Matendo 7:1-60
7 Lakini kuhani mkuu akasema: “Je, mambo haya ndivyo yalivyo?”
2 Akasema: “Wanaume, akina ndugu na akina baba, sikieni. Mungu wa utukufu+ alimtokea babu yetu Abrahamu alipokuwa Mesopotamia, kabla ya kuanza kukaa Harani,+
3 naye akamwambia, ‘Toka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na uje mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.’+
4 Ndipo akatoka nchi ya Wakaldayo na kuanza kukaa Harani. Na kutoka huko, baada ya baba yake kufa,+ Mungu akamfanya abadili makao yake mpaka kwenye nchi hii ambamo ninyi sasa mnakaa.+
5 Na bado hakumpa urithi wowote ndani yake, hapana, hata upana wa wayo mmoja wa mguu;+ bali aliahidi kumpa hiyo kuwa miliki,+ na uzao wake baada yake,+ alipokuwa bado hana mtoto.+
6 Zaidi ya hayo, Mungu alisema hivi, kwamba uzao wake ungekuwa wakaaji wageni+ katika nchi ya kigeni+ na watu hao wangewafanya watumwa na kuwatesa kwa miaka mia nne.+
7 ‘Na taifa ambalo watalitumikia nitalihukumu,’+ Mungu akasema, ‘na baada ya mambo hayo watatoka na kunitolea utumishi mtakatifu mahali hapa.’+
8 “Alimpa pia agano la tohara;+ na kwa hiyo akamzaa Isaka+ na kumtahiri siku ya nane,+ na Isaka akamzaa Yakobo, na Yakobo akawazaa wale vichwa vya familia kumi na wawili.+
9 Na wale vichwa vya familia wakamwonea Yosefu wivu+ na kumuuza Misri.+ Lakini Mungu alikuwa pamoja naye,+
10 naye akamkomboa kutoka katika dhiki zake zote na kumpa neema na hekima machoni pa Farao mfalme wa Misri. Naye akamweka aongoze Misri na nyumba yake yote.+
11 Lakini njaa ikaja juu ya Misri yote na Kanaani, hata dhiki kuu; na mababu zetu hawakuwa wakipata chakula chochote.+
12 Lakini Yakobo akasikia kulikuwa na vyakula Misri+ naye akawatuma mababu zetu mara ya kwanza.+
13 Na mara ya pili Yosefu akajulishwa kwa ndugu zake;+ na ukoo wa familia ya Yosefu ukajulishwa kwa Farao.+
14 Kwa hiyo Yosefu akatuma watu wamwite Yakobo baba yake na jamaa zake wote kutoka hapo,+ wenye kufikia hesabu ya nafsi 75.+
15 Yakobo akashuka kuingia Misri.+ Naye akafa;+ na pia mababu zetu,+
16 nao wakahamishwa mpaka Shekemu+ na kulazwa katika kaburi+ ambalo Abrahamu alikuwa amenunua kwa bei fulani kwa fedha kutoka kwa wana wa Hamori katika Shekemu.+
17 “Wakati ulipokuwa ukikaribia kwa ajili ya utimizo wa ahadi ambayo Mungu alikuwa amemtangazia Abrahamu waziwazi, watu wakaongezeka na kuzidi katika Misri,+
18 mpaka akainuka mfalme tofauti juu ya Misri, ambaye hakujua habari za Yosefu.+
19 Huyo akatumia hila ya serikali juu ya jamii+ yetu na kulazimisha kimakosa akina baba wawatupe watoto wao wachanga, ili wasihifadhiwe hai.+
20 Katika wakati huo maalumu Musa akazaliwa,+ naye alikuwa mwenye sura nzuri+ machoni pa Mungu. Naye akanyonyeshwa kwa miezi mitatu nyumbani mwa baba yake.
21 Lakini alipotupwa, binti ya Farao akamwokota na kumlea kama mwana wake mwenyewe.+
22 Kwa sababu hiyo Musa akafundishwa hekima+ yote ya Wamisri. Kwa kweli, yeye alikuwa mwenye nguvu katika maneno+ na matendo.
23 “Sasa wakati wa mwaka wake wa 40 ulipokuwa ukitimia, wazo likaingia moyoni mwake, awakague ndugu zake, wana wa Israeli.+
24 Naye alipomwona mtu fulani akitendewa isivyo haki, akamtetea na kulipiza kisasi kwa ajili ya yule mwenye kutendewa vibaya kwa kumpiga na kumuua Mmisri.+
25 Alikuwa akidhani ndugu zake wangefahamu ya kwamba Mungu alikuwa akiwapa wokovu kwa mkono wake,+ lakini hawakufahamu hilo.
26 Na siku iliyofuata akawatokea walipokuwa wakipigana, naye akajaribu kuwapatanisha tena wawe na amani,+ akisema, ‘Wanaume, ninyi ni ndugu. Kwa nini mnatendeana isivyo haki?’+
27 Lakini yule aliyekuwa akimtendea jirani yake isivyo haki akamsukuma mbali, akisema, ‘Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mtawala na mwamuzi juu yetu?+
28 Unataka kuniangamiza vile ulivyomwangamiza yule Mmisri jana, sivyo?’+
29 Kwa maneno hayo Musa akakimbia na kuwa mkaaji mgeni katika nchi ya Midiani,+ ambako alizaa wana wawili.+
30 “Na miaka 40 ilipotimia, malaika akamtokea katika mwali wa moto wa mti wa miiba katika nyika ya Mlima Sinai.+
31 Sasa Musa alipouona akastaajabia maono hayo.+ Lakini alipokuwa akikaribia ili kuchunguza, sauti ya Yehova ikaja,
32 ‘Mimi ni Mungu wa mababu zako, Mungu wa Abrahamu na wa Isaka na wa Yakobo.’+ Akitetemeka, Musa hakuthubutu kuchunguza zaidi.
33 Yehova akamwambia, ‘Vua viatu kutoka miguuni, kwa maana mahali ambapo umesimama ni udongo mtakatifu.+
34 Kwa hakika nimeona jinsi watu wangu walio Misri+ wanavyotendewa vibaya, nami nimesikia kuugua+ kwao na nimeshuka ili kuwakomboa.+ Na sasa njoo, nitakutuma uende Misri.’+
35 Musa huyo, ambaye hao walimkana, wakisema, ‘Ni nani aliyekuweka wewe kuwa mtawala na mwamuzi?’+ mtu huyo Mungu alimtuma+ aende akiwa mtawala na pia mkombozi kwa mkono wa malaika aliyemtokea katika mti wa miiba.
36 Mtu huyo aliwaongoza watoke+ baada ya kufanya mambo ya ajabu na ishara katika Misri+ na katika Bahari Nyekundu+ na katika nyika kwa miaka 40.+
37 “Huyo ndiye Musa aliyewaambia wana wa Israeli, ‘Mungu atawainulia kutoka kati ya ndugu zenu nabii kama mimi.’+
38 Huyo ndiye+ aliyekuja kuwa katikati ya kutaniko+ katika nyika pamoja na malaika+ aliyesema naye juu ya Mlima Sinai na pamoja na mababu zetu, naye akapokea maneno matakatifu+ yaliyo hai ili awape ninyi.
39 Mababu zetu walikataa kumtii, bali wakamsukuma kando+ na katika mioyo yao wakageuka kurudi Misri,+
40 wakimwambia Haruni, ‘Tufanyie miungu iende mbele yetu. Kwa maana huyo Musa, aliyetuongoza kutoka katika nchi ya Misri, hatujui lililompata.’+
41 Kwa hiyo wakafanya ndama siku hizo+ wakailetea hiyo sanamu dhabihu na kuanza kujifurahisha katika kazi za mikono yao.+
42 Kwa hiyo Mungu akageuka na kuwakabidhi+ watoe utumishi mtakatifu kwa jeshi la mbinguni, kama vile ambavyo imeandikwa katika kitabu cha manabii,+ ‘Je, mimi ndiye mliyetolea wanyama na dhabihu nyikani kwa miaka 40, Ee nyumba ya Israeli?+
43 Bali mlichukua hema la Moloki+ na nyota+ ya mungu Refani, maumbo mliyoyafanya ili kuyaabudu. Kwa sababu hiyo nitawahamishia+ ninyi ng’ambo ya Babiloni.’
44 “Mababu zetu walikuwa na hema la ushahidi nyikani, kama vile alivyotoa maagizo alipokuwa akisema na Musa ili kulifanya kulingana na mfano aliokuwa ameuona.+
45 Na mababu zetu waliolirithi waliliingiza pamoja na Yoshua+ ndani ya nchi iliyomilikiwa na mataifa,+ ambayo Mungu aliyafukuza kutoka mbele ya mababu zetu.+ Lilibaki humo mpaka siku za Daudi.
46 Alipata kibali+ machoni pa Mungu na kuomba pendeleo la kuandaa makao+ kwa ajili ya Mungu wa Yakobo.
47 Hata hivyo, Sulemani alimjengea nyumba.+
48 Ingawa hivyo, Aliye Juu Zaidi hakai katika nyumba zilizofanywa kwa mikono;+ kama vile nabii anavyosema,
49 ‘Mbingu ni kiti changu cha ufalme,+ nayo dunia ni kiti cha miguu+ yangu. Mtanijengea nyumba ya aina gani? Asema Yehova. Au mahali pangu pa kupumzika pako wapi?+
50 Mikono yangu ilifanya vitu vyote hivi, sivyo?’+
51 “Ninyi watu wenye shingo ngumu na wasiotahiriwa katika mioyo+ na masikio, sikuzote mnaipinga roho takatifu; kama mababu zenu walivyofanya, ndivyo ninyi mnavyofanya.+
52 Ni yupi kati ya manabii ambaye mababu zenu hawakumtesa?+ Ndiyo, waliwaua+ wale waliotangaza kimbele kuhusu kuja kwa Aliye mwadilifu,+ ambaye ninyi sasa mmemsaliti na kumuua,+
53 ninyi mliopokea Sheria kama ilivyopitishwa na malaika+ lakini hamkuishika.”
54 Basi, waliposikia mambo hayo wakahisi wamechomwa mioyoni+ mwao na kuanza kumsagia+ meno yao.
55 Lakini yeye, akiwa amejaa roho takatifu, akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume+ wa Mungu,
56 naye akasema: “Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka+ na Mwana wa binadamu+ akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume+ wa Mungu.”
57 Ndipo wakapaaza sauti ya juu na kuweka mikono yao juu ya masikio yao,+ wakamrukia wote pamoja.
58 Na baada ya kumtupa nje ya jiji,+ wakaanza kumtupia mawe.+ Na wale mashahidi+ wakaweka chini mavazi yao ya nje miguuni pa kijana aliyeitwa Sauli.+
59 Nao wakaendelea kumtupia Stefano mawe huku akiomba na kusema: “Bwana Yesu, pokea roho yangu.”+
60 Ndipo akapiga magoti yake, akapaaza sauti kubwa: “Yehova, usiwahesabie dhambi hii.”+ Na baada ya kusema hayo akalala usingizi katika kifo.