Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 12:1-33

  • Rehoboamu awajibu watu kwa ukali (1-15)

  • Makabila kumi yaasi (16-19)

  • Yeroboamu awekwa kuwa mfalme wa Israeli (20)

  • Rehoboamu aambiwa asipigane na Waisraeli (21-24)

  • Yeroboamu aanzisha ibada ya ndama (25-33)

12  Rehoboamu alienda Shekemu, kwa maana Waisraeli wote walikuwa wamekuja Shekemu+ kumfanya kuwa mfalme.+  Mara tu Yeroboamu mwana wa Nebati aliposikia habari hizo (bado alikuwa akiishi Misri kwa sababu alikuwa amemkimbia Mfalme Sulemani),+  wakawatuma watu waende kumwita. Kisha Yeroboamu na Waisraeli wote wakaja kwa Rehoboamu na kumwambia hivi:  “Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito.+ Lakini ukiufanya utumishi mzito wa baba yako kuwa mwepesi zaidi na kupunguza nira nzito* aliyotutwika, tutakutumikia.”  Ndipo akawaambia: “Nendeni, kisha mrudi baada ya siku tatu.” Basi watu wakaenda zao.+  Kisha Mfalme Rehoboamu akashauriana na wanaume wazee waliomtumikia Sulemani baba yake alipokuwa hai, akawauliza: “Mnanishauri niwape jibu gani watu hawa?”  Wakamjibu: “Leo ukiwa mtumishi wa watu hawa na kukubali ombi lao na kuwapa jibu linalofaa, watakuwa watumishi wako sikuzote.”  Hata hivyo, alikataa ushauri aliopewa na wanaume wazee, akashauriana na vijana wa rika lake na ambao sasa walikuwa watumishi wake.+  Aliwauliza: “Mnashauri tuwape jibu gani watu hawa ambao wameniambia, ‘Ifanye nira ambayo baba yako alitutwika iwe nyepesi zaidi’?” 10  Vijana hao wa rika lake wakamwambia: “Hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia watu hao waliokwambia, ‘Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito, lakini wewe unapaswa kuifanya kuwa nyepesi zaidi kwa ajili yetu’; hivi ndivyo unavyopaswa kuwaambia, ‘Kidole changu kidogo kitakuwa kinene kuliko kiuno cha baba yangu. 11  Baba yangu aliwatwika nira nzito, lakini mimi nitazidisha uzito wa nira yenu. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.’” 12  Yeroboamu na watu wote wakaja kwa Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyokuwa amesema: “Rudini kwangu siku ya tatu.”+ 13  Lakini mfalme akawajibu watu kwa ukali, akaukataa ushauri aliopewa na wanaume wazee. 14  Akawajibu kama alivyoshauriwa na vijana wa rika lake, na kusema: “Baba yangu aliifanya nira yenu kuwa nzito, lakini mimi nitazidisha uzito wa nira yenu. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.” 15  Basi mfalme hakuwasikiliza watu, kwa sababu Yehova ndiye aliyesababisha badiliko hilo la mambo,+ ili atimize neno ambalo Yehova alimwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kupitia Ahiya+ Mshilo. 16  Waisraeli wote walipoona kwamba mfalme amekataa kuwasikiliza, wakamwambia hivi mfalme: “Tuna ushirika gani na Daudi? Hatuna urithi wowote katika mwana wa Yese. Nendeni kwa miungu yenu, enyi Waisraeli! Sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi!” Ndipo Waisraeli wakarudi katika nyumba zao.*+ 17  Lakini Rehoboamu akaendelea kuwatawala Waisraeli walioishi katika majiji ya Yuda.+ 18  Kisha Mfalme Rehoboamu akamtuma Adoramu,+ aliyekuwa msimamizi wa watu waliofanya kazi ya kulazimishwa, lakini Waisraeli wote wakamuua kwa kumpiga mawe. Mfalme Rehoboamu akafaulu kupanda gari lake na kukimbilia Yerusalemu.+ 19  Na tangu siku hiyo Waisraeli wamekuwa wakiiasi+ nyumba ya Daudi. 20  Mara tu Waisraeli wote waliposikia kwamba Yeroboamu amerudi, wakamwita mbele ya kusanyiko, nao wakamweka kuwa mfalme wa Waisraeli wote.+ Hakuna yeyote aliyeifuata nyumba ya Daudi isipokuwa kabila la Yuda.+ 21  Rehoboamu alipofika Yerusalemu, mara moja aliikusanya nyumba yote ya Yuda na kabila la Benjamini, mashujaa 180,000 waliozoezwa,* ili wapigane na nyumba ya Israeli na kuurudisha ufalme kwa Rehoboamu mwana wa Sulemani.+ 22  Kisha neno hili la Mungu wa kweli likamjia Shemaya+ mtu wa Mungu wa kweli: 23  “Mwambie Rehoboamu mwana wa Sulemani mfalme wa Yuda na nyumba yote ya Yuda na Benjamini na watu wengine, 24  ‘Hivi ndivyo Yehova anavyosema: “Msipande kwenda kupigana na ndugu zenu Waisraeli. Kila mmoja wenu anapaswa kurudi nyumbani kwake, kwa maana nimesababisha mambo haya yatukie.”’”+ Basi wakalitii neno la Yehova na kurudi nyumbani, kama Yehova alivyowaambia. 25  Kisha Yeroboamu akalijenga* jiji la Shekemu+ katika eneo lenye milima la Efraimu na kuishi humo. Kutoka huko, akaenda kulijenga* jiji la Penueli.+ 26  Yeroboamu akasema moyoni mwake: “Sasa ufalme utarudi katika nyumba ya Daudi.+ 27  Watu hawa wakiendelea kupanda kwenda kutoa dhabihu katika nyumba ya Yehova huko Yerusalemu,+ mioyo ya watu hawa itamrudia pia bwana wao, Mfalme Rehoboamu wa Yuda. Naam, wataniua na kumrudia Mfalme Rehoboamu wa Yuda.” 28  Baada ya kushauriana, mfalme akatengeneza ndama wawili wa dhahabu+ na kuwaambia watu: “Inachosha sana kwenu kupanda kwenda Yerusalemu. Ndiye huyu hapa Mungu wenu, enyi Waisraeli, aliyewatoa nchini Misri.”+ 29  Kisha akamweka ndama mmoja kule Betheli,+ na mwingine akamweka kule Dani.+ 30  Na jambo hilo likawafanya watende dhambi,+ watu wakaenda mpaka Dani kuabudu ndama aliyekuwa huko. 31  Naye akajenga nyumba za ibada mahali pa juu na kuchagua makuhani kutoka miongoni mwa watu wa kawaida, ambao hawakuwa Walawi.+ 32  Pia, Yeroboamu akaanzisha sherehe katika mwezi wa nane, siku ya 15 ya mwezi huo, kama ile sherehe iliyokuwa ikifanywa kule Yuda.+ Kwenye madhabahu aliyojenga kule Betheli,+ alitoa dhabihu kwa wale ndama aliokuwa ametengeneza, na huko Betheli akaweka makuhani wahudumu mahali pa juu alipokuwa amejenga. 33  Katika siku ya 15 ya mwezi wa nane, mwezi aliojichagulia, akaanza kutoa dhabihu kwenye madhabahu aliyokuwa amejenga huko Betheli; akaanzisha sherehe kwa ajili ya Waisraeli, naye akapanda juu ya madhabahu ili kutoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu.

Maelezo ya Chini

Au “inayokandamiza.”
Tnn., “mahema yao.”
Tnn., “waliochaguliwa.”
Au “akaliimarisha.”
Au “kuliimarisha.”