Matendo 4:1-37

4  Sasa hao wawili walipokuwa wakisema na watu, wakuu wa makuhani na kapteni wa hekalu+ na Masadukayo+ wakawajia,  wakiwa wameudhika kwa sababu walikuwa wakiwafundisha watu na walikuwa wakiutangaza waziwazi ufufuo kutoka kwa wafu kwa kisa cha Yesu;+  nao wakawashika na kuwaweka katika kizuizi mpaka siku iliyofuata,+ kwa maana tayari ilikuwa jioni.  Hata hivyo, wengi kati ya wale waliokuwa wamesikiliza maneno hayo wakaamini,+ na hesabu ya wanaume ikawa karibu elfu tano.+  Siku iliyofuata kukawa na mkutano wa watawala wao na wanaume wazee na waandishi katika Yerusalemu+  (pia Anasi+ mkuu wa makuhani na Kayafa+ na Yohana na Aleksanda na wengi waliokuwa watu wa jamaa ya huyo mkuu wa makuhani),  nao wakawasimamisha katikati yao na kuanza kuuliza: “Mlifanya jambo hilo kwa nguvu gani au katika jina la nani?”+  Ndipo Petro, akiwa amejazwa roho takatifu,+ akawaambia: “Watawala wa watu na wanaume wazee,  ikiwa leo sisi tunahojiwa, juu ya msingi wa tendo jema kwa mtu mwenye kuugua,+ kuhusu ni nani amemponya mtu huyu, 10  acheni ijulikane kwenu nyote na kwa watu wote wa Israeli, kwamba katika jina la Yesu Kristo Mnazareti,+ ambaye mlimtundika mtini+ lakini ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu,+ kupitia kwake, mtu huyu anasimama hapa akiwa na afya mbele yenu. 11  Hilo ndilo ‘jiwe ambalo ninyi wajenzi mlilitendea kana kwamba si la maana ambalo limekuwa jiwe kuu la pembeni.’+ 12  Zaidi ya hayo, hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina+ lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo lazima sisi tupate kuokolewa.”+ 13  Sasa walipoona maneno ya waziwazi ya Petro na Yohana, na kufahamu kwamba walikuwa watu wasio na elimu na wa kawaida tu,+ wakaanza kustaajabu. Nao wakaanza kutambua juu yao kwamba walikuwa pamoja na Yesu;+ 14  nao walipokuwa wakitazama mtu aliyekuwa ameponywa akiwa amesimama pamoja nao,+ hawakuwa na jambo la kukanusha.+ 15  Kwa hiyo wakawaamuru waende nje ya jumba la Sanhedrini, nao wakaanza kushauriana, 16  wakisema: “Tutafanya nini na watu hawa?+ Kwa sababu, kwa kweli, ishara kuu imetukia kupitia kwao, ambayo ni wazi kwa wakaaji wote wa Yerusalemu;+ nasi hatuwezi kuikana. 17  Hata hivyo, ili isipate kusambazwa zaidi kotekote kati ya watu, acheni tuwaambie kwa vitisho wasiseme tena kamwe na mtu yeyote juu ya msingi wa jina hilo.”+ 18  Ndipo wakawaita na kuwaamuru wasiseme wala kufundisha popote juu ya msingi wa jina la Yesu. 19  Lakini Petro na Yohana wakajibu wakawaambia: “Kama ni jambo la uadilifu mbele za macho ya Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. 20  Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”+ 21  Kwa hiyo, walipokuwa wamewatisha zaidi, wakawafungua, kwa kuwa hawakupata msingi wowote wa kuwaadhibu na kwa sababu ya watu,+ kwa sababu wote walikuwa wakimtukuza Mungu juu ya jambo lililokuwa limetukia; 22  kwa maana mtu ambaye ishara hiyo ya kuponywa ilikuwa imetokea juu yake alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 40. 23  Baada ya kufunguliwa wakaenda kwa watu wao+ wenyewe na kuwaeleza mambo ambayo wakuu wa makuhani na wanaume wazee walikuwa wamewaambia. 24  Waliposikia hayo wakampaazia Mungu+ sauti zao kwa umoja na kusema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu,+ wewe Ndiye uliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo,+ 25  na ambaye kupitia roho takatifu ulisema kwa kinywa cha babu yetu Daudi,+ mtumishi wako, ‘Kwa nini mataifa yakawa yenye fujo na vikundi vya watu vikatafakari juu ya mambo matupu?+ 26  Wafalme wa dunia walichukua msimamo wao nao watawala wakajikusanya pamoja kama mtu mmoja dhidi ya Yehova na dhidi ya mtiwa-mafuta wake.’+ 27  Ijapokuwa hivyo, Herode na pia Pontio Pilato+ pamoja na watu wa mataifa na pamoja na vikundi vya watu wa Israeli kwa kweli walikusanyika pamoja katika jiji hili dhidi ya mtumishi wako mtakatifu+ Yesu, ambaye ulimtia mafuta,+ 28  ili afanye mambo ambayo mkono wako na shauri viliagiza kimbele yatukie.+ 29  Na sasa, Yehova, viangalie vitisho vyao,+ na kuwawezesha watumwa wako kuendelea kusema neno lako kwa ujasiri wote,+ 30  huku ukiunyoosha mkono wako ili kuponya na huku ishara+ nyingi na mambo ya ajabu yakitukia kupitia jina+ la mtumishi+ wako mtakatifu Yesu.” 31  Nao walipokuwa wameomba dua, mahali hapo walipokuwa wamekusanyika pamoja pakatikiswa;+ nao wote wakajazwa roho takatifu+ na wakawa wakisema neno la Mungu kwa ujasiri.+ 32  Zaidi ya hayo, umati wa waliokuwa wameamini ulikuwa na moyo na nafsi moja,+ na hakuna hata mmoja aliyekuwa akisema kwamba chochote kati ya vitu vilivyokuwa mali yake kilikuwa chake mwenyewe; bali walikuwa na vitu vyote kwa ushirika.+ 33  Pia, wakiwa na nguvu nyingi mitume wakaendelea kutoa ushahidi kuhusu ufufuo wa Bwana Yesu;+ na fadhili zisizostahiliwa kwa kadiri kubwa zilikuwa juu yao wote. 34  Kwa kweli, hapakuwa hata mmoja mwenye uhitaji kati yao;+ kwa maana wale wote waliokuwa na mashamba au nyumba walikuwa wakiviuza na kuleta thamani za vitu vilivyouzwa 35  nao walikuwa wakiziweka miguuni pa mitume.+ Na kila mmoja alikuwa akigawiwa,+ kulingana na uhitaji wake. 36  Kwa hiyo Yosefu, ambaye mitume walikuwa wakimwita Barnaba,+ jina ambalo linapotafsiriwa linamaanisha Mwana wa Faraja, Mlawi, mzaliwa wa Kipro, 37  akiwa na sehemu ya shamba, akaiuza na kuzileta pesa na kuziweka miguuni pa mitume.+

Maelezo ya Chini