Matendo 27:1-44

27  Basi kwa kuwa iliamuliwa tusafiri kwenda Italia,+ walikuwa wakikabidhi Paulo na pia wafungwa fulani wengine kwa ofisa-jeshi anayeitwa Yulio wa kikosi cha Augusto.  Tukapanda ndani ya mashua kutoka Adramitiamu, iliyokuwa karibu kusafiri mpaka kandokando ya pwani ya wilaya ya Asia, tukasafiri kwa mashua, naye Aristarko+ Mmakedonia kutoka Thesalonike alikuwa pamoja nasi.  Na siku iliyofuata tukashuka mpaka Sidoni, na Yulio akamtendea Paulo kwa fadhili za kibinadamu+ na kumruhusu aende kwa rafiki zake na kutunzwa nao.+  Tulipotoka huko tukasafiri chini ya Kipro, kwa sababu pepo zilikuwa zikitukabili;  nasi tukaendesha kupitia bahari kuu kandokando ya Kilikia na Pamfilia na kuegesha bandarini kule Mira katika Likia.  Lakini huko ofisa-jeshi akapata mashua kutoka Aleksandria+ iliyokuwa ikisafiri kwenda Italia, naye akatupandisha chomboni.  Ndipo, baada ya kusafiri kwa mashua polepole kwa siku kadhaa na kufika Kinido kwa shida, kwa sababu upepo haukuturuhusu tuendelee mbele, tukasafiri chini ya Krete katika Salmone,  tukapita kandokando ya pwani yake kwa shida tukafika mahali fulani panapoitwa Bandari Nzuri, ambapo jiji Lasea lilikuwa karibu na hapo.  Kwa kuwa muda mrefu ulikuwa umepita na kufikia sasa ilikuwa hatari kusafiri kwa sababu hata kufunga kwa siku ya upatanisho+ kulikuwa tayari kumepita, Paulo alitoa pendekezo, 10  akiwaambia: “Ninaona kwamba safari itakuwa na madhara na hasara kubwa si ya shehena na mashua tu bali pia ya nafsi zetu.”+ 11  Hata hivyo, ofisa-jeshi akawa anamsikiliza nahodha na mwenye meli badala ya mambo yaliyosemwa na Paulo. 12  Sasa kwa kuwa bandari hiyo haikufaa kukaa wakati wa majira ya baridi kali, walio wengi wakakata shauri kusafiri kutoka hapo, ili kuona kama wangeweza kwa njia fulani kufaulu kufika Feniki ili kukaa huko wakati wa majira ya baridi kali, ambayo ni bandari ya Krete inayofunguka kuelekea kaskazini-mashariki na kuelekea kusini-mashariki. 13  Zaidi ya hayo, upepo wa kusini ulipovuma kwa utulivu, walifikiri walikuwa wamefikia kusudi lao, nao wakang’oa nanga na kuanza kufuata pwani karibu na pwani ya Krete. 14  Hata hivyo, baada ya muda usiokuwa mrefu, upepo wenye tufani+ unaoitwa Euroakilo ukavuma kasi juu yake. 15  Kwa kuwa mashua ilishikwa na upepo wenye nguvu nayo haikuweza kushindana na upepo huo, tukaiachilia, nao ukatuchukua. 16  Basi tukasafiri upesi chini ya kisiwa fulani kidogo kinachoitwa Kauda, na bado ilikuwa vigumu kuiongoza kikamili mashua+ ndogo kwenye tezi. 17  Lakini baada ya kuiingiza ndani wakaanza kutumia misaada ili kuikaza mashua chini; nao wakiogopa kupanda mwamba katika Sirti, wakashusha vifaa vya kuendeshea na hivyo wakachukuliwa. 18  Lakini kwa sababu tulikuwa tukirushwarushwa kwa nguvu nyingi na tufani hiyo, siku iliyofuata tukaanza kupunguza uzito+ wa meli; 19  na siku ya tatu, kwa mikono yao wenyewe, wakatupa ayari za mashua hiyo. 20  Basi, wakati ambapo jua wala nyota hazikuonekana kwa siku nyingi, nayo tufani+ iliyokuwa juu yetu ikiwa si ndogo, mwishowe tukaanza kukata tumaini la kuokolewa. 21  Na baada ya kujiepusha na chakula kwa muda mrefu, Paulo akasimama katikati yao+ na kusema: “Mlipaswa kufuata shauri langu na kutosafiri katika bahari kutoka Krete na hivyo mwepuke kupatwa na madhara na hasara hii.+ 22  Hata hivyo, sasa ninapendekeza mchangamke, kwa maana hakuna nafsi kati yenu itakayopotea, mashua tu ndiyo itakayopotea. 23  Kwa maana usiku huu malaika+ wa Mungu ambaye mimi ni mali yake na ambaye mimi ninamtolea utumishi mtakatifu, alisimama karibu nami,+ 24  akisema, ‘Usiogope, Paulo. Utasimama mbele ya Kaisari,+ na, tazama! Mungu amekupa wale wote wanaosafiri pamoja nawe.’ 25  Kwa hiyo changamkeni; kwa maana ninamwamini Mungu+ kwamba itakuwa kama vile ambavyo nimeambiwa. 26  Hata hivyo, lazima tutupwe pwani juu ya kisiwa fulani.”+ 27  Sasa usiku wa kumi na nne ulipofika nasi tukawa tukirushwa huku na huku katika bahari ya Adria, katikati ya usiku mabaharia wakaanza kudhani walikuwa wakikaribia nchi fulani. 28  Nao wakapima kina kwa bildi na kupata kuwa ni pima 20; kwa hiyo wakaendelea mbele umbali mfupi na wakatia bildi tena na kupata kuwa ni pima 15. 29  Na kwa sababu ya kuogopa kwamba tungeweza kutupwa mahali fulani juu ya miamba, wakatupa nanga nne kutoka kwenye tezi na kuanza kutamani kupambazuke. 30  Lakini mabaharia walipoanza kutafuta kukimbia katika mashua na kushusha mashua ndogo ndani ya bahari kwa kusingizia kuwa walikusudia kuzishusha nanga kutoka kwenye omo, 31  Paulo akamwambia ofisa-jeshi na askari-jeshi: “Watu hawa wasipobaki katika mashua, ninyi hamwezi kuokolewa.”+ 32  Ndipo askari-jeshi wakakata kamba za mashua+ ndogo na kuiacha ianguke. 33  Sasa karibu na mapambazuko Paulo akaanza kuwatia moyo wote wale chakula, akisema: “Leo ni siku ya kumi na nne ambayo mmekuwa mkikesha na kukaa bila chakula, mkiwa hamjala chochote. 34  Kwa hiyo ninawatia moyo mle chakula, kwa ajili ya usalama wenu; kwa maana hata unywele+ mmoja wa kichwa cha mmoja kati yenu hautaangamia.” 35  Baada ya kusema jambo hilo, pia akachukua mkate, akamshukuru+ Mungu mbele yao wote akaumega na kuanza kula. 36  Kwa hiyo wote wakachangamka na kuanza kula chakula wao wenyewe. 37  Basi, sote pamoja, sisi nafsi tuliomo ndani ya mashua tulikuwa 276. 38  Walipokuwa wameshiba chakula, wakaanza kupunguza uzito+ wa mashua kwa kutupa ngano baharini. 39  Mwishowe kulipopambazuka, hawakuweza kuitambua nchi hiyo lakini walikuwa wakiangalia ghuba fulani yenye pwani, na hapo ndipo walipoazimia, ikiwa wangeweza, kuipeleka mashua pwani.+ 40  Kwa hiyo, wakizikata nanga, wakaziacha zianguke ndani ya bahari, wakati huohuo wakifungua amari za makasia ya mtambo wa usukani na, baada ya kutweka tanga la mbele kwenye upepo, wakaenda pwani. 41  Walipotua juu ya fungu la mchanga lililorundikwa na bahari pande zote mbili, wakaiendesha meli juu ya mwamba na omo ikakwama na kukaa bila kuondoleka, lakini tezi likaanza kuvunjika vipande-vipande kwa nguvu nyingi.+ 42  Ndipo askari-jeshi wakaazimia kuwaua wafungwa, ili yeyote asiogelee na kutoroka. 43  Lakini ofisa-jeshi akataka kumpitisha Paulo akiwa salama naye akawazuilia wasitimize kusudi lao. Naye akawaamuru wale ambao wangeweza kuogelea wajitupe baharini na kufika kwenye nchi kavu kwanza, 44  na wale wengine wafanye hivyo, wengine wakiwa juu ya mbao na wengine juu ya vitu fulani kutoka katika mashua. Na hivyo ikawa kwamba wote wakafika salama kwenye nchi kavu.+

Maelezo ya Chini