, akamuuliza, “Kwa nini umehuzunika* sana hivi kwamba unakataa kula?”  Akamjibu: “Ni kwa sababu nilimwambia Nabothi Myezreeli, ‘Niuzie shamba lako la mizabibu. Au ukipenda, nitakupa shamba lingine la mizabibu badala ya shamba hilo.’ Lakini akaniambia, ‘Sitakupa shamba langu la mizabibu.’”  Yezebeli mke wake akamwambia: “Je, si wewe unayetawala ukiwa mfalme wa Israeli? Inuka, kula chakula, moyo wako na uchangamke. Nitakupa shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli.”+  Basi Yezebeli akaandika barua kwa jina la Ahabu, akazipiga muhuri wa Ahabu+ na kuzituma barua hizo kwa wazee+ na wakuu walioishi katika jiji la Nabothi.  Aliandika hivi katika barua hizo: “Tangazeni watu wafunge, halafu mketisheni Nabothi mbele ya watu. 10  Nanyi muwaketishe watu wawili wasiofaa kitu mbele yake ili watoe ushahidi dhidi yake,+ wakisema, ‘Umemtukana Mungu na mfalme!’+ Kisha mtoeni nje na kumuua kwa kumpiga mawe.”+ 11  Basi watu wa jiji lake, wazee na wakuu walioishi katika jiji lake, wakafanya kama ilivyoandikwa katika barua ambazo Yezebeli aliwatumia. 12  Wakatangaza watu wafunge, kisha wakamketisha Nabothi mbele ya watu. 13  Ndipo watu wawili miongoni mwa watu wasiofaa kitu wakaja na kuketi mbele yake, nao wakaanza kutoa ushahidi dhidi ya Nabothi mbele ya watu, wakisema: “Nabothi amemtukana Mungu na mfalme!”+ Kisha wakamtoa nje ya jiji, wakamuua kwa kumpiga mawe.+ 14  Halafu wakamtumia Yezebeli ujumbe huu: “Nabothi ameuawa kwa kupigwa mawe.”+ 15  Mara tu Yezebeli aliposikia kwamba Nabothi amepigwa mawe akafa, akamwambia Ahabu: “Inuka, chukua shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli,+ ambalo alikataa kukuuzia, kwa maana Nabothi hayuko hai tena. Amekufa.” 16  Mara tu Ahabu aliposikia kwamba Nabothi amekufa, Ahabu aliondoka, akashuka kwenda kwenye shamba la mizabibu la Nabothi Myezreeli ili alichukue. 17  Lakini neno la Yehova likamjia Eliya+ Mtishbi, likisema: 18  “Ondoka, nenda ukutane na Ahabu mfalme wa Israeli huko Samaria.+ Yuko katika shamba la mizabibu la Nabothi, ameenda huko kulichukua. 19  Mwambie hivi: ‘Yehova anauliza hivi: “Je, umemuua mtu+ na kuchukua mali yake?”’+ Kisha mwambie, ‘Yehova anasema hivi: “Mahali ambapo mbwa waliramba damu ya Nabothi, ndipo watakapoiramba damu yako mwenyewe.”’”+ 20  Ahabu akamwambia Eliya: “Yaani umenipata, ewe adui yangu?”+ Akajibu: “Nimekupata. ‘Kwa sababu umeazimia* kutenda maovu machoni pa Yehova,+ 21  sasa ninakuletea msiba, nami nitafagia kabisa baada yako na kumwangamiza kila mwanamume* wa Ahabu,+ kutia ndani wasio na uwezo na walio dhaifu katika Israeli.+ 22  Nami nitaifanya nyumba yako iwe kama nyumba ya Yeroboamu+ mwana wa Nebati na kama nyumba ya Baasha+ mwana wa Ahiya, kwa sababu umenikasirisha na kusababisha Waisraeli watende dhambi.’ 23  Pia Yehova anasema hivi kumhusu Yezebeli: ‘Mbwa watamla Yezebeli katika shamba la Yezreeli.+ 24  Mtu yeyote wa Ahabu anayefia jijini mbwa watamla, na yeyote anayefia shambani ndege wa angani watamla.+ 25  Kwa kweli, hajawahi kamwe kutokea mtu yeyote kama Ahabu,+ aliyeazimia kabisa* kutenda maovu machoni pa Yehova, akichochewa na Yezebeli mke wake.+ 26  Alitenda kwa njia yenye kuchukiza kabisa kwa kufuata sanamu zenye kuchukiza,* kama Waamori wote walivyokuwa wamefanya, ambao Yehova aliwafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.’”+ 27  Mara tu Ahabu aliposikia maneno hayo, akararua mavazi yake na kuvaa nguo za magunia; akaanza kufunga na kulala chini katika nguo za magunia na kutembea kwa huzuni. 28  Kisha neno hili la Yehova likamjia Eliya Mtishbi: 29  “Je, umeona jinsi ambavyo Ahabu amejinyenyekeza kwa sababu yangu?+ Kwa sababu amejinyenyekeza mbele zangu, sitauleta msiba huo akiwa hai. Nitailetea nyumba yake msiba huo katika siku za mwanawe.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Kwa nini roho yako imehuzunika.”
Tnn., “umejiuza.”
Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.
Tnn., “aliyejiuza.”
Huenda neno la Kiebrania linahusiana na neno “mavi,” nalo hutumiwa kuonyesha dharau.